Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana. Na mimi naomba nitoe mchango wangu mdogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niamze kwa masikitiko katika Wizara hii. Kama ambavyo wenzangu wameongea kama pato la Wizara hii ni shilingi bilioni moja, na sisi Watanzania tunapigwa bakora, wananchi wanaenda kwenye msitu wanapigwa bakora, ifike mahali tuone basi kile kinachopatikana kina tija kiasi gani. Ninaomba sheria ya Wizara hii iwekwe mbele ya Bunge hili tuipitie upya yote tuangalie upya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria nyingi za Wizara hii zimekuwa kandamizi na hii inaipelekea jamii yetu kupata matatizo mara nyingi hasa wale wanaokaa na kukutana na mazingira yale ya hifadhi. Kwa hiyo, naomba sheria itazamwe upya mbele ya Bunge hili ili tuione jinsi ambavyo inaenda na wakati wa sasa na pia ni sheria yenye manufaa kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ninaomba basi pia tutazame, muone jinsi ambavyo fidia inayotolewa ni ya ajabu sana. Mwaka jana kabla ya mwezi Oktoba tembo walitoka Msitu wa Marang wakaenda mpaka kwenye Wilaya yangu ndani ya Jimbo langu wakaua watu watatu hadi mazishi hakuna mtu wa TANAPA aliyekuja. Kama anaweza kutoka tembo mpaka kilometa 40 au 30 akamuua mtu na bado sisi tunakaa huku tunazungumza mjadala wa bajeti ya Wizara hii tunakwenda wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu inaelekea pabaya, inaonesha tembo ndio wana thamani kuliko binadamu. Na mimi nikuombe wewe na Serikali kwa ujumla jinsi ambavyo tunapata madhara makubwa ya tembo hawa wanaotoka msitu wa Marang katika Jimbo langu na wanakula mazao ya watu mashambani huku wanaua wananchi, hakuna hatua inayochukuliwa tulipowaita TANAPA hawakuja mpaka siku ya tatu, hatimaye tembo wanaua watu watatu kwa siku tofauti. Tuangalie sana upana wa jambo hili, kama ambavyo wananchi wanapata madhara na pia fidia hakuna hatushiriki kwenye mazishi, tunapata matatizo makubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla kabisa tutazame jinsi ambavyo sheria ipo nyuma ya wakati, sheria ipo nyuma ya maisha ya wanadamu wetu na haiwatendei haki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu wa kawaida akiingia msituni katika misitu ya Marang huko Jimboni kwangu, Waziri afahamu hili, mtu wa kawaida akipita kwenye msitu au akakutwa kwenye msitu hana kitu chochote anapigwa na askari; sisi bado tunaanza kupiga meza tunafurahia Wizara hii. Kama ni hiyo shilingi bilioni moja iondolewe kwenye bajeti upatikanaji wa huduma upungue kupitia fedha hizo ambazo mnatarajia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasikitika sana kama askari alieenda shule aliyepata taaluma anaanza kumpiga badala ya kumpeleka mbele ya sheria tunakwenda wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamsikitikia sana Mheshimiwa Waziri kwa jinsi ambavyo watu wake wamekuwa wa ajabu. Tuliendesha operation tokomeza ikazalisha mambo ya ajabu sana na Watanzania wengi wakafa bado Bunge halijaanza kutazama jambo hili leo bado askari wanapiga wananchi wetu. Ninamuomba Waziri, nilimuomba mara nyingi afanye ziara kwenye Jimbo langu awasikilize wananchi, aje na karatasi nyeupe wananchi waandike mambo waliyofanyiwa na kama Rais anatumbua atumbue kuanzia kwa Waziri mpaka kwa watendaji wengine wote. Nimekasirika sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana, wananchi wangu wamedhurika na pia kama ambavyo tukio linatokea Waziri ni mzito kufika, watendaji ni wazito kufika, hatimaye wananchi wanawekwa njia panda. Mimi siko tayari kuungana na hii Wizara, nipo kinyume kabisa. Nimtake Waziri apange ziara na apange ratiba ya vikao vya ujirani mwema kote Tanzania kwenye mazingira ambayo kuna hifadhi hizi ili kila mara kwa kila robo tuone wananchi wamefanyiwa nini. Hifadhi hizi zilikuwepo kabla TANAPA hawajaja, jamii walilinda, walihifadhi ndiyo maana hifadhi ziko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasikitika sana; mimi ni wa CCM habari ya CCM hapa hakuna, hapa tuzungumze uchafu. Bila ziara, askari wanatoka kwenye msitu wanaenda kukamata wananchi, wanawapiga wananchi bado mnasema eti tunafanya vizuri, hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; vikao vya ujirani mwema vimeachwa kwa sababu matendo yao hayafanani na hali halisi ya Watanzania na haki za binadamu. Nimekasirishwa sana, kijiji cha Tawi nilikotoka mimi tembo wameuwa watu wawili kilometa 50; kama hatuwezi kuwarudisha tembo msituni tuna sababu gani sasa ya kupiga makofi eti kushabikia hii Wizara? Halafu mtu wa Mbulu anafuata fidia Dar es Salaam; aliwe shamba fidia Dar es salaam, fidia yenyewe shilingi laki moja. Anakwenda tena anakufa mtu fidia sijui shilingi laki tano Dar es Salaam; hivi kutoka Mbulu kwenda Dar es Salaam na kuishi kwenye gesti na hoteli na nini ni shilingi ngapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni shilingi ngapi zinapotea? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushiriki wa TANAPA kwenye misiba inayotokana na wanyama iwekwe kwenye sheria, migogoro itatuliwe haraka; migogoro inaaachwa mpaka wananchi na TANAPA wanaingia uadui, tunapata uadui. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchimbaji wa madini msitu wa Marang. TANAPA wanachimba madini kwenye msitu, mwananchi akiingia anakamatwa na anauawa. Kama Usalama wa Taifa wapo, wale watu watatu waliokufa kule Magara fanyeni uchunguzi walikufa kwa ajili ya nini. Wananchi wanasema walikufa kwa sababu walikwenda kuiba madini, Kaizer akienda kuiba madini ndipo anauawa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri afanye ziara, aende msitu wa Marang, Jimbo la Mbulu, aende Yaeda Chini. Yaeda Chini usiku hutatoka, majangiri ni bunduki zinatembea utafikiri hii ni nchi ya vita. Habari ya u-CCM mnayoleiteta hapa ni ya kazi gani kama mambo ni ya hovyo hovyo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaitaka Serikali hii ijiangalie upya!, Serikali hii ijiangalie upya. Kama watu wanauawa kwa ajili ya kwenda kuchimba madini na TANAPA wanachimba; ninakutaka Waziri, nenda kwenye msitu wa Marang ukachukue hatua ya wale wanaochimba msitu wa Marang na wa Manyara, watoke wale TANAPA na wao wasichimbe, hawana sababu ya kuchimba pale. Mali zinazokamatwa zinakuwa miradi ya watu. Mali inakamatwa, mbao inakamatwa inauzwa, ni miradi ya watu, mnasema tunapata shilingi bilioni moja ya kazi gani? Shilingi bilioni moja itatufikisha wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba sana, na ninaitaka Serikali; kazi ya Bunge ni kuibana Serikali, na wewe Waziri tunaanza na wewe. Tuanze na wewe na wewe uwabane walio chini yako. Mtu yeyote wa CCM achukue hatua juu yangu kama anaweza. Kama ni namna hii... (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nani alikuja kwenye kampeni wakati tunafanya kampeni? Kila mmoja alitetea kiti chake ndiyo maana tuko huku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kura zangu zilipungua kule Daudi, Gehandu, Marang kwa ajili ya mtindo huu huu wa kuleana.
MWENYEKITI: Ahsante, ahsante