Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kutoa mchango wangu kwa njia ya maandishi. Aidha, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kazi ngumu lakini nzuri wanayoifanya. Mchango wangu utajielekeza kwenye mambo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya hifadhi; kwa takwimu nilizonazo, Tanzania ina eneo la uhifadhi ambalo ni asilimia 38 ya eneo lote la nchi. Hili ni eneo kubwa sana na nchi yetu ni moja ya nchi iliyo na eneo kubwa sana la uhifadhi duniani. Wakati wa uhuru nchi yetu ilikuwa na watu karibu milioni kumi tu, lakini hivi leo watu tunakaribia milioni 50. Eneo la makazi ya watu haliongezeki, watu wakiongezeka na shughuli zao za kiuchumi, kijamii nazo zinaongezeka na kwa sababu shughuli hizi zinafanyika kwenye ardhi, lazima maeneo ya uhifadhi yatalazimika kutumiwa na watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali ni kwamba Serikali iangalie upya maeneo ya uhifadhi kwa kuyapunguza ili yatumike kwa shughuli za watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mapato ya utalii na idadi ya watalii; mapato yatokanayo na utalii bado ni madogo. Nakubaliana na hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwamba juhudi kubwa zinafanyika ili kufikisha kipato kitokanacho na utalii hapo kilipo. Kama nchi yetu ni ya pili kwa kuwa na vivutio bora vya utalii duniani baada ya Brazil, kwa nini mapato yetu kama nchi yakabaki kidogo namna hii? Mheshimiwa Waziri ni vyema akatoa maelezo juu ya jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mapato yetu ni kidogo kwa sababu idadi ya watalii wanaotembelea maeneo yetu ya utalii ni wachache. Ni kweli watalii wamekuwa wakiongezeka mwaka hadi mwaka, lakini ongezeko hili ni dogo kuwezesha kutupatia mapato makubwa ambayo yanatokana na utalii. Ninamtaka Mheshimiwa Waziri atueleze ana mkakati gani mpya wa kuongeza idadi ya watalii na hatimaye kutuongezea mapato kama nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la migogoro ya wafugaji na hifadhi; ipo migogoro kati ya wafugaji na Hifadhi za Taifa kwa sababu wafugaji wanapopata matatizo ya malisho na maji wanatafuta malisho na maji kwenye hifadhi. Nakubali huku ni kuvuruga sheria, lakini wafugaji hawa wanapovunja sheria kwa kuingiza mifugo yao kwenye hifadhi, Serikali nayo kwa kutumia wafanyakazi wake nao wavunje sheria kwa kuua ng‟ombe ama mifugo yao? Nao pia wavunje sheria kwa kuchoma nyumba za wanavijiji, wafugaji ambao wanaishi kando kando ya hifadhi? Wafanyakazi hao nao waombe rushwa kutoka kwa wafugaji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima Serikali i-balance, hapa sheria zifuatwe, lakini with a human face. Umefika wakati sasa maeneo ya wafugaji yatengwe na kuwekewa miundombinu muhimu inayohitajika ikiwepo utatuzi wa tatizo la malisho ya mifugo ya wafugaji. Serikali ikae kitako kwa kuhusisha Wizara zinazohusika ili kutatua migogoro hii na nchi ipate mabadiliko ambayo wananchi wanayahitaji. Wizara na Serikali ziache kufanyakazi kwenye silo, Serikali ni moja lazima ije na mkakati wa pamoja ili kuondoa udhia huu kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.