Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba kuchangia juu ya umuhimu wa Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro. Mlima Kilimanjaro kimekuwa chanzo kikuu cha utalii katika nchi yetu hivyo ni vizuri Serikali ikaamua kwa makusudi kuhakikisha mazingira yanayotunza Mlima Kilimanjaro ni mazuri. Yapo matatizo yafuatayo ambayo ni hatari kwa hifadhi ya mlima:-
(i) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni tatizo la moto. Mara kwa mara hutokea moto katika Mlima Kilimanjaro, ni vyema Serikali ikadhibiti vyanzo vya moto na tabia zinazosababisha moto. Lakini pia ni vyema Serikali kufuatilia kwa makini juu ya tuhuma za watumishi na baadhi ya wafanyakazi wasio waaminifu kujihusisha na tuhuma za kusababisha moto kwa sababu zao binafsi za kujinufaisha kimaslahi.
(ii) Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, lipo tatizo kubwa la mifugo kuwapo ndani ya hifadhi na kuharibu sana mazingira na uoto wa asili wa Mlima Kilimanjaro ambao husababisha ukosefu wa mvua, pia katika vyanzo vya mito vinavyoanzia kandokando ya Mlima Kilimanjaro.
(iii) Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, lipo pia tatizo kubwa la ukataji wa magogo na upasuaji wa mbao katika misitu inayozunguka Mlima Kilimanjaro. Aidha, ukataji mkubwa wa magogo na upasuaji miti unatokana na matumizi makubwa ya chainsaw ambazo nyingi zilitoka Kenya mara baada ya udhibiti mkubwa wa upasuaji mbao na magogo uliofanywa ndani ya nchi ya Kenya.
Aidha, yapo mahitaji ya badhi ya viwanda vinavyohitaji magogo, mbao na kadhalika na matokeo yake wananchi wa kawaida wanachukua tender ya kusambaza/kutoa magogo na mbao ambayo wanalazimika kuingia katika misitu ya hifadhi. Naishauri Serikali kwa nguvu zinazostahili izuie kwa nguvu zoezi hili la ukataji wa magogo na mbao katika maeneo ya Mlima Kilimanjaro ambapo inaharibu na kuuwavyanzo vya mito na chemchemi za maji.
(iv) Mheshikiwa Mwenyekiti, tatizo la kilimo pia ni moja kati ya vyanzo vikubwa vya uharibifu wa mazingira. Bado hatujawa na udhibiti mkubwa wa watu wanaolima na kuharibu mazingira katika vyanzo vya maji na maeneo ya ardhi oevu. Ni vyema Serikali ikajipanga vizuri na kusimamia Sheria za Kilimo zikiwepo zinazozuia kulima katika kingo za mito, vyanzo vya maji, na kadhalika. Sheria ya mita 60 ni muhimu izingatiwe.
(v) Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo la nusu maili (half mile)ambalo ni buffer zone kwa ajili ya Mlima Kilimanjaro. Dhamira kubwa ya eneo hili la kuwa kinga ya Mlima Kilimanjaro imepotea kwa watu kuvamia eneo hili kwa kilimo, ujenzi na upandaji wa miti usio rafiki na mazingira ya Mlima Kilimanjaro. Ni vyema Serikali ikafanya maamuzi ya makusudi ya kulinda eneo hili kwa ajili ya hifadhi ya Mlima Kilimanjaro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni na mapendekezo yangu ya jumla:-
(a) Juhudi za upandaji wa miti katika eneo lote linalozunguka Mlima Kilimanjaro, ni vyema Serikali ifanye juhudi ya hali ya juu ya suala hili.
(b) Ufanyike udhibiti madhubuti katika kuzuia kilimo holela na hifadhi ya ardhi.
(c) Udhibiti wa ukataji miti uwe wa kina na kuzisimamia sheria zote.
(d) Udhibiti wa mifugo inayoingia msituni uwe wa nguvu zaidi na adhabu kali kwa wanaovunja sheria zichukuliwe.
(e) Uaminifu na uadilifu na kufanya kazi kwa weledi ni muhimu kwa watumishi wa KINAPA na TANAPA kwa ujumla, Serikali ione namna ya kuimarisha na kuhakikisha weledi kwa watumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri maalum ni kuwa utalii wa Mlima Kilimanjaro ni muhimu na unakubalika sana duniani, lakini lazima tufikiri zaidi. Wapo ambao wangependa kuupanda Mlima Kilimanjaro, lakini wanashindwa kutokana na sababu mbalimbali ikiwepo afya ya mtu, umri wa mtu, mapenzi ya kutembea/interest, uwezo wa kutembea kwa kupanda mlima kwa siku tano na kadhalika, ili watu wengi waweze kupanda na kuona Mlima Kilimanjaro. Upo uwezekano wa kutengeneza mnara/tower au reli/treni ya juu ya mlima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vyema Serikali ikaandaa mazingira haya kwa kuweka vitu vitakavyowawezesha watalii wengi wanaovutiwa na Mlima Kilimanjaro kuja kutalii kwa njia nyingine na si ya kuupanda mlima kwa kutembea; njia hii itawezesha kuongeza watalii wengi zaidi ya mara mbili ya watalii wanaokuja kupanda Mlima Kilimanjaro. Uzoefu wa China kutengeneza tower ndefu ungeweza kutumika kujenga tower katika maeneo yanayozunguka Mlima Kilimanjaro na watalii kuja kwenye tower na kutembelea mlima kwa kutumia tower hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, dhamira ya Manispaa ya Songea ni kuuingiza Mji wa Songea katika sekta ya utalii ili kuweza kuufanya uwe mji wa utalii. Songea ina vivutio vingi vya utalii ambavyo inabidi viendelezwe na kutangazwa; mambo kama:-
(i) Vita vya Majimaji, watu/mababu zetu walionyongwa katika mapambano na ukoloni wa Kijerumani.
(ii) Kumbukumbu za mashujaa na mapambano ya Wajerumani na mababu zetu.
(iii) Maeneo ya mapango na maporomoko ya maji.
(iv) Mila na desturi za makabila mbalimbali ya Songea, vyakula, malazi, mavazi, zana za kazi, uwindaji, utunzanji wa chakula, ngoma, tamaduni za malezi bora na kadhalika.
(v) Michezo ya jadi; mieleka, mashindano ya mila, ngoma za kivita, michezo ya kishujaa na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara ione uwezekano wa kutuma ujumbe Songea, tutakaokaa nao pamoja ili kupanga na kuchambua mambo yanayoweza kutangazwa na kuanza kazi ya kutangaza utalii wa Songea na kuanzisha utalii katika Mji wa Songea. Aidha, ni vizuri kwa Wizara kwa kushirikiana na Manispaa ya Songea kuanzisha Kituo cha Taarifa za Utalii (Tourism Information Centre) ili baada ya kuvibainisha vituo hivyo vya utalii na mambo ya utalii kuwe na kituo cha kupokelea na kutolea taarifa za utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa ushirikiano kati ya Serikali Kuu na Manispaa ya Songea tuweze kuvitangaza vivutio hivyo kwa njia mbalimbali. Dhamira kuu ni kukuza utalii na kuupelekea Mji wa Songea kuwa mji wa utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.