Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii na mimi nitoe mchango wangu kwenye Wizara hii ya Maliasili. Wizara ya Maliasili ni Wizara ambayo nilikuwa naisubiri kwa hamu sana kwa sababu asilimia 60 ya Wilaya ya Liwale ni Mbuga ya Selous. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina wasiwasi na weledi, ufahamu na nia ya Mheshimiwa Waziri. Tunalo tatizo kama Watanzania, tunazo fursa nyingi sana Watanzania, lakini maisha yetu fursa hizi hazijawahi kutusaidia. Hivi najaribu kujiuliza nini tatizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufahamu wangu mdogo tatizo la Watanzania ni kwamba tumepoteza uzalendo wa nchi yetu, tumetawaliwa na ubinafsi. Hii ndiyo sababu kubwa inayotufanya tushindwe kufikia malengo yetu pamoja na kuwa na rasilimali za kutosha katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye vivutio vya utalii hasa malikale. Hapa tunalo tatizo la Watanzania kupoteza historia ya nchi yetu. Tunashindwa kutambua vivutio vilivyopo kwenye nchi yetu ni kwa sababu watu tumepoteza historia ya nchi yetu, hatujui historia ya nchi yetu, tumepoteza hata jiografia ya nchi yetu. Natoa wito kwa Waziri wa Elimu aimarishe somo la historia na jiografia pengine vizazi vijavyo vitaweza kukumbuka haya ninayoyasema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kuisahau Liwale kama utaikumbuka vita ya Majimaji. Lipo boma pale la Mjerumani linaitwa Boma la Mdachi, boma lile pale mpaka leo ziko picha za wahanga wa vita ya Majimaji, ziko sanamu za wahanga wa vita ya Majimaji. Nani analikumbuka Boma la Liwale leo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Liwale tunao mlima ule tunauita Mlima Lukundi, uko Lilombe, mlima ambao ulikuwa na volcano iliyolala, nani anaijua hii? Tumepoteza historia. Naomba turudi kwenye historia, tutaweza tu kuzikumbuka hizi rasilimali zetu kama tutakwenda na historia ya nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Hifadhi ya Selous, asilimia 60 ya Wilaya ya Liwale imezungukwa na Mbuga ya Selous katika vijiji vya Mpigamiti, Barikiwa, Ndapata, Kimambi na Tukuyungu, lakini kuwepo kwetu Selous hakujatusaidia chochote. Nimezunguka katika vijiji hivi nilivyovitaja hatuna alama yoyote kuonesha kwamba sisi tuko karibu na Selous. Hatuna hoteli, hatuna barabara, hatuna miundombinu yoyote wala hatuna kiwanja cha ndege.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie kwa Kusini nzima kwa upande wa utalii tumeiacha nyuma. Lindi hakuna hoteli, Mtwara hakuna hoteli. Mtwara ndiko kuna uwanja wa ndege, lakini siyo ule wa Kimataifa kama ambavyo viwanja vingine vipo. Sasa tunategemea ile rasilimali ya Kusini, ule utalii wa Kusini ni nani atakuja kuukumbuka? Kama Mjerumani anaijua Kusini kwa nini Watanzania tusiijue?
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mji wa Liwale kuna kumbukumbu ya Mikukuyumbu, pale ndipo ambapo mmisionari wa kwanza kuja Pwani ya Afrika Mashariki waliuwawa pale. Mpaka leo Wafaransa wanakuja Liwale, wanakuja Mikukuyumbu kuzuru pale, lakini Watanzania hatuna habari hiyo, tumepoteza historia yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu askari wa wanyamapori, mimi nina wasiwasi na askari wa wanyamapori, aidha kwa sababu ya kutokutunzwa vizuri wanafanya haya mambo makusudi kuwachonganisha Serikali na wananchi. Kwa sababu vitendo wanavyovifanya askari wa wanyamapori havilingani na ubinadamu. Mimi nasema hivyo kwa ushahidi, ninayo picha hapa, huyu ni Mwenyekiti wa Kitongoji wa Kijiji cha Kichonda, hana mkono wa kulia, amekatwa mkono mnamo tarehe 08 Septemba, 2015 tukiwa kwenye kampeni na kesi yake imefutwa tarehe 08 Februari, 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kesi hii kisa chake ni nini, huyu amekatwa mkono akiwa nyumbani kwake. Askari wa wanyamapori wametoka porini wamemfukuza mtu na pikipiki wamesema ameingia pale kijijini wanataka kwenda ku-search. Wanakivamia kile kijiji kufanya searching nyumba kwa nyumba. Mwenyekiti wa Kitongoji akatoka akawauliza, ninyi mmekujaje hapa? Mbona hamna kibali cha polisi? Mbona hamjasindikizwa na polisi? Mbona hamjaja ofisini? Imekuwaje muwaingilie watu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo ni kosa lake lililomfanya akose mkono na file la kesi yote ninalo hapa. Hii kesi imefutwa na Wakili wa Serikali. Wakili wa Serikali anasema silaha zile zilikuwa ni zaidi ya moja, kwa hiyo, haijulikani katika zile silaha ni ipi iliyomjeruhi huyu mkono, yule mshtakiwa ameshindwa kumtia hatiani kuona kwamba je, ni bunduki yake au bunduki nyingine? Ndiyo kesi ikafutwa hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema hawa askari wa wanyamapori wana ajenda ya siri na Serikali yenu, inawezekana hamuwahudumii vizuri, wanafanya mambo kuwachonganisha ndiyo maana watu wengine wote hapa watasema, utampaje adhabu mtu afanye mapenzi na mti ina uhusiano gani? Tunaomba hawa askari waangaliwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upande wa TFS. Jamani TFS ni taasisi ya Serikali, lakini hii tuiangalie, hawa TFS kwa jinsi nilivyowaona wao kazi yao ni moja tu, kufanya udalali wa mbao na mali za misitu, hawana kazi nyingine wanayoifanya. Ukiwauliza mna mikakati gani ya kuendeleza misitu, hawajui chochote. Wao kazi yao ni kugonga mbao, kugonga mali za misitu, basi wamemaliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala hili la kitanda. Tunaomba hili suala la kitanda mliangalie. Kwa nini Kusini leo hii tumetengeneza vijana wajiajiri, wana viwanda vyao vidogo vidogo vya mbao, lakini havina soko. Ukinunua kiti Liwale, ukinunua kiti Kusini huwezi kukisafirisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hatujui kwamba zile mbao zote wanazotengeneza furniture ni za wizi, maana haiwezekani? Watu wanakwenda mpaka kwenye majumba, kwenye paa. TFS wanafuata mbao kwenye paa zinashushwa. Sasa mbao zimefikaje kule? Hili ni suala ambalo tunatakiwa tuliangalie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mgogoro kwa upande wa Liwale. Mgogoro ule umetengenezwa kati ya Hifadhi ya Selous pamoja na Kijiji cha Kikulyungu, huu mgogoro ni wa muda mrefu sana. Tatizo lake ni kwamba huu mgogoro wakati walikuja kutengeneza barabara wakasema tutengeneze barabara ili tuweze kufanya patrol, lakini badala yake leo wanasema ule ndiyo mpaka wa Selous. Hata GN hawana, lakini ukienda kuwauliza hakuna wanachofanya zaidi ya kupiga watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuambie hiki Kijiji cha Kikulyungu leo askari hakuna anayekanyaga, hivi vijiji nimevitaja hapo zaidi ya vitano, ina maana vijiji vyote hivi vikifunga njia Selous askari wa wanyamapori hawaingii. Tutafikia huko iwapo huu mgogoro hautaweza kutatuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi sasa kwenye wanyamapori, tembo, simba pamoja na nguruwe. Kule kwetu ukisikia njaa Liwale imeletwa na nguruwe, ukisikia njaa Liwale imeletwa na tembo, simba kule Liwale ni kama mbwa au kama paka wako wengi sana, tunaomba mje mtusaidie. Tunapokwenda pale kituoni kuomba msaada tunapovamiwa na simba wanatuambia usafiri hawana. Hawana askari wakutosha, watu wetu wanateseka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi kabla sijaja Bungeni nilikwenda kwa Mhifadhi wa Kanda anaitwa Salum, nikamwambia Salum kinachokubakiza hapa ni uvumilivu tu wa hawa watu, siku watakapokataa huna kazi hapa. Haiwezekani watu wanauwawa, haiwezekani watu mazao yao yanaliwa wewe unakuja hapa unaleta nahau. Nikamwambia Salum tafadhali, siku nitakayokuja kusema nimechoka, huna salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mtusaidie, Mikoa ya Kusini mtuwekee hata Chuo kimoja cha Misitu.