Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Daniel Nicodemus Nsanzugwako

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii. Hata hivyo, nashauri niseme machache.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana Wilaya ya Kasulu kuanzisha Baraza la Ardhi tangu mwezi Aprili, 2016. Nashauri basi wataalam hao wafike haraka Kasulu ili Baraza lianze kazi mara moja. Ni hatua nzuri yenye manufaa kwa Wilaya za Kasulu na Buhigwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upo uhaba mkubwa sana wa Maafisa Ardhi na Maafisa Mpango Miji. Ni vizuri Serikali iliangalie jambo hili ili wahitimu wa vyuo vyetu vya ardhi waajiriwe moja kwa moja bila kusubiri nafasi hizo eti zitangazwe, ni jambo muhimu sana. Kama walimu wanaajiriwa moja kwa moja, kwa nini isiwe hivyo kwa wapimaji wa ardhi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara sasa iongeze hoja hii Serikalini ili mwaka huu shida hii kwenye Halmashauri, Wilaya, Manispaa na Miji imalizike. Kasulu Town Council ina uhaba mkubwa wa upimaji ardhi, valuers na Afisa Mipango miji yupo mmoja. Hatuna muda wa kusubiri, wakati ni sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu zoezi hili hati za ardhi za kimila limefanyika nchi nzima, Wilaya ya Kasulu na hasa vijiji vinavyounda Halmashauri ya Mji bado hati hazijatolewa, licha ya baadhi ya vijiji kupimwa. Ni muhimu sasa zoezi la kutoa hati za kimila lihamie Wilaya ya Kasulu na hasa vijiji vya Nyumbigwa, Mhunga, Malumba Herujuu, Karanga, Mpanza na Masambara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Mji wa Kasulu (Kasulu Town Council) tumetenga ardhi, viwanja kwa ajili ya wawekezaji wa nyumba na hasa nyumba za gharama nafuu za NHC. Tafadhali kupitia kwa Mheshimiwa Waziri, aagize NHC waje sasa Kasulu, soko ni zuri kwa sababu sasa Kasulu ina Halmashauri mbili; Kasulu DC na Kasulu TC, nyumba zinahitajika sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mahitaji ya nyumba za walimu na waganga ni kubwa, mfano Wilaya ya Kasulu, Halmashauri ya Mji na Halmashauri ya Wilaya, mahitaji ya nyumba ni zaidi ya nyumba 2000. Kwa nini NHC wasiagizwe kufanya kazi hiyo badala ya Halmashauri ya Wilaya kujenga nyumba chache chache kwa kipindi kirefu? Hii inaweza kufanywa kwa uamuzi wa Serikali na hasa Wizara yako ili NHC wasijikite mijini tu na waelekezwe kupeleka nguvu maeneo ya vijijini wakajenge nyumba za gharama nafuu.