Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DKT. HARRISON G. MWAKYEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kwanza kwa kuwasilisha hotuba ya Bajeti ya Wizara yao kwa ufasaha mkubwa na pili kwa kusimamia utekelezaji wa shughuli za Wizara kwa ujasiri mkubwa. Hivyo bila kigugumizi chochote, naunga mkono hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii vilevile kuipongeza Wizara hii kwa kuitikia kilio changu cha muda mrefu cha kuanzisha Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya ya Kyela. Kilio changu kiliitikiwa mwezi Julai, 2014 kwa kuanzisha Baraza hilo lakini kwa kutumia Mwenyekiti na Maafisa wengine wa Baraza ambao huazimwa kutoka Mbeya zaidi ya kilometa 100 kutoka Kyela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu huo sasa umegeuka kero kubwa kwa wananchi kukosa huduma ya uhakika ya Baraza kutokana na Mwenyekiti na Maafisa wake kushindwa kufika Kyela pale inapobidi na kuwaacha wananchi wengi wakisubiri, wakienda na kurudi bila mafanikio.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Waziri na Naibu wake wanipatie uongozi/uendeshaji wa Baraza wa kudumu badala ya kusubiri maafisa wa kuazima kutoka Mbeya ambao hawafiki Kyela kwa sababu wanazozijua wenyewe. Nina uhakika, timu hii imara ya uongozi wa Wizara itasikia ombi langu na kulifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine tena naunga mkono hoja.