Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kutoa mchango wangu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango.
Napenda tu kumtia moyo Mheshimiwa Waziri kwamba kuwa Waziri wa Mipango na Fedha kwenye nchi inayoendelea kama Tanzania ni kazi. Na mimi nakutia moyo tu kwamba kazi hii unaiweza na ninakuamini utatuvusha kabisa na pia ukizingatia mashauri na maelekezo ambayo Waheshimiwa Wabunge wanakupa kwenye michango yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuzungumzia kilimo. Uchumi wa viwanda ambao tunautamani, unategemeana sana na hali yetu ya kilimo. Kwenye taarifa ambazo tumezisoma, hali yetu ya kilimo imepungua sana. Uzalishaji wa mazao ya nafaka umepungua na uzalishaji wa mazao ya biashara umepungua. Kwenye taarifa na hotuba ya Mheshimiwa Waziri inasema mwaka huu kilimo chetu kimeanguka mpaka kwenye asilimia 2.3. Kwenye mazao ya nafaka kilimo chetu kimepungua kutoka asilimia 3.4 kuja asilimia 3.2; pia tumepunguza uzalishaji kwenye mazao ya biashara, mazao kama pamba, kahawa na katani yamepungua sana uzalishaji wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ambazo zimetajwa mojawapo ni hali ya hewa, kwa sababu kilimo chetu kinategemea hali ya hewa. Tunaposema hali ya hewa, maana yake ni mvua ambayo tunategemea kudra za Mwenyenzi Mungu. Tatizo lingine linalotajwa kwenye maelezo ya Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2016/2017 ni upungufu au kukosekana kwa masoko ya mazao yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesahau pia yako matatizo mengi yanayokikumba kilimo chetu ambayo sijaona kama yameshughulikiwa au yamekuwa addressed vizuri kwenye mpango wa mwaka huu 2016/2017. Mojawapo ni bei za mazao hasa mazao ya biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, bei za mazao ya biashara zimekuwa ndogo kwa wakulima ambao ni wakulima wadogo wadogo kiasi kwamba wamekata tamaa kulima mazao hayo. Kule kwenye Jimbo langu tunalima pamba na tulikuwa tunalima pamba kwa wingi kweli; lakini pamba imeendelea kushuka uzalishaji wake, mwaka jana imeshuka, mwaka juzi ilishuka na mwaka huu itakuwa ni mbaya zaidi kwa sababu najua wakulima wa pamba hawakulima pamba nyingi kwa sababu bei waliyokuwa wanatarajia ni kidogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashangaa hata sasa Serikali haijatoa bei elekezi itakuwa ni shilingi ngapi kwa zao la pamba. Kwa hiyo, mwakani pia tutegemee zao hili litapungua sana kiuzalishaji kwa sababu wakulima wanalima kwa kutegemea bei waliyopata mwaka 2015. Sasa mwaka huu kutakuwa na pamba kidogo sana. Kwa hiyo, uzalishaji katika kilimo utaendelea kuwa chini. Sasa nilikuwa naiomba Serikali wajaribu kuangalia, najua ya kwamba kuna tozo zilizokuwepo, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo alituambia zitaondolewa, sasa hatujui zikiondolewa zitakuwa zimepandisha bei za mazao haya kwa wakulima kwa kiasi gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri ikaeleweka mapema, tozo zilizoondolewa ili wakulima hawa watiwe moyo kulima haya mazao; vinginevyo mazao ya kilimo, hasa ya biashara ambayo tunayategemea kwa muda mrefu yataendelea kupungua. Kwa hali hiyo, malighafi ambazo tunazitegemea kwa viwanda hazitakuwepo, mazao ambayo tunategemea kuyauza nje na yenyewe yatapungua.
Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ni sababu nyingine, lakini sababu ya pili tumepuuza kilimo cha umwagiliaji. Nchi hii ina hekta nyingi, mamilioni ya umwagiliaji ambayo yanaweza yakatumia kilimo cha kumwagilia, yakatuzalishia mazao ya nafaka na mazao ya biashara, lakini hatujaweka nguvu ya kutosha hapo, ndiyo maana hata bajeti ya Kilimo, hata tulipendekeza iongezwe lakini sijaona kama imeongezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo ambalo linalimwa kwa kumwagiliwa kwa sasa ni asilimia moja tu, lakini hiyo asilimia moja inatupa mazao ya nafaka kama asilimia 26 hivi. Kwa hiyo, utaona Kilimo cha Umwagiliaji kina uhakika namna gani kutupa mazao tunayotaka, kama tungeongeza nguvu kidogo tu, tukatoa bajeti ya kutosha, tukawa na sehemu nyingi za kumwagilia, tungeweza kupata mazao mengi ya biashara na ya nafaka kwa ajili ya nchi yetu. Sasa tumepunguza bajeti yake na sijui umwagiliaji utafanyika kwa kiasi gani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu nyingine ambayo imefanya kupungua kwa mazao ya kilimo au kudorora kwa kilimo chetu ni pembejeo mbalimbali tunazopeleka kwa wakulima. Tunapeleka kwa kuchelewa na wakati mwingine tunapeleka kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, safari hii tumeweka bajeti kidogo mno na ndiyo hicho ambacho tulikuwa tunapigania hata kwenye Kamati kwamba bajeti ya pembejeo iongezwe, haijaongezwa mpaka leo. Kwa hiyo, tutegemee pia mwakani kilimo chetu kitakuwa ni kidogo sana. Mazao tutakayovuna yatakuwa kidogo sana kwa sababu ya tatizo la pembejeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lingine lililokuwepo hapo ni utafiti. Serikali inapeleka fedha COSTECH, lakini kwa nini pesa hizi zisiende moja kwa moja kwenye Taasisi za Utafiti za Mazao ya Kilimo? Kwa nini zisiende moja kwa moja kule, zinapitia COSTECH? Kwa nini zisiende moja kwa moja Uyole, Ukiriguru, Seliani kule Arusha? Kwa nini zisiende moja kwa moja mpaka zipitie COSTECH?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tusipoangalia haya mambo, yataendelea kufanya kilimo chetu kipungue uzalishaji wake mwaka hata mwaka. Kilimo kikipungua tusahau sasa uchumi wa viwanda kwa sababu malighafi nyingi inatoka kwenye kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba wakati Mheshimiwa Waziri anajaribu kujumuisha, atuambie ni mikakati gani sasa ipo angalau kupandisha hadhi ya kilimo kinachoendelea kudorora mwaka hadi mwaka? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kuzungumzia ni kodi kwenye vifaa vya ujenzi. Kwenye bajeti hii kuna kodi kwenye nondo na vifaa vingine vya chuma vimewekewa kodi na sababu inayosemwa ni kwamba tunataka tulinde viwanda vyetu vya ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, sina uhakika Serikali imefanya utafiti kiasi gani kuona kwamba viwanda vyetu vya ndani vinaweza vikazalisha nondo za kutosha, vinaweza vikazalisha vifaa vingine vya ujenzi vya kutosheleza mahitaji. Kuna mwamko mkubwa sasa hivi wa wananchi wetu kujijengea nyumba bora na suala la nyumba bora liliwekwa pia hata kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Chama cha Mapinduzi walisema tutahamasisha wananchi wetu kujenga nyumba bora lakini pia kwa kuwezesha vifaa kupatikana kwa bei nafuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunapoweka kodi na ushuru kwenye vifaa vya ujenzi, tutegemee watu wetu kuendelea kuishi kwenye nyumba za majani, tutegemee watu wetu kuendelea kuishi kwenye nyumba za tembe, tutegemee mazingira ambayo tunapiga kelele kila wakati kwamba lazima yawe mazuri na yenyewe yaendelee kuharibika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja.