Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma alienijalia afya njema kusimama ndani ya hili Bunge lako hili Tukufu. Lakini pia nimtakie pole bibi yangu Nyankulu kutoka kule Mtanange, leo hii anapambana na vita ya kansa, namuombea apone haraka ili aendelee kuniombea.
Tatu niseme tu kwamba niwashukuru wananchi wa Jimbo langu la Rufiji kwa namna ya kipekee kabisa kuniomba leo hii nibaki ndani ya Bunge kwa sababu siku ya leo ni siku ambayo Mwenge umefika katika Jimbo langu la Rufiji. Kwa kutambua kwamba Jimbo la Rufiji linabeba asilimia 50 ya Hifadhi ya Taifa letu, wakaniambia nibaki kwa ajili ya kuzungumza mambo ya msingi kabisa kwa ajili ya ustawi wa taifa letu hili la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba hii ni nchi yetu sote, nianze kwa kusisitiza kwamba nchi hii ni yetu sote. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kumteua Brigedia Jenerali Gaudencia Milanzi. Tunatambua uteuzi wake una changamoto nyingi kwamba anapaswa kufanya kazi, kupambana na majangili ili ni kufuta aibu kubwa iliyotokea mwezi Januari ya kuuwawa kwa rubani wa ndege Bwana Roger Gower. Hakika jina la pilot huyu litakumbukwa katika nchi yetu na litaandikwa katika historia kwani alikuwa ni miongoni mwa wapambanaji wanaosaidia kupambana na ujangili katika nchi yetu hii ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefuatilia kwa undani sana taarifa za kwenye mitandao lakini pia nimefuatilia kwa umakini uwasilishwaji wa hoja mbalimbali ndani ya Bunge lako hili Tukufu. Pia nina fahamu zipo taarifa za wadau mbalimbali kutumiwa ili kujaribu kukwamisha bajeti ya Wizara hii; wadau mbalimbali wakiwemo na wanasiasa pia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, michango mbalimbali iliyowasilishwa katika Bunge lako hili Tukufu imejikita kwa watu wengi kuzungumzia haki za wafugaji lakini wamesahau kwamba wakulima tunao na wana haki zao za msingi na wanachangia asilimia 25 ya Pato la Taifa la nchi yetu hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwalimu Nyerere aliwahi kutukumbusha kuhusiana suala hili la kubagua au kubaguana, kuanza kuwabagua watu fulani kuwaona watu fulani wao ni muhimu kuliko watu wengine. Lakini naomba nisisitize Ibara ya 13(4) ambayo inafafanua kuhusu haki ya kutobagua watu au kundi fulani. Wakulima wamebaguliwa sana ndani ya hili Bunge lako Tukufu. Ninaomba niseme wakati wa uwasilishwaji wa Wizara ya Kilimo tuliona wafugaji wengi walifika hapa Dodoma, lakini pia wakati wa uwasilishwaji wa Wizara hii wafugaji wengi pia wapo ndani ya Dodoma hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilikumbushe Bunge lako Tukufu Ibara ya 13(5) ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inayofafanua mambo kadhaa na emphasis is mine na nisisitize hili:- “Katika kutimiza haja ya haki au mahitaji mengineyo kwa watu mbalimbali kwa kuzingatia utaifa wao, kabila, pahali wanapotoka, maono yao ya kisiasa, rangi, dini, jinsia au hali yao ya maisha kwa namna ambayo watendewe wao ili waweze kupewa fursa au faida katika nchi hii.” Ibara hii inasisitiza haki ya kutobagua watu fulani. Naomba msisitizo huu Waheshimiwa Wabunge wauchukue ili tunapokuwepo hapa tujadili haki za msingi za wananchi wetu wote wa Tanzania bila kubagua huyu ni mfugaji au huyu ni mkulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vurugu hizi kati ya wakulima na wafugaji nizungumze kidogo, hazikuanza zamani sana sisi kule Rufiji tulizoea kuamka unakutana na mpunga; lakini leo hii mifugo imeingia, lakini silaumu kilichotumika ni Ibara ya 14 ya Katiba yetu ambayo inaruhusu Mtanzania kuishi popote. Ibara hii ya 14 ilitumia baada ya Waziri Mkuu Fredrick Sumaye pamoja Lowassa kuendeleza mchakato huu wa kuhakikisha kwamba mifugo inasambaa ndani ya nchi yetu. Si tatizo baya kwa sababu huu ni utekelezaji wa Ibara hii ya 14. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hapa nikumbushie Ibara hii ya 14 ambayo inakwenda sambamba na ukumbushwaji wa sheria mbalimbali. Ninaamini Wabunge wengi wanasahau kwamba tunazo sheria nyingi ambazo zinatuongoza katika nchi yetu hii, na iwapo tutawashauri wananchi wetu kufuata sheria hizi hakutakuwepo na mgogoro wowote kati ya wakulima na wafugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikumbushie Sheria ya Matumizi ya Ardhi Namba 6 ya mwaka 2007 ambayo inatoa mchakato mzima wa namna gani ardhi itatumika na wapi wakulima waweze kufanya kilimo chao na wafugaji waweze kufuga wapi mifugo yao. Pia tunayo Sheria ya Mpango wa Vijiji sheria ya mwaka 1999 lakini pia tunao Mpango wa Taifa wa Matumizi ya Ardhi. Mpango huu ni wa mwaka 2013 mpaka 2033. Tunayo sheria ya kuhifadhi maliasili pamoja na miongozo mbalimbali ya viongozi isiyokinzana na Katiba. Tunayo Ibara ya 26 ya katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inatusisitiza wananchi wetu kufuata sheria. Tatizo hapa ni wananchi kutotaka kufuata sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikumbushe tu kwamba sheria hizi zilitungwa na Bunge hili, kama tunaona sheria hizi ni mbovu ni jukumu la Bunge letu hili Tukufu kubadilisha sheria hizi.
Katika kubadilisha sheria hizi Ibara ya 26 inazungumza wazi sina sababu ya kuisistiza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nirudi kwenye hoja zangu za msingi, hoja ambazo wa Rufiji wamenituma nije niwawakilishe hapa. Nianze kuzungumzia kodi ya kitanda. Niende haraka haraka, kodi hii ya kitanda ambayo ilitoka shilingi 8,000 kwenda shilingi 120,000 kodi hii iliundwa ili kuwakandamiza Warufiji. Mimi nikuombe kodi hii ambayo hata kama Mrufiji umelalia kitanda miaka 30 unawajibika kukilipia kodi iwapo unatoka nacho Rufiji unakwenda Wilaya zinazofuata Kibiti na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe kodi hii Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba sana Mheshimiwa Waziri aweze kuiondoa kodi hii ambayo ni kodi kandamizi.
Kwa wananchi wangu wa Jimbo la Rufiji. Nitaomba taarifa kuhusiana na kuondolewa kwa kodi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 30(3) ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inanipa mamlaka mimi kupitia iwapo sheria au miongozo ya Serikali inakinzana na Katiba, mimi kama Mbunge na mwanasheria nguli nitakuwa na uwezo wa kufungua kesi ya Kikatiba ilikuweza kuomba Mahakama kutoa tafsiri fasaha ya kuondoa kodi hii ya kitanda ambayo ni kandamizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe taarifa mbele ya Bunge lako hili Tukufu, baada tu ya kumaliza Bunge hili iwapo Waziri hataifuta kodi hii nitafungua kesi ya Kikatiba kwa sababu kodi hii ni kandamizi na ikinzana na Katiba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaona hiyo nisiizungumzie kiundani zaidi lakini nirudi kwenye kodi ya mkaa. Kodi hii ya mkaa imekuwa ikiongezeka siku hadi siku. Niliwahi kufanya tafiti kuhusiana na kodi ya excise duty, kodi hizi ambazo zinakuwa zinatolewa na Serikali ili ku-discourage consumption. Kuongezeka kwa kodi ya mkaa kunasababisha ongezeko kubwa la maisha kwa wananchi wetu wa Jimbo la Rufiji ambao wanategemea biashara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende mbele, nikimbie haraka haraka kidogo, naomba nizungumzie kuhusiana na pesa ya upandaji wa miti. Wananchi wangu wamekuwa wakichangia wanapokuwa wanalipa kodi ya mkaa wanachangia kiasi cha shilingi 830 kwa gunia kwa ajili ya kupanda miti. Naomba nipate taarifa kutoka kwa Waziri miti ambayo imeshawahi kupandwa na watu wa TFS ili kuweza kujiridhisha kwamba miti hiikweli inapandwa na pesa hii inatumika inavyotakiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende haraka haraka kutokana na muda nizungumzie suala la migogoro…
MWENYEKITI: Ahsante.