Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii kuchangia bajeti hii ya Serikali. Katika mchango wangu kwanza naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, nitaongea maneno mawili matatu kuhusiana na kilimo, ushirika pamoja na tozo za zao la korosho katika maeneo yale ambayo yanalima korosho.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza kuzungumzia suala la ushirika ninaamini Sheria Na. 6 ya mwaka 2013 ilianzisha Tume ya Maendeleo ya Ushirika, lakini katika bajeti yetu ya kilimo ipo chini ya asilimia tano, sidhani kama Tume hii ya Maendeleo ya Ushirika imepewa kipaumbele kwa ajili ya kuendeleza wakulima wetu, kwa sababu wakulima walio wengi vijijini wanategemea sana ushirika ili kupata masoko ya mazao yao pamoja na pembejeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kutegemea huko, jambo kubwa lililopo kwenye Tume ya Ushirika, ninaomba Serikali tangu sheria hii imeanza huu ni mwaka wa tatu Tume ile haina Mwenyekiti wa Tume imekuwa ni jina peke yake, Makamishna hawapo. Naomba sana katika bajeti hii iangalie namna ya kuiwezesha Tume hii iweze kufanya kazi kwa kuteua Mwenyekiti wa Tume ya Ushirika na kupata Makamishna wake ili waweze kusimamia ushirika usimame vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna matatizo mengi sana ya ushirika, lakini yanatokana na uongozi kukosa viongozi walio imara katika Idara ya Maendeleo ya Ushirika. Pamoja na hilo watumishi waliopo kwenye ushirika ni wachache, ninaomba sana kwa sababu tunapitisha bajeti hii basi waliangalie namna ya kuongeza watumishi kwenye Idara hii ya Tume ya Ushirika ili waweze kusimamia Vyama vyetu vya Ushirika viweze kufanya kazi vizuri. Kwa mfano, vyama vya Mkoa wa Mtwara, Lindi, Pwani Ruvuma ambavyo vinajihusisha na shughuli za biashara ya korosho vinatumia zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya biashara ya korosho, usimamizi haupo makini kwa kuwa Maafisa Ushirika wamekuwa ni wachache.
Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwa Serikali ni kuhakikisha kwamba wanaongeza watumishi walio na elimu ya ushirika pamoja na uwezo wa kufanya na kusimamia ukaguzi wa vyama vya ushirika mara kwa mara, kwa sababu vyama hivi vina-transact fedha nyingi sana kinyume na Sheria ya Fedha inavyotaka. Vyama vyetu vya Msingi viongozi walio wengi ni darasa la saba, mtu wa darasa la saba anafanya transaction ya shilingi bilioni mbili, bilioni tatu! Kwa kuwa Maafisa Ushirika ndiyo wasimamizi tunaomba Maafisa Ushirika wenye taaluma ya kusimamia na kukagua vyama hivi vya msingi waajiriwe waweze kuendelea kusimamia vyama hivi ili tupunguze malalamiko ya watu na wakulima wengi huko vijijini hasa kwenye Mikoa ya inayozalisha korosho na Mikoa inayozalisha tumbaku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, moja kwa moja naomba niende kwenye tozo ya zao la korosho kama ilivyopendekezwa katika bajeti hii. Nakubaliana kwenye mchakato wa kutoa tozo katika unyaufu. Nimekuwa kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani zaidi ya miaka nane, mfumo ulivyoanza kulikuwa na tozo 17, taratibu namna utendaji wa mfumo wa stakabadhi ghalani ulivyoendelea zimepunguza zile tozo mpaka zikafikia saba kwa umuhimu wake ili kuweze kumsaidia mkulima aweze kupata hela yake. Kwa mapendekezo yaliyojitokeza naomba nieleze yale ambayo ninayaona mbele ya safari yataleta mkanganyiko katika kutekeleza mfumo wa stakabadhi ghalani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni suala la ushuru wa kusafirisha korosho wa shilingi 50. Mfumo wa stakabadhi ghalani unataka ghala lolote lenye uwezo wa kuhifadhi kwa wakati mmoja tani 200 uweze kupewa kibali cha kuhifadhi korosho. Maghala yetu yaliyopo vijijini mengi yapo chini ya uwezo huo. Mbaya zaidi ubora wa yale maghala hauruhusu kuifadhi korosho kwa muda mrefu; mbaya zaidi maghala yale hayana umeme, ni vumbi tu, hakuna chochote ambacho kinaweze kustahili kuweka korosho kwa muda mrefu ili mfumo wa stakabadhi ghalani uweze kufanya kazi vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hivyo tunalalamika wataalam wa ugani hawapo katika maeneo mengi, kwa kuhakiki ubora kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani tunahitaji Maafisa Ugani katika kila Chama cha Msingi. Katika sekta ya korosho kuna vyama 739 ambavyo vinajihusisha na biashara ya korosho, kwa hiyo, tunahitaji Maafisa Ugani 739 ili kuhakikisha kila chama kinakuwa na Mhakiki Ubora ambao utasadia kuhakikisha zao linakwenda v izuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mbaya zaidi tunahitaji kipimo kinachotumika kupima ubora wa korosho kwa content ya moisture na nut counting pamoja na ubora wenyewe wa korosho kama ilivyo kile kipimo kinauzwa shilingi milioni sita kwa bei ya mwaka 2014/2015 tulinunua shilingi milioni sita, tunahitaji vipimo 739 kwa kila chama cha msingi ili viweze kuhakiki huu ubora. Kwa matatizo haya naamini kwamba mfumo wa stakabadhi ghalani ukihamia kwenye maghala ya chama cha msingi moja kwa moja tayari tutawakaribisha Wahindi waende moja kwa moja kwenye maghala ya vyama vya msingi wawe wanatembea na moisture meter yao na watakuwa tayari kuwadanyanya wakulima wetu matokeo yake bei ya korosho itakuwa imeshuka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana kuondoa tozo hii maana yake tunaondoa wakulima kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani. Sambamba na hilo usimamizi wote unaofanyika kwenye vyama vya msingi unafanywa na Chama Kikuu kwa sababu Chama Kikuu ndicho chenye wahasibu…
Mheshimiwa Naibu Spika, ooh! Ahsante, naomba kuunga mkono hoja.