Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Naomba niseme kwamba wapinzani wamewasilisha malalamiko ya mtu mmoja bila ya kuleta bajeti mbadala ya upinzani. Hawa ni sawa sawa tu na Mbunge mmoja amesimama pale amechangia, lakini kusema hiyo ni hotuba ya upinzani kama bajeti mbadala hiyo ni bajeti hewa. Niliamini kama kweli ingekuwa ni Serikali kivuli basi ingewasilisha bajeti mbadala, mfano kama ameona shilingi trilioni 29.5 ni nyingi sana wao wanapendekeza trilioni ngapi? Tungesikia kutoka kwao, naamini Watanzania wamewaelewa hawa ndugu nadhani tuwaache kama walivyo na hawapo hapa Bungeni kwa sababu wamedharau. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kimkakati bajeti yetu ni nzuri sana, na vyanzo vya mapato vya bajeti hivi vinakusanyika vizuri. Kwa mfano kuondoa kodi ya majengo (property tax) kutoka kwenye Serikali za Mitaa ambazo kwa pamoja zilikuwa na uwezo wa kukusanya kati ya asilimia tano hadi 10 tu ya fedha ya kodi yote ambayo inaweza kukusanywa ni jambo la kupongeza sana. TRA kama watajitahidi, kama ninavyowafahamu mimi, wanao uwezo mkubwa wa kukusanya kati ya asilimia 50 hadi 70 ya potential. Ina maana wanaweza wakakusanya hadi trilioni 1.8 ambayo ukilinganisha na pato la zamani la shilingi bilioni 300 ina maana tutakuwa tumepiga maendeleo makubwa sana kwa hiyo naipongeza sana Serikali kwa uamuzi huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mfano wa pili, makusanyo ambayo yalikuwa ya retention yalikuwa yanatumika vibaya sana kwa hiyo kwa sasa hivi itakuwa ni fursa ya mapato hayo kutumika vizuri.
Suala lingine zuri tumepunguza mikopo ya nje kwa trilioni 0.03 kulinganisha na mwaka jana kwa ajili ya kupunguza utegemezi, kwa hiyo, hilo ni jambo lingine la kupongeza sana Serikali. Angalizo pekee hapo ni kwamba tumeongeza mikopo ya ndani kwa trilioni 1.34 hatua hii ni nzuri, lakini Wizara ya Fedha itahitaji udhibiti na ufuatiliaji wa karibu sana, kwa sababu riba za mikopo ya ndani zipo juu sana Wizara ya Fedha na Benki Kuu wakizembea kidogo tu tutatumbukia kwenye mizozo isiyo na tija inayoweza kusababisha sintofahamu kupitia matokeo hasi kama mfumuko wa bei. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maoni ya upinzani dhidi ya bajeti ya Serikali yana ukakasi wa hasira ya kugomea Bunge bila sababu za msingi. Kwa nini tuandikie mate na wino upo? Wanazo Halmashauri kadhaa ambazo wanaziongoza hivi huko kwenye Halmashauri zao wamesamehe ushuru wote na tozo zote? Badala yake wameongeza ushuru na kodi kwa hiyo ina maana kwamba hapa wanakuja kufanya mchezo wa maigizo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana Watanzania waelewe kwamba sisi Wabunge wa CCM tuko hapa kuwawakilisha na tuko makini katika kazi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kuweka vipaumbele vya kujenga uchumi wa viwanda kwenye bajeti hii mpya. Katika vipaumbele hivyo nashauri Serikali ikamilishe maandalizi muhimu yanayotakiwa kwenye sekta wezeshi ili kuhakikisha kwamba bajeti hiyo itatekelezeka vizuri sana. Kwa mfano kule kwetu kuna barabara ya kutoka Chunya hadi Itigi na barabara ya Ipole hadi Rungwa, barabara hizo mbili ni barabara muhimu sana kwa kwetu kwa uchumi wa viwanda, tunaomba sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa maji wa Ziwa Victoria ni mradi mmoja wezeshi ambao ni muhimu sana. Miradi ya umeme vijijini, zahanati, vituo vya afya, shule ni miradi wezeshi ambayo tunaomba sana fedha ambazo zimepangwa kwa mwaka ujao ziweze kutolewa zote zitumike zote kwa ufanisi. Na vilevile pale ambapo kutakuwa na upungufu mwaka 2017/2018 tusisahaulike kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kusimamia utekelezaji wa mpango na bajeti napenda kujua ni shilingi ngapi zimewekwa kwa ajili ya monitoring and evaluation? Kwa sababu haiku wazi kwenye Bajeti hii. Bila monitoring and evaluation tutapata matatizo makubwa. Kwa mfano Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali amepangiwa shilingi bilioni 34, kwa mtazamo wangu fedha hizo ni ndogo sana. Tunamtarajia Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Ofisi yake iimarishwe zaidi ili afanye kazi vizuri zaidi. Tunahitaji awe na uwezo mkubwa wa kufanya ukaguzi wa kitaalamu au technical audit ambapo haiitaji wahasibu na wakaguzi wa ndani peke yake. Inahitaji wahandisi, wakadiriaji wa majengo, wachumi na wataalamu wengine wengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunahitaji ofisi hii iweze kuimarishwa kwa nguvu kazi na uwezo wa kufanya kazi. Sasa hii pesa iliyowekwa hapa ni ndogo sana, kwa hiyo tunaomba sana ifikiriwe mara mbili ili kusudi bajeti hiyo iongezwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kusisitiza ni bajeti ya utafiti. Kwenye sekta karibu zote ni bajeti ndogo sana imepangwa. Utafiti duniani kote ni jukumu la Serikali, kwa hiyo inatakiwa bajeti ya utafiti hasa kwenye mazao ya biashara na chakula iongezwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo napenda kuchangia ni kwamba, Serikali imekiri hapa kwamba kuna ugumu wa kukusanyaji wa mapato kwenye sekta isiyo rasmi. Sasa Serikali imejua tatizo inatakiwa ikamilishe sasa sehemu muhimu ya namna gani ya kutatua tatizo hili, kwa sababu tunahitaji kukusanya mapato kutoka kwenye sekta isiyo rasmi. Nashauri Serikali iweke kipaumbele cha kuisajili sekta yote isiyo rasmi ili kuijua vizuri na kurahisisha Serikali kukusanya mapato yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nafurahi kusikia kuwa deni letu la Taifa bado ni himilivu, na ili kudhibiti deni letu Wizara ya Fedha inatakiwa kuwa macho sana na madalali wa mikopo ya miradi mikubwa ambao hujiita transaction agents, ambao hujifanya wanasaidia nchi kupata mikopo mikubwa kutoka kwenye Serikali rafiki za nchi nyingine. Kama watu hao wasipodhibitiwa hatimaye tutakuwa na mikopo yenye gharama kubwa sana maana nao huwa wanatoza tozo.
Mheshimiwa Naibu Spika, miradi yetu mikubwa kama ya reli, bwawa la Kidunda, bomba la mafuta, itaathirika kwa kuiingiza nchi kwenye gharama kubwa zaidi kama hatutawadhibiti hao transaction agents. Naomba sana Serikali iwe makini.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nina wasiwasi na bajeti ndogo sana kwenye sekta ya ardhi kukidhi kazi muhimu za kupima viwanja nchi nzima, lakini hasa hasa lile swala ambalo Mheshimiwa Waziri Mkuu alikubali hapa, kwamba inatakiwa iteuliwe Kamati ya Kitaifa ambayo itaunganisha Wizara zaidi ya nne kwa ajili ya kufanya kazi ya kubaini maeneo yote ambayo yanahitaji kuongezwa ili kusudi wakulima na wafugaji wapate maeneo mengi zaidi ya kufanya shughuli zao. Hii bajeti iliyoko kwenye sekta ya ardhi ambayo ndiyo ingegharamia kazi hiyo hakuna.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Serikali ifikirie mara mbili, kazi hiyo ni ya muhimu sana kwa maendeleo ya taifa. Na kwa ajili ya kuliweka taifa letu katika amani na utulivu ni muhimu sana mapori ya akiba ambayo yamekosa sifa mpaka sasa hivi yako mengi sana hapa nchini hii timu inatakiwa iende ikafanye ukaguzi na kuleta mapendekezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningependa kulitolea maoni yangu, ni kukata kodi gratuity ya Wabunge. Sidhani kama kulikuwa na ulazima wa kuleta suala hilo mwaka huu, lakini vilevile si dhani kama kuna ulazima wa kukata hiyo gratuity. Najua, inaletwa ili kusudi makato yaanze kufanyika kuanzia mwezi wa saba unaokuja.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Ofisi ya Mbunge ni Taasisi inayojitegemea, na ina majukumu mengi sana kwenye jamii, na wananchi wanaitegemea, na fedha hizi nyingi huwa hazitumiwi na Mbunge binafsi, fedha nyingi huwa zinakwenda kwenye jamii, Mbunge huwa anachangia miradi mbalimbali. Kwa hiyo, mimi naomba sana...
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kakunda muda wako umekwisha.
Naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.