Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Elias John Kwandikwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ushetu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye hoja hii ya Wizara ya Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nianze kwa kuunga mkono hoja. Pia nimshukuru Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa namna ambavyo ameanza kwa kuonesha juhudi ya kuweza kuhakikisha kwamba rasilimali hii muhimu inakuwa katika hali ambayo inalineemesha Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana wananchi wa Jimbo langu la Ushetu kwa sababu tumekuwa na matatizo makubwa sana, lakini wamekuwa wavumilivu lakini pia wamekuwa sehemu ya kutoa ushirikiano ili kuweza kutatua matatizo ya migogoro ambayo ipo kwenye mipaka. Sisi katika Jimbo letu la Ushetu tumepakana na Hifadhi ya Kigosi Moyowosi lakini pia tuna hifadhi za misitu nyingi kwenye Kata za Ulowa, Ubagwe, Ulewe, Nyankende, Idahina na Igomanoni. Kote huko tunapakana na misitu lakini wananchi hawa wamekuwa na utayari wa kushirikiana ili tuhakikishe kwamba uhifadhi unaendelea lakini pia mifugo yetu inapata sehemu ya malisho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakubaliana kwamba sekta hii ya maliasili na utalii imetoa mchango mkubwa sana kwenye Taifa letu. Utashuhudia kwamba kuna ajira imepatikana maeneo mbalimbali ya moja kwa moja na ile ambayo ni indirect. Pia imechangia kama wachangiaji wengine walivyosema katika pato la Taifa, fedha za kigeni tumezipata lakini mchango mkubwa umekwenda katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Jambo lingine pia uhifadhi wetu umeipa heshima nchi yetu, niipongeze sana Wizara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini utaona katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumza pia kwamba uko mchango mkubwa kwenye nishati. Asilimia 90 ya nishati imetokana na rasilimali zetu hasa hasa za kwenye misitu. Pia kumekuwa na 75% kwa mujibu wa taarifa ya Mheshimiwa Waziri imetupa faida ya kupata vifaa vya ujenzi. Kwa hiyo, utaona kabisa sekta hii ni muhimu lakini ni lazima kuhakikisha kwamba kunakuwa na uhifadhi lakini pia kutokuwa na migogoro ambayo inatusumbua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alivyoanza kutoa hotuba yake aliturejesha kwenye Ibara ya 27 ya Katiba lakini napenda nimshauri Mheshimiwa Waziri ajaribu kuiangalia Ibara ya 24 kwa madhumuni ya kuziangalia sheria zetu. Hizi sheria zetu ambazo zinatoa fursa ya uhifadhi wa misitu yetu zinahitajika ziletwe katika Bunge lako kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho. Kwa sababu ukiiangalia Ibara ya 24, naomba kwa ruksa yako niisome kwa haraka, inazungumza juu ya haki ya kumiliki mali, inasema kwamba:-
“(1) Kila mtu anayo haki ya kumiliki mali, na haki ya hifadhi ya mali yake aliyonayo kwa mujibu wa sheria.
(2) Bila kuathiri masharti ya Ibara ndogo ya (1), ni marufuku kwa mtu yeyote kunyang’anywa mali yake kwa madhumuni ya kuitaifisha au madhumuni mengineyo bila idhini ya sheria ambayo inaweka masharti ya kutoa fidia inayostahili”. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo yetu tumekuwa na utaifishaji wa mifugo, sasa nashauri sheria hizi zije hapa tuzitazame. Sheria hizi zimepitwa na muda kwa sababu ukiangalia hata zile sheria ambazo zinatoa uhifadhi katika maeneo kama ya TANAPA ziko faini ndogo sana. Nilikuwa nafikiria kwamba tufanye marekebisho lakini pia itupe nafasi sisi wananchi, kama Mheshimiwa Waziri alivyozungumza katika hii Ibara ya pili, anapozungumza juu ya uhifadhi, nani ahifadhi na hizi rasilimali ni za nani, ni zetu sisi sote. Kwa hiyo, lazima tushiriki pia kuhifadhi na kulinda hizi rasilimali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri afanye mapitio ili tu tupate sheria ambazo na sisi wananchi kwa kupitia vikundi vyetu kama wakati mwingine nilivyoshauri hapa tuweze kutoa nafasi kwa wananchi kupitia vikundi vyetu na uongozi wa mila kuweza kupeana faini kidogo kidogo za kila siku ili kuhakikisha kwamba uhifadhi unakwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kuangalia katika migogoro hii ambayo imekuwepo, chanzo chake ni nini? Ni ukweli Mheshimiwa Waziri akubaliane na mimi kwamba siku za nyuma tumekuwa na utaratibu kwamba wale wahifadhi walikuwa kwanza hawatoshi lakini pia wamekuwa wakitumika katika kuhifadhi watu ambao walikuwa wanawachukua kwa muda ambao sasa kutokana na kutokuwa na nidhamu tulichochea sana wananchi wetu kuingiza mifugo katika hifadhi. Matokeo yake ilizoeleka kama ni jambo la kawaida kwa mwananchi kupeleka mifugo yake katika hizi hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo kadhaa napenda kushauri. La kwanza Mheshimiwa Waziri lazima tuwe na dhamira ya kweli kwa upande wa Serikali na kwa upande wa wananchi na Waheshimiwa Wabunge ya kutatua hii migogoro, lazima tudhamirie kuliondoa hili suala. Tukidhamiria tutapata nafasi ya kurejesha yale mahusiano ambayo yalianza kupotea ili tushirikiane kwa pamoja kuona kwamba uelewa wa uhifashi unapanuka lakini pia tunashiriki kuweza kuhifadhi maeneo haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko pengo la uelewa ambalo nimwombe Mheshimiwa Waziri na timu yake wajipange vizuri ili tuendelee kuwaelimisha wananchi kwa kuweka vile vikundi ambavyo vimetajwa na sheria kwa ajili ya kushiriki katika uhifadhi, kwa pamoja tatizo hili tutaweza kuliondoa. Pia bajeti ya Mheshimiwa Waziri haitoshi ili kuhakikisha mafunzo yanatolewa na vikundi vinasaidiwa ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la wafanyakazi hawa kwa ajili ya doria hawatoshi. Mheshimiwa Waziri litazame suala hili ili tupate watu wenye weledi ili tuweze kwenda vizuri. Pia liko jambo ambalo nafikiria kwamba lazima tuwe na sheria ndondogo kwa upande wetu wa uhifadhi ili tuweze kusaidia kama walivyofanya wenzetu upande wa TANAPA na maeneo ya kwetu iwe hivyo ili tuweze kupiga hatua vyema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najaribu kuangalia taarifa hizi za bajeti katika kipindi hiki cha miaka miwili, mitatu, utaona uharibifu kwa mwaka ni hekta 372,000 lakini kwa mwaka tunapanda miti 95,000 na tunasema ikifikia 2030 tutakuwa angalau tumeweza kuwa na misitu ya kutosha, haiwezekani kwa sababu uharibifu huu ni mkubwa kuliko namna ambavyo tunaweza kufanya hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kuangalia gharama za kupanda miti, miche ya miti ina bei kubwa sana Mheshimiwa Waziri aangalie eneo hili kwani wananchi wetu wakipata miche ya miti watasaidia kupanda miti mingi ili tuweze kurejesha huu uharibifu. Kwa hiyo, ukiangalia uwiano wa uharibifu na namna ambavyo tunarejeshea misitu utaona kabisa haiwezekani kuhakikisha kwamba kweli hii maliasili inabaki vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo mengi tumeyazungumza kwenye mifugo, lakini tumesahau kuna eneo lingine ambalo pia linaharibu misitu yetu. Utaona kabisa kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwamba mkaa tani milioni 1.7 inaingia mjini, asilimia 50 inaingia Dar es Salaam, inatoka maeneo ya pembezoni kuja mjini. Eneo hii ni muhimu sana tuliangalie vinginevyo tutaona kwamba labda mifugo ndiyo inaharibu misitu hii, lakini bado nishati ni sehemu kubwa ya uharibu wa misitu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri aje na mkakati mzuri wa kuhakikisha kwamba tunaweza kushikiriana na upande mwingine wa nishati mbadala ili kuhakikisha kwamba hii retention ya misitu inakwenda vizuri. Suala la uhifadhi shirikishi ni muhimu sana, lazima tushirikiane na wananchi ili kuhakikisha kwamba misitu yetu inakaa vizuri. Twende sambamba na Wizara zingine kuhakikisha wananchi wetu tunawajengea kipato cha kutosha ili ule ushawishi wa kuharibu na kutumia rasilimali zetu uweze kupungua ili misitu yetu iweze kwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumze juu ya utafiti na sensa ya wanyamapori. Nimejaribu kuangalia ripoti mbalimbali naona kwamba kulikuwa kuna sample tu ya sensa kwa kuangalia namna ambavyo wanyama wamepungua, kama tembo wamepungua sana...
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.