Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Rais kuikabidhi Wizara hii kwa Mheshimiwa Profesa Jumanne Maghembe, Mbunge ambaye ni mbobevu wa hifadhi za wanyamapori na misitu. Naamini tembo wa Selous Game Reserve sasa wamepata mlinzi na naahidi kwa eneo la Namtumbo nitamsaidia kwa uwezo wangu wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba atusaidie wakazi wa Wilaya ya Namtumbo katika masuala yafuatayo:-
(i) Vijiji saba vya Jumuiya ya Mbarang‟andu na vijiji vingine vinavyounda jumuiya mbili, nyingine za Kimbanda na Kusangura vinahitaji kuhuisha mipaka yao ya WMA ili kutoa fursa ya ardhi ya kilimo. Wananchi wameongezeka, wanahitaji maeneo zaidi ya kilimo kwa ajili ya kujikimu kimaisha. Muda wa kupitia upya mipaka hiyo ilikubalika miaka kumi na hadi sasa miaka imezidi bila kufanyika kwa makubaliano hayo ya kupitia upya mipaka hiyo ya WMA.
(ii) Watumishi wa Selous Game Reserve wameonekana wakiweka beacons ndani ya maeneo ya vijji vya Mputa, Luhimbalilo, Luhangano, Mhangazi, Kitanda, Nangero, Mtumbatimaji na Nambecha na hivyo kutishia ama kuenea uvumi wa maeneo yao kuchukuliwa, yaani kupanua mipaka ya hifadhi na kuingilia WMA na mashamba ya wanavijiji bila taarifa yoyote kwao. Nitashukuru kama wananchi hao watahakikishiwa usalama wa maeneo yao.
(iii) Vijiji vinavyoizunguka Selous Game Reserve, Undendeule Forest Reserve na Lukwika Forest Reserve wala Halmashauri yetu ya Wilaya Namtumbo hainufaiki na uwepo wa hifadhi hizo. Namuomba Mheshimiwa Waziri atufikirie kama ilivyo kwa wenzetu wanaozunguka hifadhi za Kaskazini.
(iv)Operesheni Tokomeza imewaacha baadhi ya wakazi wa Namtumbo bila silaha zao walizokuwa wakizimiliki kihalali kwa mujibu wa sheria na walielekezwa wakazikabidhi kwa uchunguzi na hadi leo hawajarudishiwa bila maelezo yoyote. Naomba Mheshimiwa Waziri silaha hizo warudishiwe waliokuwa wakizimiliki ili waendelee kuzitumia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Waziri kwa kutusikiliza na kutujali. Tafadhali Waziri chapa kazi ukimshirikisha Naibu wako Mheshimiwa Engineer Ramo Makani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilichangia kwa maandishi masuala manne yaliyojitokeza kwa nguvu kipindi cha Kampeni ya Uchaguzi Mkuu. Leo asubuhi Mkuu wa Wilaya ameniomba nikueleze yafuatayo ambayo kama Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama yanasumbua sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana hiyo alitembea Kijiji cha Likuyu Mandela ambacho asili yake ni waliokuwa wakimbizi kutoka Msumbiji na wamepata uraia wa Tanzania. Tembo wanaingia majumbani wanaipua hata mahindi yaliyoko jikoni. Mazao yao yamekuwa yakiliwa kila mwaka na maombi yao ya kulipwa fidia au kifuta jasho hayajashughulikiwa toka mwaka 2011. Wiki iliyopita mkazi mmoja ameuawa na tembo. Hiyo ni moja kati ya matukio ya karibuni ya madhara ya tembo ambao idadi yao imeongezeka sana baada ya ujangili kudhibitiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba hoja za wakazi hao wa kijiji cha Likuyu Mandela zipatiwe ufumbuzi. Aidha, kijiji hicho kisaidiwe chakula na itafutwe njia nzuri ya kuwazuia wanyamapori kutovuka mipaka ya hifadhi hata kwa kutumia uzio wa umeme kama inavyofanyika katika nchi za wenzetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hoja hii iunganishwe na hoja zangu nyingine nne za jana nilizochangia vilevile kwa maandishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawasilisha na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.