Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia. Nami niungane na wengine kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia katika Bunge hili, niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Ubungo kwa kuniamini na kunichagua kuwa Mbunge wao, kwa kura zaidi ya 87,000 dhidi ya yule ambaye upande wa pili wanamwita hajawahi kushindwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja katika hoja yangu katika kuchangia Mpango wa Maendeleo, katika ukurasa wa 50(6)(a) ambayo ni Vihatarishi katika Mpango. Vihatarishi katika utekelezaji wa Mpango, vimeelezwa kwamba ni pamoja na kumekuwa na changamoto katika upatikanaji wa mikopo kwa wakati, na riba kubwa hivyo kuathiri uwezo wa nchi kukopa, kwa upande wa misaada kumekuwepo na masharti magumu na utayari wa washirika wa maendeleo kutoa fedha kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeelezwa hapa kwamba vihatarishi vya Mpango ni pamoja na Washirika wa Maendeleo kukataa kutoa fedha kwa wakati. Washirika wa Maendeleo nchi ya Marekani, Taifa kubwa duniani, tayari limekataa kutoa fedha za MCC, na Umoja wa Ulaya uko njiani kuzuia misaada. Sababu wanasema kwamba kuna tatizo Zanzibar, uchaguzi wa Zanzibar umefanyika na kuna tatizo kubwa la msingi ambalo linapaswa kutatuliwa, sisi tuko hapa Bungeni tunajifungia ndani ya Bunge hili, tunajifanya hamnazo, tunaona kwamba Zanzibar hakuna tatizo tunashangilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanasimama katika Bunge, wanajipa mamlaka wa kuwa Maamiri Jeshi Wakuu, na wanatangaza kwamba Zanzibar hakuna tatizo. lakini ukweli ni kwamba, uchaguzi wa Zanzibar utatuletea matatizo makubwa kama Taifa, tusipokuwa makini katika kutatua tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hakuna namna yoyote ya Bunge hili kukwepa kuzungumza suala la Zanzibar. Uchaguzi wa Zanzibar ulifanyika tarehe 25 Oktoba na matokeo yote yakawa yameshakusanywa na yapo.
MHE. HAFIDH ALI TAHIR: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwongozo...
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naomba ulinde muda wangu. Iwapo matatizo haya Zanzibar hayatatatuliwa kwa umakini vinginevyo mpango huu mzima hautatekelezwa.
MHE. HAFIDH ALI TAHIR: Taarifa...
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naomba ulinde muda wangu, lakini nimepokea maelezo ya Mheshimiwa Hafidh Ali Tahir, nimemshangaa kwamba anataka tusizungumzie masuala ya Zanzibar, wakati yeye ametoka Zanzibar amekuja hapa kuiwakilisha Zanzibar. Yuko kwenye Bunge hili kwa sababu ya Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia Mpango wa Maendeleo na ninapozungumzia maendeleo, tunazungumzia maendeleo katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Zanzibar ikiwemo, Katiba hii imeitaja Zanzibar kuwa ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; asome vizuri. Matatizo ya Zanzibar ya uchaguzi yasipopatiwa ufumbuzi wa kudumu tukakaa humu ndani tukajifanya hatujui kama Zanzibar kuna tatizo, Maaskofu wanahubiri katika Madhabahu, Mashehe wanasema katika Misikiti, wadau wa maendeleo wanatukanya, kwamba Zanzibar kuna matatizo sisi tunakaa hapa tunajidanganya. Nchi yetu tunaipeleka pabaya na Mpango huu wa Maendeleo hautafanikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tokea mwaka 1964 mpaka mwaka 1980 hakuna Mpango wowote wa Maendeleo uliofanikiwa kwa zaidi ya asilimia hamisini kwa sababu wadau wa maendeleo walikataa kutoa fedha. Fedha za maendeleo kutoka kwa nchi wahisani zilikuwa hazitoshi na huu mpango mzima unaokuja hapa unategemea fedha za wahisani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa thelethini na moja wa kitabu hiki, kimeelezwa juu ya suala zima la utawala bora. Bunge hili ambalo Mpango unasema kuimarisha utawala bora, lilifanya kazi kubwa sana katika Bunge la Kumi, kulipitishwa maazimio hapa juu ya fedha za escrow, Tume zikaundwa, Majaji ambao walituhumiwa kuhusika na kashfa ya Escrow wakaundiwa Tume za uchunguzi, ilitangazwa. Mawaziri wanne wakajiuzuru katika Bunge hili, Wenyeviti wawili wa Kamati za Bunge wakajiuzuru. Serikali ikasema inaunda Tume lakini Tume ya majaji haikuundwa, Mawaziri waliojiuzuru mmoja Profesa Sospeter Muhongo amerudishwa katika Bunge hili akiwa Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aliyeondolewa na Bunge leo anaongoza Bunge kama Mwenyekiti wa Bunge. Hii maana yake nini, maana yake suala zima la rushwa lililotajwa katika ukurasa wa 34 kwamba ni tatizo katika nchi yetu linaonekana halina tatizo kabisa.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa! Nampa taarifa Mheshimiwa Saed Kubenea...
MWENYEKITI: Mheshimiwa Kubenea endelea.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nilikuwa naeleza na bado nasisitiza kwamba suala la utawala bora ni jambo la muhimu sana katika Taifa letu. Hatuwezi kukaa hapa tukawa tunahubiri amani na utulivu wakati Taifa letu halina utawala bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana mmoja wa wachangiaji katika Bunge hili alisema kwa sauti kubwa kwamba Chama ambacho kimegombea uongozi kwa vipindi vitatu mfululizo kikishindwa kitaingia kuwa chama cha ugaidi. Hata hivyo, namsamehe kwa sababu hasomi historia anaishia hapa hapa Tanzania. Ukienda India, Uingereza, Canada na Newzealand vyama vyote vikubwa vilivyoshindwa uchaguzi vimebaki kuwa imara, Chama kinachoshindwa uchaguzi lakini kinaendelea kuimarika kwa kushinda Majimbo mengi na kuchukua Halmashauri nyingi na kile ambacho kinashinda uchaguzi, lakini kinaendelea kuporomoka siku hadi siku kipi kinachoelekea kwenye ugaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila shaka Chama kile ambacho kinashinda uchaguzi lakini kinaendelea kuporomoka siku hadi siku ndicho kinachoelekea katika ugaidi. Hayo yanaonesha ni jinsi gani Taifa letu leo usalama wa raia wetu ulivyokuwa mashakani. Mimi mwenyewe ni muhanga wa usalama wangu na nimetajwa katika Bunge hili la Kumi katika ripoti ya richmond.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanauwawa, watu wamepigwa na Serikali iliyopo madarakani imeshindwa kulinda raia na mali zao. Waandishi wa Habari kina Mwangosi, Mwandishi wa Habari mwenzangu ameuwawa, Absalom Kibanda amepigwa, Dkt. Steven Ulimboka ametekwa na kutupwa katika Msitu wa Mabwepande, lakini Serikali imekaa kimya na inasema hawa watu wasiojulikana. Serikali ni lazima ichukue hatua madhubuti kulinda usalama wa raia na mali zao ili kuimarisha utawala bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wenzangu wanazungumza sana mambo ya reli ya kati na mimi naomba nizungumze kuhusu reli ya Kati.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mpango mzima wa reli ulioletwa hapa na Serikali, wakati sisi tunaonya kwamba nchi wahisani zimekataa kutoa fedha na kwamba mipango hii ya maendeleo haiwezi kutekelezwa. Kuna Mpango umekuja hapa wa reli. Reli hii inahitaji dola bilioni saba, karibu shilingi trilioni kumi na tano. Serikali ya Tanzania ilikuwa inaomba fedha kutoka Serikali ya China. Naomba niwapeleke shule, Serikali ya China imekataa kutoa fedha kwa ajli ya kujenga reli ya kati, mtafute fedha kutoka maeneo mengine.MWENYEKITI:
Mheshimiwa Kubenea muda wako umekwisha.