Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona na mimi nichangie katika bajeti hii muhimu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nianze na suala la Mkaguzi na Mdhibiti wa Serikali (CAG) kwamba pesa alizotengewa shilingi bilioni 44.7 ni pesa ambazo haziwezi zikamfanya afanye kazi yake kwa ufanisi. Tunapozungumza matatizo yaliyoko kwenye Halmashauri zetu tunayatambua na Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua kwamba ni Serikali ambayo imekuja kudhibiti ufisadi, sasa huyu mtu ambaye ndiye anayetambua ngazi ya mafisadi katika ngazi ya Halmashauri na kwenye taasisi tunapompa fungu dogo maana yake tusitarajie kwamba hata yale majipu yatakuja kupasuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumeona kwamba ofisi hii tangu imeanza kufanya kazi imekuwa inafanya kazi nzuri sana, kazi ambayo kila mwaka ilikuwa inatoa tija na ilikuwa inaleta mwanga hata kwenye Halmashauri zetu na walikuwa wanatujengea uwezo hata Waheshimiwa Wabunge kupitia Kamati hizi za LAAC namna ambavyo tunaweza kudhibiti mianya ya pesa za Serikali ambazo zinapotea kupitia Halmashauri zetu.
Kwa hiyo, nitoe rai kwa Waziri wa Wizara husika aliangalie suala hili kwa jicho la tahadhari sana kwamba kama tutamnyang’anya CAG uwezo maana yake ufisadi uliotamaliki katika Halmashauri zetu utaendelea zaidi kutafuna miradi mbalimbali inayoelekea katika Halmashauri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili nizungumzie suala la gratuity (mafao haya ya Ubunge). Mimi niseme kwamba Mheshimiwa Waziri amewahisha shughuli, suala la mwaka 2020 analizungumza leo, niungane na wenzangu kusema kwamba anatu-beep Wabunge. Niseme Sheria Namba 4 ya mwaka 1999 inazungumzia wigo mpana wa hawa wanasiasa ambao walikuwa wamesamehewa hii kodi. Kwa nini wawe Wabunge peke yao, hili ni suala la kutufanya tuamini kwamba kweli anatu-beep. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niseme kwa kuwa kodi hii ya mwendo kasi ambayo anajaribu kwenda nayo atukimbize kwa miaka minne ambayo haina tija kwa bajeti ya mwaka huu basi alitafakari kwa kina sana na aangalie hivi vilio vya hawa Waheshimiwa Wabunge sisi huko majimboni kila jambo ni la kwetu.
Vipaimara vinatuhusu, Maulid tunamaliza sisi, kukiwa na watoto kwenye chanjo, kwenye mwenge, kwenye kila kitu sisi ndiyo tunaohusika. Kwenye majimbo huko michezo inabembwa na Wabunge na hata ukitoka kwenye mageti yetu sasa hivi pale unakuta wauza mipira wote wamejaa kwenye mageti wanasubiri zianze Jimbo Cup, utashangaa mara Mhagama Cup, Mwinyi Cup, Cosato Chumi Cup yote haya ni matatizo ambayo yanawasibu Wabunge. Naamini hata kule Mbeya mwaka huu utasikia Tulia Ackson Cup. Sasa Mheshimiwa Waziri tunakuomba sana uliangalie hili kwa jicho la tahadhari. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye tozo ya utalii ya asilimia 18 kwenye VAT kwenye suala la usafirishaji, hili nalo ni eneo ambalo lazima tuliangalie kwa jicho la tahadhari sana. Wenzetu Kenya miundombinu yao ya utalii ni wezeshi sana, Shirika la Ndege linawa-support sana katika utalii sisi bado ndiyo kwanza tumepanga tununue ndege tatu za kuweza ku-boost eneo letu la utalii.
Ningemshauri Waziri kwamba angalau tuende taratibu, hii VAT tunayotaka kuiweka kwenye tozo ya usafirishaji ya utalii hebu kwanza twende kwa tahadhari. Sasa hivi kutokana na nchi jirani ya Kenya kutokuwa na usalama wa kutosha kutokana na mashambulizi ya magaidi wa Al-Shabab sisi tuna advantage nzuri ya kuteka hili soko. Kwa hiyo, ni vizuri tusiongeze gharama za ziada, twende hivi hivi kwanza soko letu liwe madhubuti mbele ya safari huko tunaweza tukaangalia maeneo gani tunaweza tukaboresha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala zima la reli ya Tanga – Moshi - Arusha - Musoma. Tunapozungumzia msongamano mkubwa wa mizigo na magari katika Bandari ya Dar es Salaam tiba pekee ni kuiwezesha reli ya Tanga kufanya kazi inavyotakiwa. Tunashukuru tumepata neema ya bomba la kusafirisha gesi ghafi kutoka Ziwa Albert kule Uganda mpaka Bandari ya Tanga. Sambamba na hili bomba la mafuta tungeweza kuboresha Bandari ya Tanga ili mizigo ya nchi ya Uganda pamoja na Sudan Kusini iweze kupitia Bandari ya Tanga. Tukipitisha mizigo katika bandari hii tutakuwa tumeimarisha uchumi wa Mikoa ya Kanda ya Kaskazini mpaka kule Musoma na tutakuwa tumewawezesha wananchi wote ambao wanapitiwa na hii reli ya Tanga - Arusha - Musoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la afya. Afya yetu ya msingi inaanzia katika ngazi ya zahanati, lakini pia tunavyo vituo vya afya vingi sana katika nchi yetu. Pamoja na nia nzuri ya Wizara ya Afya kwamba watakuwa wanaleta sera kwamba kila Halmashauri iwe na hospitali ambayo inaweza ikawa na ngazi ya Hospitali ya Wilaya basi lazima pia waviangalie vituo vyetu vya afya. Kule Mlalo tunacho kituo kikubwa cha afya kinatoa huduma za upasuaji, lakini kinakosa miundombinu ya wodi za wagonjwa lakini pia miundombinu wezeshi kama ambulance kwa ajili ya kuwasafirisha hawa wagonjwa wanaofanyiwa operesheni kama ita-fail katika kituo kile cha afya.
Kwa hiyo, niiombe Wizara pamoja na kwamba safari hii wametenga takribani shilingi trilioni 1.9 ambayo ni sawa na asilimia 92 basi tujitahidi bajeti inayokuja mwakani angalau tufike asilimia 15 ili kufikia yale Maazimio ya Abuja ili tuweze kuhudumia wananchi wetu vile ambavyo inapaswa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza pia Wizara kwa kukufuta kodi kwenye vifaa vya walemavu. Mwalimu Nyerere aliwahi kusema ukitaka usawa wa binadamu ndugu zetu walemavu tuwaajiri. Kwa hiyo, niipongeze Wizara kwa kuliona hili, lakini tunaomba kwamba misaada hii waisimamie ili iende kwa wale ambao wanakusudiwa. Miundombinu hii isiishie tu kwenye wheelchair na vitu vingine vya kawaida, lakini ifike pia kwenye zile facilities kwa mfano wale ambao wanauoni hafifu vifaa vyao vyote viweze kupatikana kwa urahisi. Aidha, isingekuwa tu kuwaondolea kodi lakini pia Serikali ingeenda mbali zaidi hata kuweza kuwajengea uwezo wa kupata hivi vifaa bure kabisa kwa watu wale ambao wana ulemavu mahsusi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka kulizungumzia ni suala zima la maji. Tumeona kwenye bajeti iliyopita maji yameelekezwa zaidi mjini. Tunaiomba Serikali ihakikishe kwamba pesa zilizotengwa kwa ajili ya miradi ya maji vijijini safari hii zote zinaenda.
Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Makamu wa Rais wakati wanapita kuomba kura walikuwa na kauli mbiu ya kumtua mama ndoo kichwani. Ninachoamini kwamba akina mama ambao wanabeba ndoo kichwani ni wale ambao wako vijijini, mijini maji mengi yanachotwa kwa mabomba tu nje hatua chache. Ili kumtua mama wa kijijini ndoo kichwani ni lazima tuhakikishe kwamba pesa zilizotengwa katika bajeti hii zinakwenda katika maeneo mahsusi na Wizara inasimamia miradi yote ili wananchi hao waweze kufaidika na huduma za jamii katika nchi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho nimalizie kodi kwenye muamala wa simu. Hili suala nalo ni muhimu, naomba Waziri atakaposimama ku-wind up alitolee ufafanuzi maana wapo baadhi ya wanasiasa wanalipotosha huko nje kwa wananchi. Kwa hiyo, hapa inatakiwa lielezwe kwa ufasaha. Vilevile pia Wizara itumie nafasi hii kuwabana hawa wenye makampuni za simu kwa sababu wengi wanaofanya miamala ni wananchi wa kawaida na hata wale wanaofanya biashara hii ya uwakala pia ni wananchi wa kawaida ambao wanatumia mitaji yao wenyewe lakini gharama ambazo mashirika haya yanachukua ni kubwa zaidi kuliko wale mawakala wanachokipata. Unakuta wakala anapata pesa ndogo sana wakati mtaji ni wake, wafanyakazi ni wake, yeye ndiyo analipa kodi lakini makampuni haya yanachukua gawio kubwa zaidi kuliko hao mawakala ambao ndiyo wanaofanya kazi kubwa zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, ahsante sana.