Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JUMAA H. AWESO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha leo kuchangia hotuba iliyoko mbele yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nitumie nafasi hii kumpongeza Waziri Profesa Maghembe kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika Wizara hii, kwa kweli anaitendea haki. Waswahili wanasema mzigo mzito mpe Mnyamwezi, naamini Wizara hii Mnyamwezi ni Mheshimiwa Profesa Maghembe na kazi anaifanya. Pamoja na changamoto kubwa anazokabiliana nazo, namwambia songa mbele bahari kubwa ndiyo ivukwayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina maneno mengi sana ila kubwa nataka nijikite katika suala zima la mambo kale. Tanzania ni miongoni mwa nchi zenye hazina kubwa ya mali kale. Baadhi ya mali kale zilizopo ni pamoja na majengo ya zamani ambayo yalijengwa na matumbawe katika Miji ya Pwani ikiwemo Pangani, Bagamoyo, Kilwa na Kilindi lakini Serikali haijawekeza katika utalii wa mali kale hizi. Serikali inapoteza mapato mengi kwa kutowekeza kwenye utalii huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe katika bajeti hii itenge fedha za kutosha kuhakikisha kwamba inakarabati majengo yale ili yawe katika hadhi na kuongeza utalii katika mali kale na kuongeza pato la Taifa. Hii iende sambamba na kuajiri watumishi wanaohusiana na mambo ya kale ili kuhakikisha kwamba tunaongeza pato la Taifa katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii ya maliasili na utalii ni muhimu na mhimili wa maendeleo katika Taifa letu, lakini mchango wake siyo mkubwa pamoja na fursa zilizopo. Nchi yetu imejaaliwa kuwa na vivutio mbalimbali kama vya wanyamapori na hifadhi mbalimbali, lakini mchango wake umekuwa ni mdogo sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali itenge fedha na kuhakikisha kwamba inakuwa na mpango mkakati wa kuvitangaza vivutio hivi ili viende kuchangia pato la Taifa. Biashara ya utalii inategemea matangazo. Tunapovitangaza vivutio hivi kwa kasi kubwa, ndiyo tunapoongeza watalii kuja kuvitembelea na kuchangia pato la Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya yangu ya Pangani nataka nizungumzie mbuga ya Saadani. Mbuga ya Saadani ni miongoni mwa mbuga pekee Afrika ambayo imepakana na bahari. Mbuga hii inapata changamoto kubwa ya miundombinu mibovu ya barabara. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, ni muda muafaka sasa akae na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kuhakikisha kwamba wanaiangalia barabara hii ya Tanga - Pangani - Saadani na kuhakikisha inajengwa kwa kiwango cha lami ili kuweza kuwavutia watalii kutoka Kanda ya Kaskazini, Zanzibar pamoja na nchi jirani ya Kenya kuja katika Wilaya ya Pangani na kuinua sekta hii ya utalii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mengi sana ya kusema ila kikubwa tu nimwombe Mheshimiwa Waziri aendelee kufanya kazi na kuweza kuwatumikia Watanzania na sisi kama viongozi vijana tunaendelea kumuunga mkono kuhakikisha kwamba anafikia azma iliyowekwa katika Jamhuri yetu ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.