Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nichangie katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kumteua Profesa Jumanne Maghembe kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii. Tunamtambua Mheshimiwa Maghembe yeye ni profesa, ni mtalaam na tuna imani naye sana kwamba ataweza kuingoza vizuri Wizara hii. Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wake wote wanatosha na wanafaa kuiendesha Wizara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wengine ni Walimu tumetoka mashuleni, tunafundisha watoto nidhamu na nini wafanye au ni wakati gani wazungumze na mazungumzo hayo yatolewe kwa wakati gani? Tunakwazika, tunachanganyikiwa tunapoona zinatolewa sentensi nyingine hazieleweki ndani ya Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa nirudi kwenye hoja yangu. Wabunge wenzangu wamechangia mengi sana, lakini naomba nichangie katika eneo la misitu. Serikali ilikuwa na nia njema sana ya kuhifadhi maeneo ya ardhi yetu kwa kuweka misitu kwa akiba ya baadaye lakini pia katika kusaidia kuboresha mazingira lakini kila panapokuwa na jambo jema halikosi kuwa na ubaya ndani yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hizi hifadhi kwa mfano sisi tunaotoka maeneo ya Mbagala kuna hifadhi ya Mwandege, hifadhi hii haiendelezwi, haina usafi, matokeo yake imekuwa ni makazi ya majambazi. Majambazi yanakuja yanaua watu Mbagala, Temeke, Vituka huko yanakimbilia kwenda kujificha katika msitu huu wa Mwandege. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima nitoe pongezi za wazi kwa Kamanda wangu wa Polisi wa Mkoa wa Dar es Salaam, Kamanda Siro, amekuwa akifanya operesheni na katika operesheni yake idadi kubwa ya majambazi, majangili, magaidi, yamekamatwa katika msitu huu wa Mwandege uliopo Mkuranga. Hili sasa limekuwa tatizo badala ya raha. Kweli tuna nia njema ya kuhifadhi msitu ule lakini kwa hali ilivyofikia sasa hivi msitu ule ni tatizo kwa wakazi wa Dar es Salaam hususan wakazi wa maeneo ya Mbagala. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kuna changamoto nyingi sana katika maeneo haya lakini niiombe Serikali sasa hivi Mkoa wa Dar es Salaam una matatizo makubwa ya ardhi lakini pia kuna msongamano wa magari usiokwisha katika maeneo ya Mbagala. Niiombe kabisa Serikali kwa nia njema kwa nini wasipunguze eneo la msitu huu wakatengeneza kituo kikubwa cha mabasi kuondoa ule msongamano uliko pale Mbagala Rangitatu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo hivi huu msitu mwisho wake ni nini? Msitu huo umekuwa ukiingiliwa na wakazi kwenye maeneo yote ya pembezoni lakini wakati watu wale wanajenga nyumba Serikali inawaangalia, kesho na keshokutwa Serikali inakuja kuwavunjia zile nyumba, hawaoni kwamba wanawaonea wale wananchi? Dar es Salaam imejaa, maeneo ya ujenzi yamekuwa machache watu wanaanza kumega kidogokidogo pembeni mwa msitu ule, Serikali inawaona, Maafisa Misitu wapo hakuna wanachowaambia. Sasa mimi kama Mbunge ole wenu mkawaambie wale watu waje wavunje nyumba zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie gharama za tozo za misitu. Katika maeneo ya Mkuranga kwenye kituo cha Mkuranga ukitaka kupitisha kitanda kimoja gharama yake unalipia Sh.120,000/=, kitanda hicho kiwe cha zamani, kiwe kipya au kabati liwe la zamani au liwe jipya. Sasa Mkoa wa Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani maeneo ya Mkuranga umeungana, mtu anaweza kuhama kwenye nyumba Mkuranga akahamia Mbagala Temeke, akahama Mwandege akahamia Kongowe. Sasa hizi gharama wakati mtu anahamahama atakuwa anatozwa Sh.120,000/= kila anapohama kutoka huku kwenda kule, hii kweli ni sawa, huu siyo uonevu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iangalie hiyo sheria inavyosema kwamba watu wanapotoa kitanda au mazao yoyote ya misitu kutoka huku kwenda huku kulipa gharama kubwa. Kitanda cha futi tatu hapa Dodoma kinauzwa Sh.180,000/= wewe unalipiwa ushuru Sh.120,000/= hivi jamani hii ni kweli! Niiombe kabisa Serikali iangalie eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwenye manunuzi ya mkaa, unakuja pale Mkuranga ukitoka Rufiji unakuta kuna barrier kibao, mbona wenzetu huku Dodoma hakuna barrier za aina ile? Kwa nini kule kumekuwa barriers hizo kila sehemu unatozwa tozo mpaka unachanganyikiwa. Niombe hilo nalo liangaliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niingie kwenye eneo la utalii. Nitazungumzia utalii wa mambokale au wa maeneo ya kihistoria. Kuna maeneo ya kihistoria yanapotea, maeneo kama Bagamoyo, Kaole, Kunduchi, Isimila, Olduvai Gorge, Mapango ya Amboni, Mikindani, Kilwa Kisiwani, Songomnara, yote hayo ni maeneo ya kihistoria ambayo kama yataboreshwa yangeweza kutuletea mapato makubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo haya hayawekewi bajeti nzuri ya kuyaendeleza matokeo yake yanasambaratika, urithi ule wa kihistoria unasambaratika. Kwa hiyo, niiombe Serikali iweke bajeti ya maeneo hayo. Pia maeneo haya hayana information yoyote, hujui hiki kiko wapi wala kile kiko wapi. Kwa hiyo, niiombe Serikali iyatolee maelezo maeneo haya lakini pia iyatangaze. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda kwenye nchi za wenzetu, kwa mfano unakwenda India, unakuta ushawishi mkubwa, wewe kama mgeni unaambiwa nenda Taj Mahal, huelewi, mara nyingine unafuata tu mkumbo lakini sisi mbona tumekuwa kimya! Mtalii anakuja hapa, hakuna maelezo yoyote, hakuna promotion yoyote, unaingia kwenye ndege mpaka unafika Dar es Salaam hata huambiwi kwenye ndege Dar es Salaam utakumbana na kitu gani cha kitalii au ukaone maeneo gani ya kitalii, hili kwa kweli ni tatizo. Niiombe sasa Serikali yetu ibadilike, itangaze vyanzo vyake vya utalii vizuri ili wageni wanapoingia wavitambue na waende wakavitembelee. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Mkoa wangu wa Dar es Salaam kuwa mji wa kihistoria. Hakuna ambaye hafahamu kwamba Dar es Salaam ndiyo mji mkuu kuliko mikoa yote ya Tanzania lakini wapi Dar es Salaam imewekwa, wapi Dar es Salaam imepangwa kiutalii, tujue Dar es Salaam hii inakwendaje au tunamshawishije mtu wa kutoka nje akiingia Dar es Salaam aweze kutambua kwamba anaingia kwenye mji mkuu, mji bora, mji ambao una mambo yote muhimu, hata uhuru wa nchi hii bendera yake ilipandishwa katika Mkoa wa Dar es Salaam, Uwanja wa Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali, najua mpango huu ulizungumzwa hapa lakini ukaishia, je, imepanga mkakati gani wa kuitangaza Dar es Salaam sasa? Tunataka Dar es Salaam uwe mji wa kiutalii na utangazike na watu walioko nje wautambue. Ndiyo wenye uwanja mkubwa wa Kimataifa, Serikali imejenga ule uwanja, uwanja ule ni wa nini, wa kushusha na kupandisha tu, ni lazima ulete soko la watalii. Kwa hiyo, niiombe Serikali ipange mpango mkakati wa kuitangaza Dar es Salaam kama mji wa kitalii.