Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nachukua nafasi hii na kwa sababu nasema kwa mara ya kwanza, nawashukuru sana wananchi wangu wa Songea Mjini kwa ushindi mkubwa walionipatia. Ninachotaka kuwahakikishia ni kwamba, nimekuja kama Mwakilishi wao na sitawaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sikupata bahati ya kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Rais, lakini labda nianze na hilo kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais katika ukurasa wa 20, pamoja na hotuba nzuri sana aliyoitoa, lakini ukurasa wa 20 alikuwa amezungumzia kero kwa wananchi, hasa wafanyabiashara ndogo ndogo kuhusiana na ushuru wanaoutoa. Naungana na Mheshimiwa Rais na kwa kweli naomba wenzetu wafanye utaratibu wa kuhakikisha ushuru huu unafutwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijue, kwa sababu ninachokumbuka, ni miaka ya nyuma hivi karibuni walifuta ushuru wa kero kwa wananchi wote kwa maana ya kwamba ushuru uliokuwa unakusanywa kwa njia ya kero ulifutwa na Serikali ilikuwa inatoa ruzuku kwenye Halmashauri za Wilaya ili kufidia ushuru huo wa kero. Sasa sielewi ule ushuru wa kero umeishia wapi. Kwa nini Halmashauri zetu zimeingia tena kuwa-charge wafanyabiashara ndogo ndogo wa mchicha, vitumbua, Mama Ntilie ambapo sasa imekuwa ni kero kubwa mno! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kitu kimoja hapa, inachekesha kweli! Ukiangalia leseni za biashara zinazotoa Sh. 70,000/= kwa mwaka, ukalinganisha na ushuru wanaotoa akinamama Nntilie, unakuta Mama Ntilie anagharamia gharama kubwa zaidi kuliko mtu anayelipa ushuru wa Sh. 70,000/=. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hesabu za haraka haraka, ni kwamba anayelipa leseni ya Sh. 70,000/= maana yake ukigawanya kwa miezi 12 na ukagawanya kwa siku 30 maana yake mfanyabiashara huyu wa duka au wa mgahawa analipa kwa siku Sh. 194/=. Wakati huyu Mama Ntilie anayelipa Sh. 400/= kama ushuru, ukifanya hesabu za siku maana yake unamkuta analipa ushuru kwa mwaka 144,000/= akimzidi mfanyabiashara wa kawaida wa duka au mgahawa.
Kwa hiyo, ni kitu kinachoshangaza sana. Ni vizuri tukiangalie vizuri; na kwa kweli kama alivyosema Mheshimiwa Rais, nadhani umefika wakati sasa tuwafutie ushuru huu ili wananchi wafanye biashara zao vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mpango, kwanza nami naungana na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa kazi nzuri aliyoifanya. Mpango huu umezungumzia sana mahusiano ya kibiashara, ya kiuchumi kati ya Tanzania na nchi jirani, lakini katika Mpango ule umezungumzia sana mipaka ya Kenya, mipaka ya Uganda na mipaka ya nchi nyingine. Haujazungumzia kabisa mpaka wa Kusini mwa Tanzania, Mkoa wa Ruvuma ukihusika na hasa kwa nchi ya Msumbiji na nchi ya Malawi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mpango huu utambue kuwapo kwa barabara inayounganisha Tanzania na Msumbiji, kupitia Songea Mjini kwenye eneo la Likuyufusi kwenda kwenye eneo la Mkenda, Kaskazini ya Msumbiji. Barabara hii haijaingizwa na wala haijazungumzwa. Ni vizuri iingizwe na izungumzwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile upanuzi wa uwanja wa ndege wa Songea Mjini ambao ungeweza kusaidia sana suala la wafanyabiashara na wananchi kutoka nchi jirani wanaopenda kutembelea Tanzania, hasa kutoka Msumbiji na Malawi, kuweza kutumia ndege zitakazotoka Songea kwenda Dar es Salaam kufanya shughuli mbalimbali za kibiashara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru vilevile kwa kazi nzuri ya Serikali inayofanywa hasa ya kutengeneza barabara ya kutoka Mtwara kwenda Mbambabay. Barabara hii bado kuna maeneo mawili haijakamilika na wala haijashughulikiwa. Ukitoka Namtumbo kwenda Tunduru kuna Makandarasi wanashughulikia, lakini kati ya Luhira na Ruhuiko, Mjini Songea, wananchi wamewekewa „X,’ wamefanyiwa tathmini, lakini mpaka sasa hawajalipwa fidia zao na kwa hiyo, wanaishi katika maisha ya kutokuwa na uhakika watahama lini. Kwa hiyo, naomba Serikali ifanye utaratibu wa haraka ili watu wanaostahili kulipwa fidia katika eneo hilo waweze kulipwa fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile bado kuna kipande kimoja hakijajengwa kati ya Mbinga na Mbambabay. Naomba Serikali ione namna ya kufanya katika hiyo sehemu ili kuhakikisha inatengenezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kuna mwenzetu mmoja amezungumza habari ya reli; nashukuru kwa mpango kabambe wa Serikali wa kujenga reli ya kati kwa kiwango cha Standard gauge, lakini vilevile kwa mpango kabambe ambao upo katika Kitabu chetu cha Mwelekeo wa Uchumi kuhusu barabara ya Mtwara – Mbambabay.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba basi, Serikali ione namna ya kufanya utaratibu wa kuhakikisha reli hii inajengwa ili kuweza kuimarisha uchumi katika Mikoa ya Kusini, hasa kutokea kule Mbambabay. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala lingine. Kwa muda mrefu sana wananchi wa Mkoa wa Ruvuma na Songea kwa ujumla tumekuwa tukiahidiwa kupatiwa umeme wa Grid ya Taifa kutoka Makambako kuja Songea, lakini sasa kila mwaka linazungumzwa hili suala, lakini bado halijapatiwa ufumbuzi.
Kwa hiyo, naiomba Serikali ifanye utaratibu na itupe uhakika hili suala la umeme kati ya Makambako na Songea litakamilika lini na kwa hiyo, lini utaanza utekelezaji wa suala hilo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho, naomba nizungumzie juu ya suala la EPZA. Katika Taarifa ya Mheshimiwa Dkt. Mpango, amezungumzia EPZA katika maeneo mengi sana, lakini Jimboni kwangu Songea kuna wananchi katika maeneo ya Mwenge Mshindo, Luhila Kati, Kilagano, Ruawasi na Ruhuiko, hawa watu wamechukuliwa maeneo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu hawa ni zaidi ya 2,200 na wamechukuliwa ekari zaidi ya 5,000 kwa ajili ya kuweka EPZA, lakini nasikitika kwamba mpaka sasa watu waliolipwa ni wachache sana, hata kiwango cha fedha walicholipwa ni mwaka 2008. Wamelipa 2015, kiwango kile hakilingani na hali halisi ya sasa na vilevile wanatakiwa kuhama kwenye maeneo yale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo inasababisha kero kwa wananchi wangu na vilevile kuhakikisha kuendeleza umaskini, kwa sababu hawawezi kujiendeleza kiuchumi, hawawezi kujenga nyumba, lakini hawana mahali pa kwenda palipoandaliwa na Serikali na pesa waliyopata haiwawezeshi kuweza kwenda kuweka makazi katika maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kwa kutumia nafasi hii naiomba sana Serikali, hebu imalize tatizo hili la wananchi hao niliowataja katika eneo la Mwenge Mshindo ili tuweze kupata maendeleo, wananchi waweze kujiendeleza wakiwa na uhakika wanakwenda wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii niseme, kwa jinsi taarifa ilivyoandaliwa na kama tutazingatia haya ambayo tumeyaomba Waheshimiwa Wabunge, basi nachukua nafasi hii kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)