Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Selemani Jumanne Zedi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukene

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi jioni ya leo niweze kuchangia mjadala huu ambao uko mezani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitajielekeza kwenye maeneo kadhaa ambayo ningependa nitoe mchango kuhusu hotuba ya mapendekezo ya bajeti iliyotolewa na Waziri wa Fedha na Mipango. Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua vizuri sana kwa kuja na nguvu sana katika eneo la kudhibiti ubadhirifu katika matumizi ya fedha za umma na mimi naunga mkono kabisa kwa sababu ni jambo jema. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baada ya kupitia hotuba ya mapendekezo ya Waziri wa Fedha nimeona kuna contradiction ya ajabu. Kwa sababu huwezi kupambana na ubadhirifu wa matumizi ya fedha za umma kwa kauli tu za kisiasa. Ni lazima uwe na vitendo ambavyo kweli vitapelekea kupambana na ubadhirifu huu wa fedha za umma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna taasisi muhimu ya kimkakati katika kupambana na ubadhirifu wa fedha za umma basi taasisi hiyo ni Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali yaani CAG. Contradiction ninayoisema ni kwamba kwa upande mwingine Serikali inasema tumedhamiria kupambana na ubadhirifu wa matumizi ya fedha za umma, lakini kwa upande mwingine taasisi ambayo ndiyo taasisi ya mkakati, ndiyo hasa kiini, ndiyo key institute katika kupambana na ubadhirifu ambayo ni CAG imepangiwa fedha ambayo kwa kweli haiwezi kabisa kutimiza majukumu yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii tunayokwenda nayo ambayo inakwisha mwezi huu wa Sita ni bajeti ya shilingi trilioni 22. Katika bajeti hii CAG tumemtengea shilingi bilioni 74 ili kukagua shilingi trilioni 22. Bajeti hii ambayo tunaijadili sasa ni ya shilingi trilioni 29 lakini CAG tumempangia shilingi bilioni 44 tu. Huu ndiyo nauita mkanganyiko na contradiction ya ajabu kwa sababu kwenye bajeti ya shilingi trilioni 22 CAG tumempa shilingi bilioni 74 kwa ajili ya kukagua lakini kwenye bajeti ya shilingi trilioni 29 ambapo kuna ongezeko la shilingi trilioni saba tumepunguza hela ya kumwezesha kukagua sasa tunategemea nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwangu mimi hii ni contradiction na naona kabisa kama hatutafanya chochote, basi kauli za kusema tumejipanga kupambana na ubadhirifu ni kauli tu za kisiasa na ambazo hatutafikia matokeo tunayotaka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo napenda kuchangia, nimeangalia katika hotuba Mheshimiwa Waziri wa Fedha amependekeza kufuta utaratibu wa retention kwenye taasisi za Serikali ambazo kimsingi zilikuwa zinaruhusiwa kubakiza fedha ambazo zinakusanywa ili ziweze kutekeleza majukumu yake. Mojawapo kati ya taasisi hizo ni Shirika la Maendeleo la Petrol (TPDC).
Mheshimiwa Naibu Spika, sipingani na wazo la kufuta retention, lakini angalizo ninalolitoa ni kwamba, kuna taasisi nyingine muhimu, ni taasisi za kimkakati kwa mfano TPDC. Najaribu ku-imagine endapo Wizara ya Fedha kupitia Hazina itakapotekeleza agizo la kutoruhusu TPDC kuwa na retention ikachukua fedha zote ambazo TPDC inakusanya ikazipeleka Mfuko Mkuu wa Serikali halafu ikashindwa au ikachelewesha kupeleka fedha TPDC kwa mujibu wa bajeti yake na ikaifanya TPDC ikashindwa kufanya baadhi ya majukumu, nakuhakikishia tutapoteza fedha nyingi kuliko ambazo tunadhani tutaziokoa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, TPDC ndiyo jicho la Serikali kwenye shughuli zote za gesi. Sasa hivi tumefanikiwa kugundua kiasi kikubwa sana cha gesi lakini walio kwenye biashara ya gesi wote ni wawekezaji binafsi na TPDC ndiyo mbia ambaye anasimamia kwa upande wa Serikali. Moja kati ya kazi zake ni kufanya ukaguzi wa shughuli zinazofanywa na wawekezaji wa gesi ili kujua mapato wanayopata na kujua mgao wa Serikali kama ni sahihi. Kwa hiyo, TPDC wasipokuwa na fedha za kufanya kazi hii, nakuhakikishia tutapigwa bao na hao wawekezaji wa gesi, fedha nyingi sana zitachukuliwa na lile lengo letu la kusema kwamba eti wasibaki na retention ili Serikali iweze kupata fedha nyingi halitafikiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuwe makini na angalizo langu hapa ni kwamba, tuhakikishe Mheshimiwa Waziri wa Fedha kupitia Hazina upelekaji (disbursement) wa fedha kwenye taasisi kwa kweli ni jambo ambalo lisije likawa kama utaratibu ulivyo sasa kwa sababu tutaingia kwenye athari kubwa kuliko ambavyo tunatarajia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo napenda nichangie ni suala la value for money kwa miradi ambayo imekamilika. Kuna miradi mingi nchini kwetu ambayo imekamilika lakini haijaweza kuleta manufaa kwa wananchi kama ambavyo imetarajiwa. Kuna maeneo mengi utakuta madaraja, miradi ya umwagiliaji mabilioni yametumika lakini haifanyi kazi kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jimboni kwangu mimi Serikali imetumia fedha nyingi sana kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika wameweza kujenga zahanati za kisasa katika Kata ya Itobo na Tarafa ya Bukene na wameweza kufunga vifaa vya kisasa vya upasuaji. Hata hivyo, sasa hivi ni karibu mwaka mzima umepita majengo ya kisasa yamekamilika, vifaa vya kisasa vya upasuaji vimefungwa huduma za upasuaji hazijaweza kuanza kufanyika. Kwa hiyo, mabilioni yametumika lakini wananchi hawanufaiki chochote na mabilioni hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna haja ya Serikali kujipanga kupitia Wizara ya Fedha na Wizara husika kuhakikisha kwamba pale ambako tumewekeza fedha nyingi na miradi imekamilika, ifanye kazi sasa wananchi waweze ku-enjoy matunda hayo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kushirikiana na Mheshimiwa Waziri wa Afya na TAMISEMI, naomba kabisa kupata suluhisho kuhusu huduma za upasuaji katika vituo vya afya vya Itobo na Bukene ambapo fedha nyingi zimetumika, huduma hii ianze kutolewa, ni mwaka sasa. Vifaa vilivyofungwa vinakaribia kuanza kuota kutu na mabilioni ya fedha yametumika, hatuwezi kukubali hali kama hiyo. Hivyo, nashauri huduma ya upasuaji iweze kuanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningependa niliwekee mkazo ni suala la upelekaji wa umeme REA III. Hili ni muhimu sana, nimeona Serikali imetenga fedha za kutosha na nina imani kwa namna ambavyo Wizara ya Nishati na Madini imejipanga na nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri alifanya ziara kule maeneo ya kwetu na aliongozana na mkandarasi na kuhimiza.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika baadhi ya maeneo matunda yameanza kuonekana na nina uhakika miradi ambayo iko katika REA awamu ya III itatekelezeka na wananchi waweze kupata manufaa. Kama tunataka kukuza ajira hasa maeneo ya vijijini basi umeme vijijini ni lazima uwepo kwa ajili ya shughuli za kusindika mazao ya kilimo ili yaweze kuongezewa thamani na yaweze kuuzwa sokoni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.