Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Sixtus Raphael Mapunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye hotuba ya Bajeti ya Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna nchi yoyote duniani iliyowahi kuendelea bila kuwa na mambo manne yafuatayo:-
La kwanza, ni uwezo wake kukusanya kodi; la pili, nidhamu ya kutumia kile ilichokusanya; la tatu, kujenga mazingira ya kodi endelevu yaani kodi isiyo ya muda mfupi, kutengeneza mazingira wananchi waendelee kulipa kodi kwa wakati wote; na la nne ni kutengeneza mazingira mapya ya kupata kodi mpya.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hii ya Awamu ya Tano imeonesha nia ya dhati, imeonesha dhamira ya dhati kwenye haya niliyoyasema kwa kiwango kikubwa sana. Tumeona mikakati ya kubana mianya ya wakwepa kodi, lakini tumeona mikakakti inayopelekea kukusanya kodi kwa wakati wote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, tumeiona Serikali hii katika mipango yake imeelekeza asilimia 40 kwenye shughuli za kimaendeleo, hii ndiyo inakuwa tafsiri sahihi ya kuelekeza kile ulichokikusanya kwenye eneo sahihi, yaani shughuli za maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, maamuzi haya ya Serikali ya Awamu ya Tano kwenye hii bajeti si madogo, ni kwa mara ya kwanza imewekeza pesa nyingi kwenye shughuli za kimaendeleo. Sisi Waheshimiwa Wabunge katika ujumla wetu ni wajibu wetu kuishauri Serikali na kwa wingi wetu tuna uhakika tukipeleka sauti yetu kwa Serikali watatusikiliza. Ndugu zangu Walatini wana methali yao, huwa wanasema quot capita, tot sententiae wakimaanisha kwenye wengi hapaharibiki neno. Huu wingi wetu wa Waheshimiwa Wabunge ndani ya Bunge lako Tukufu tukiipitia hii bajeti katika ujumla wake, tuna mawazo mazuri ambayo tunaamini Serikali wakiyabeba yatatufikisha kule tunakotaka kwenda kwa haraka zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeainisha mambo mengi, kwa asilimia kubwa ni mazuri sana, lakini kuna mengine machache inabidi tuyaboreshe kidogo na tuiombe Serikali iwe flexible kwenye kutusikiliza. Wasione ugumu kuyapokea yale tunayowaeleza, nia yetu ni njema kama wao walivyokuwa na nia njema, kama wenzetu wanavyosema quot capita, tot sententiae, palipo na wengi hapaharibiki neno. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya mambo ambayo Mheshimiwa Waziri amekuja nayo mazuri, nimependa wameondoa tozo na ushuru kwenye Sekta ya Kilimo. Wameondoa kwenye korosho, pamba na kahawa, lakini nimwombe Mheshimiwa Waziri, kwenye zao la kahawa, ameondoa kodi moja, leseni ya kusindika kahawa ya Dola 250, lakini siku zote tumekuwa tukisema na Mheshimiwa Rais amezunguka kwenye kampeni yake nchi nzima ameeleza wakulima wa kahawa wanasulubika sana, wana kodi na tozo 26.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ameiondoa moja tu Mheshimiwa Waziri, nimwombe, tulisema kuna ushuru wa halmashauri wa asilimia tano, tuliomba Serikali shusheni angalau uwe wa asilimia tatu ili wakulima wetu wapate ahueni. Kuna leseni ya kununua kahawa ya Sh. 300,000, kuna tozo ndogondogo, kama sisi kule kwetu Mbinga kuna tozo ya Sh. 20 kwa kila kilo kwa ajili ya wale wadudu vidung’ata, kuna leseni ya Bodi ya Kahawa ya Dola 1,024. Kuna tozo ya TACRI ya asilimia 0.75 kwa kila kilo ya kahawa, kuna mchango wa Tanzania Coffee Development Fund (TCDF) wa 0.10, kuna ushuru wa ulinzi zaidi ya 200,000/=.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hayo yote tunamwomba sana Mheshimiwa Waziri ile Dola 250 waliyotoa ya usindikaji ni ndogo sana kwa wakulima wa kahawa, aziangalie zile kodi zote katika ujumla wake, akifanya hivi itampendeza Mungu na akifanya hivi maendeleo tutayapata.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, tunatoa misamaha ya kodi, lengo la Serikali kutoa misamaha ya kodi si kupunguza mapato yake, ni kutengeneza mazingira yule mtu ambaye anasamehewa aende akawekeze au akafanye jambo lingine ambalo litaleta kodi nyingi kwa watu wengi kwa wakati mmoja, ndiyo maana Serikali imekuwa na utaratibu wa kutoa misamaha ya hizi kodi ili kutengeneza mazingira mazuri ya kukusanya hizo kwa mlango mwingine, hiyo ndiyo maana na dhamira ya dhati ya kuweka hiyo misamaha ambayo Serikali imeiweka.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mpango wa kwenda, tena kwa kiasi kikubwa kwenye maendeleo ya kiwango cha hali ya juu ya viwanda. Viwanda haviwezi kufika kama Serikali haitakusanya mapato, viwanda havitaweza kufika kama Watanzania hawatakuwa na uwezo wa kujiletea kipato na kuweza kujikwamua katika maisha yao ya kila siku. Kwa sababu viwanda vinahitaji kwanza mashine kwa upande mmoja, lakini kwa upande mwingine viwanda vinahitaji raw material, hawa wakulima lazima wawe na uwezo wa kuzalisha sana pamba, wawe na uwezo wa kuzalisha kahawa, wawe na uwezo wa kuzalisha katani, wawe na uwezo wa kuzalisha tumbaku ili viwanda vyetu viendelee kujiendesha kwa muda wote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa haya mambo yote ndiyo inakuja ile hoja ya tatu kwa Serikali makini ambayo inataka maendeleo; lazima itengeneze mazingira kwa wananchi wake waweze kulipa kodi kwa wakati wote. Hawawezi kulipa kodi kama wana mazingira magumu ya kuzalisha. Ndipo namwomba Mheshimiwa Waziri na timu yake, najua Serikali ya CCM ni sikivu, Serikali ya Awamu ya Tano ina maono, inatufikisha mbali, wakakae na timu yake akirudi aje atuelezee. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo Mheshimiwa Waziri alilisema juzi kwenye hotuba yake, sasa anaingiza VAT kwenye utalii. Hili jambo ni jambo zuri sana, lakini nilipoisoma hotuba yake inasema reference kwanza tuliweka sheria mwaka jana, tulikuwa na mikataba tukasema mwaka huu tuimalize halafu tuendelee, lakini amei-refer Kenya wenzetu wameiondoa, ami-refer Rwanda, amei-refer South Africa; juzi wenzetu wa Kenya wameiondoa VAT.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri, aende akaangalie kitu gani kilitufanya sisi tusiiweke, kitu gani kimewafanya Kenya juzi waiweke, ili aitazame katika mapana yake, siyo kwa sababu tu South Africa wanafanya, kwa sababu tu Rwanda na Kenya wananfanya, sidhani kama ilikuwa ni dhamira.
Mheshimiwa Naibu Spika, nahisi Mheshimiwa Waziri ana hoja za kutosha za kutushawishi sisi tuamini au tuelewe kwamba kuweka ile kodi ya VAT kwenye utalii itatuongezea mapato sio kutukimbizia. Tukumbuke kwa sasa utalii unatuletea Dola karibu bilioni 2.5 kwa mwaka jana, 2015. Nadhani hii ilitokana na sisi tulikuwa na mazingira mazuri ya kuwezesha watalii wakafanya kazi. Leo hii wenzetu Kenya, wanasema ile the last token tuliyokuwa nayo inayomzidi Kenya kwenye ushindani, mwenzetu ndiyo kaibana ile, ameondoa sisi tumeweka, naomba Mheshimiwa Waziri alitazame hili kwa mapana zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho, Mheshimiwa Waziri alisema sasa tutakwenda kutengeneza sheria ambayo itaondoa misamaha kwa taasisi za kidini. Hii naomba niseme kidogo na nimuunge mkono ndugu yangu, Mheshimiwa Richard Ndassa aliyeongea juzi. Hili jambo Mheshimiwa Waziri tulitizame kwa mapana kidogo. Unajua haya madhehebu ya kidini huduma wanayotoa ni huduma, hawafanyi biashara. Wamewekeza kwenye hospitali, wamewekeza kwenye elimu, wamewekeza kwenye maji safi na salama, wamewekeza kwenye shule, ndiyo kazi wanayoifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kumwambia mtu leo, anataka alete mashine ya CT Scan kwenye hospitali ile ya mission au ile ya taasisi ya kidini, alipe kwanza ushuru wote halafu baadaye tufanye assessment arudishiwe, nina uhakika hawatanunua hizo mashine, kwa sababu kwao kazi yao ya kwanza si huduma za kijamii, wao kazi yao ya kwanza ni kumtumikia Mungu na kuleta injili na kupeleka aya ili wanadamu wamfikie Mungu, ile wanatusaidia Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mkizingatia haya maeneo yote ninayoyasema, nendeni mkaangalie zahanati zilikojengwa, hospitali zilikojengwa; mnaikuta Mvumi kule, utaikuta Hospitali ya Mvumi, nenda Lugarao utaikuta kule, nenda Ikonda, nenda utakuta Hospitali ya Peramiho, Hospitali ya Ndanda, Hospitali ya Lituhi, Hospitali ya Litembo, Hospitali ya Ifakara; hizi zote zinatoa huduma na nawaambia kabisa ukifika kule unajikongoja una shida, wanaweza wakakuhudumia hata bila kukutoza halafu uje uwalipe baadaye, hiki kitu hakipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali, kwenye suala la afya tuwape msamaha, kwenye suala la elimu tuwape msamaha na kwenye suala la maji safi na salama. Kwa mfano kwangu mimi kule Mbinga, toka dunia imeumbwa maji ya kwanza ya kunywa yalikuwa ya Buruda Otmar, (Brother Otmar) leo hii akitaka kubadilisha mabomba eti alipe kwanza ushuru sisi tupate maji safi na salama. Mheshimiwa Waziri, namwomba sana kwa dhati ya moyo wangu, alitazame hili jambo vizuri sana, sisi tulioko humu ndani nia yetu ni njema sana, hatutaki watu wakwepe kodi na tutashirikiana nao wasikwepe kodi, quot capita, tot sententiae. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.