Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kuisimamia Wizara hii, Wizara ambayo kwa muda imekuwa ikikabiliwa na changamoto nyingi sana kiutendaji na kimfumo. Hongera sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utakubaliana na mimi kuwa rasilimali ardhi ina umuhimu wa kipekee kwa uhai na maendeloe ya binadamu. Aidha, kwa uchumi wa Taifa letu ambalo wanancni walio wengi wanategemea sana kilimo, sekta muhimu katika kukidhi mahitaji yao ya kila siku. Ni kutokana na ukweli huu rasilimali ardhi inabeba sifa ya kuwa haki ya kila Mtanzania na kwamba kumnyima Mtanzania yeyote haki ya kumiliki na kuitumia ni uvunjaji wa haki za binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wimbi la kuwepo kwa migogoro ya mipaka na uvamizi wa ardhi katika maeneo ya vijiji limekuwa tatizo kubwa katika nchi yetu. Tatizo hili ni kikwazo kwa maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla. Migogoro hii imeendelea kusababisha upotevu wa mali, vifo na kuendeleza uhasama kati ya jamii na jamii na hivyo kuwafanya wananchi kubaki maskini na kuishi maisha duni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, uwepo wa mashamba makubwa yasiyoendelezwa ni chanzo kingine kikubwa cha migogoro ya ardhi nchini. Kwa muda mrefu, mfumo wetu wa kufuta miliki ya ardhi isiyotumika ipasavyo kwa mujibu wa makusudio ya umiliki wa ardhi husika umetumika kutoa mwanya wa watu wachache kuhodhi ardhi bila kuitumia na kuwaacha wananchi wengi kutaabika kwa kukosa ardhi. Naipongeza sana Serikali kwa jitihada kubwa zinazofanyika sasa kuhakikisha mashamba yaliyotelekezwa yanafutiwa hati za umiliki na hatimaye kugawanywa kwa wananchi. Hongera sana Mheshimiwa Waziri kwa kusimamia vyema jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mkinga ni miongoni mwa Wilaya zinazokabiliwa na migogoro ya umiliki wa ardhi na uwepo wa mashamba yaliyotelekezwa kwa muda mrefu. Kwa nyakati tofauti ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga na mimi binafsi tumewasilisha Wizara ya Ardhi, mapendekezo ya Wilaya kuhusu utatuzi wa migogoro hiyo. Wakati mapendekezo ya ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga yaliwasilishwa Wizara ya Ardhi mapema mwaka 2007, wakati huo Mkinga ikiwa bado ni sehemu ya Wilaya ya Muheza; Ofisi yangu iliwasilisha tena maombi hayo kupitia barua yenye Kumb.MB/MKN/Ardh01/2011 ya tarehe 17 Novemba, 2011.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi chote cha uhai wa Bunge la Kumi mara kwa mara nilikuwa nakumbushia jambo hili kwa michango kwenye hotuba za bajeti za Wizara, na barua. Pamoja na jitihadi hizi bado changamoto hizi hazijapatiwa ufumbuzi. Mheshimwia Waziri nilifarijika sana kupata barua yako iliyotaka Wabunge kuorodhesha migogoro ya ardhi katika Majimbo yetu. Hivyo basi, natumia fursa hii kuikumbushia Wizara juu ya maombi haya ambayo kimsingi yamechukua muda mrefu kupatiwa ufumbuzi:-
(i) Shamba la Kilulu - shamba hili ndipo sehemu ambayo Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga yamejengwa. Shamba hili kwa mara ya kwanza lilimilikishwa kwa Ndugu Van Brandis na Bibi Mary Van Brandis hadi 31/10/1959 ambapo umiliki ulihama kwenda kwa Ndugu Akberali Walli Jiwa. Mmliki huyu hakuendeleza shamba hili lenye ukubwa wa ekari 5,699.9 hadi umiliki wake ukafutwa mwaka 1972. Baada ya kufuta umiliki, Serikali ililipa fidia na shamba likawa chini ya Serikali.
Baadaye Wilaya ya Muheza ilipokea maombi ya kumilikishwa shamba hilo toka Kampuni ya M/S Arusha Farms Ltd. (CHAVDA). Taratibu zote zilifanyika na alimilikishwa ekari 2,699.9 na ekari 3000 walipewa wananchi wa vijiji jirani vya Vuo, Mwachala na Purungu Kasera waliokuwa na shida ya ardhi. M/S Arusha Farms Ltd walipewa barua ya toleo (leter of right of occupancy) ya tarehe 10/05/1991 ambayo ilisajiliwa na Msajili wa Hati tarehe 13/05/1990 kwa Land Office Number 125127.
Mmiliki huyu aliomba mkopo kutoka CRDB kwa kuweka rehani barua ya toleo. Aidha, alishindwa kurejesha mkopo huo na CRDB waliuza shamba kwa M/s Mbegu Technologies Ltd. tarehe 27/03/2004 ambao walilipa mkopo huo, lakini pia hakuweza kuliendeleza shamba hilo. Ndugu Akberali Jiwa licha ya kunyang‟anywa shamba hilo na kulipwa fidia aliwasilisha ombi lake la kurejeshewa umiliki wa shamba hilo. Ombi lake liliwasilishwa katika kikao cha Kamati ya kugawa ardhi tarehe 10/10/1996 na iliazimiwa liwasilishwe katika Kamati ya Ushauri ya Ardhi Mkoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati hiyo chini ya Uenyekiti wa Mkuu wa Mkoa iliridhia Ndugu Akberali Jiwa apewe shamba hili kwa vile M/s Arusha Farm Ltd. wameshindwa kuliendeleza. Halmashauri ya Muheza ilitoa barua ya toleo kwa miliki ya miaka 99 kuanzia tarehe 1/10/1998 kwa Akberali Jiwa kwa jina la Kampuni ya Kilulu (2000) Ltd. Baada ya tatizo hilo la double allocation kujitokeza, Halmashauri ya Muheza iliandika barua yenye Kumb Na. MUDF/3844/63 ya tarehe 2/4/2007 kwenda kwa Kamishna wa Ardhi kwa ajili ya kuomba kufuta miliki hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa taarifa ya Halmashauri hadi leo Halmashauri haijapata majibu yoyote licha ya ufuatiliaji uliofanywa wa mara kwa mara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali halisi kwa sasa ni kwamba eneo hili lina michoro ya mipango miji minne, mitatu iliandaliwa na Katibu Tawala wa Mkoa kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Muheza kabla ya kuanzishwa Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga na mchoro mwingine umeandaliwa na Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga. Aidha, eneo hili limepimwa jumla ya viwanja 400 kwa matumizi mbalimbali ikiwemo, taasisi, majengo ya Serikali, majengo ya umma, viwanja vya michezo, maeneno ya kuabudia, makazi biashara na maeneo ya wazi. Kwa mara nyingine tena naiomba Serikali ifute milki ya Kilulu Plantation kwa manufaa ya umma.
(ii) Moa Estate - shamba hili lina ukubwa wa ekari 15,739.60 na linamilikiwa na Mkomazi Plantations Ltd. ya S.L.P 2520 Dar es Salaam ambayo baadaye ilibadilisha jina kuwa Mao Plangation and Aquaculture ya S.L.P 364 Dar es Salaam, kwa hati Na. 2468, 9780 na 9781. Halmashauri ya Wilaya ilituma notisi ya kuwafutia hati miliki yao kwa kutelekeza shamba na kulipia kodi. Baada ya hapo Halmashauri ya Wilaya iliwasilisha barua ya mapendekezo kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na. MKG/LD/F/2/54 ya tarehe 28/07/2009. Taratibu za ufutaji hati miliki ziliendelea Wizarani lakini Halmashauri ilipokea barua ya mmiliki ikieleza kuwa jina la umiliki lilibadilika na kuwa Moa Plantation and Aquaculture wa S.L.P 364 Dar es Salaam na kwamba wanataka kuendeleza shamba hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ilikwishawasilisha Wizarani barua ya mapendekezo ya kufuta hatimiliki, ililazimika kumwandikia Kamishna wa Ardhi barua yenye Kumb. Na. MKG/LD/F/2/56 ya tarehe 09/06/2001 kumweleza kupokea barua hiyo na kwamba shamba hilo lina vijiji vinne ambavyo vimeanzishwa na kusajiliwa Moa, Ndumbani, Mayomboni na Mahandakini. Aidha, vijiji hivyo tayari vina huduma za jamii kama shule, zahanati, barabara na kadhalika. Katika maeneo hayo hivyo aendelee na taratibu za ufutaji hatimiliki au kama atasitisha ufutaji basi wamiliki wakubali kumega maeneo yanayokaliwa na vijiji na kuendelezwa na wananchi. Kamishna wa Ardhi kwa barua Na. LD/70503/76 ya tarehe 23/11/2011 alisitisha ufutaji huo kwa masharti kwamba walipe kodi ya ardhi kuanzia mwaka 1996 hadi 2011/12 na kumega maeneo ambayo yenye vijiji tajwa. Hata hivyo, hawakutimiza masharti hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia hali hiyo, Halmashauri iliandika barua kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na. HW/MKG/LD/F/2/62 ya tarehe 27/07/2012 ili aendelee na taratibu za ufutaji. Kamishna wa Ardhi kupitia barua yenye Kumb. Na. LD/70503/76 ya tarehe 23/11/2011 alisitisha ufutaji huo kwa masharti kwamba walipe kodi ya ardhi kuanzia mwaka 1996 hadi 2011/2012 na kumega maeneo ambayo yenye vijiji tajwa. Hata hivyo hawakutimiza masharti hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia hali hiyo, Halmashauri iliandika barua kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na. HW/MKG/LD/F/2/62 ya tarehe 27/07/2012 ili aendelee na taratibu za ufutaji. Kamishna wa Ardhi kupitia barua yake Kumb. Na. LD/70503 ya tarehe 15/01/2013 iliitaka Halmashauri kuwasilisha vielelezo jambo ambalo Halmashauri ilifanya. Aidha, barua ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi yenye Kumb. Na. LD/NZ/12931/18/DW ya tarehe 15/04/2013 kwenda kwa Kaimu Kamishna wa Ardhi nayo inahusika akishauri ufutaji wa hati hizo uendelee. Kwa sasa Halmashauri ya Wilaya inasubiri uamuzi wa Kamishna wa Ardhi.
(iii) Mwele Seed Farm - shamba hili lina ukubwa wa hekta 954, mmiliki ni Wizara ya Kilimo. Wakati ambapo shamba hili lilikusudiwa kuwa shamba la kuzalisha mbegu, hali halisi ni kwamba kwa kipindi cha takribani miaka 15 sasa shamba hili limeshindwa kutumika kama ilivyokusudiwa na sehemu kubwa kubaki kuwa pori. Wananchi wa vijiji vinavyozunguka shamba hili Mbabakofi, Maramba A, Maramba B na Lugongo ndiyo wamekuwa nguvu kazi ya kulifanyia usafi shamba hili pale wanaporuhusiwa kufungua mashamba mapya na kulima mazao ya muda mfupi kila msimu mpya wa kilimo unapowadia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 21/09/2007, Halmashauri ya Wilaya iliandika barua kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na. MUD/ASF/VOL.VI/35 ikipendekeza kumegwa kwa shamba hili na kugawiwa kwa wananchi wa vijiji jirani kutokana na uendelezaji wake kuwa mdogo sana na kodi kutolipwa. Hata hivyo, maombi haya hayakuwahi kupatiwa majibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili linapakana na kijiji cha Mbambakofi chenye takribani kaya 500 zenye jumla ya wananchi wapatao 3,173. Mbambakofi ni kijiji pekee katika Wilaya ya Mkinga ambacho kimekosa hata eneo la kujenga huduma muhimu za kijamii kama shule ya msingi na zahanati. Aidha, shamba hili linapakana na Mji Mdogo wa Maramba ambao unakua kwa kasi kubwa, ukiwa na takribani watu 30,000 na kuzungukwa na mashamba ya Maramba JKT hekta 2445, Lugongo Estate hekta 6040, Kauzeni Estate hekta 189.66, Mtapwa Estate hekta 476.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya kutelekezwa kwa shamba hili imezidi kuwa mbaya sana sasa kuliko ilivyokuwa mwaka 2007, wakati Halmashauri ya Wilaya ilipoomba mara ya kwanza kumegwa kwa shamba hili. Kwa sasa hali imekuwa mbaya kiasi kwamba hata majengo mengi yaliyokuwepo yameanguka na machache yaliyosalia yamekuwa magofu, mashine na mitambo yoyote ya kilimo iliyokuwepo shambani hapo imeharibika na michache iliyosalia imehamishiwa Morogoro. Kwa sasa shamba limebaki na wafanyakazi wasiozidi watano kutoka waliokuwepo miaka ya 1990.
(iv) Shamba la Maramba JKT - ukubwa wake ni hekta 2,445 na linamilikiwa na Jeshi. Eneo kubwa halitumiki na halilipiwi kodi. Barua iliyoandikwa kuhusu Mwele Seed Farm iliunganishwa pia mapendekezo ya kumega shamba hili ili wananchi wa Mji Mdogo wa Maramba waweze kupata eneo la kujenga makazi yao.
(v) Shamba la Segoma - msitu wa Segoma wenye ekari 2,311 upo ndani ya shamba la Sigi Segoma lenye ukubwa wa ekari 2829. Shamba hili lilimilikishwa kwa Shirika la Uchumi la Wilaya ya Muheza (SHUWIMU) kwa hati Na. 7675 ya tarehe 01/04/1990 ya miaka 33. Kutokana na kukosa mtaji na kuzorota kwa SHUWIMU, hati hii ilibadilishwa umiliki kuwa Muheza District Council kuanzia tarehe 16/02/2007.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1992 SHUWIMU kwa kukosa mtaji na utaalam iliingia ubia na M/s Sigi Agricultural Co. Ltd., na SHUWIMU ilipovunjwa shamba lilimilikiwa na Muheza District Council ambayo ilifuta ubia uliokuwepo na kuingia ubia na SWIFTCOM ya Tanga. Hii ilisababisha M/s Sigi Agricultural Co. Ltd. kufungua kesi namba 18 ya 1996 kupiga kupinga kufutwa kwa ubia wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2011 hukumu ya kesi hii ilitolewa na Halmashauri ya Muheza kupewa ushindi. Mwaka 2007 Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ilianzishwa kwa kumegwa toka Muheza. Katika zoezi la kugawana mali, shamba hili liligawiwa kwa Halmashauri ya Mkinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hukumu kutolewa, Halmashauri kwa ufadhili wa Tanzania Forest Conservation Group (TFCG) ilifanya ukaguzi wa uhalisia wa wakati huo na kutoa taarifa katika kikao kilichofanyika tarehe 08/10/2012 kikihusisha viongozi wa kijiji cha Songea, Kata, wataalam wa Halmashauri, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania - Kanda ya Kaskazini na wataalamu wa Mkoa. Aidha, kikao kilitoka na mapendekezo kwa kuwa na kijiji cha Segoma kina tatizo kubwa la uhaba wa ardhi, ekari 518 za shamba zigawanywe kwa wananchi kwa shughuli za kilimo na makazi na ekari 2,311 zitengwe kuwa eneo la hifadhi ya msitu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 15/12/2012 kikao cha Baraza la Madiwani kama wamiliki halali wa rasilimali hii kiliridhia mapendekezo haya na kuagiza ekari 518 zigawiwe kwa wananchi wa kijiji cha Segoma kwa shughuli za makazi na kilimo na ekari 231 zimilikishwe kwa kijiji cha Segoma kuwa msitu wa kijiji. Ili kutekeleza agizo la Baraza la Madiwani, Menejimenti iliwasiliana na Meneja wa Kanda wa Wakala wa Huduma za Misitu kwa makabidhiano. Hata hivyo Meneja wa Kanda wa Wakala wa Huduma za Misitu aliomba kuonana na uongozi wa Halmashauri kwa majadiliano juu ya kijiji kumilikishwa misitu. Taarifa ya ombi hilo ilipofikishwa kwenye kikao cha Baraza cha tarehe 16-17/07/2014, Baraza liliagiza kuwa wataalam wa Ardhi na Misitu wa Wilaya watekeleze Azimio la Baraza la tarehe 05/12/2012.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Menejimenti kutekeleza agizo hilo, tarehe 28/11/2014 kwa mshangao mkubwa Halmashauri ilipokea barua kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ikiamuru kusitishwa kugawa ardhi kwa wananchi kwa ajili ya kilimo na makazi na hali kadhalika kukabidhi msitu kuwa wa kijiji cha Segoma. Jambo hili limeleta taharuki kubwa kwa wananchi kiasi kwamba walikuja Dodoma wakati wa vikao vya bajeti kuwasilisha malalamiko yao. Aidha, wakati wa kuhitimisha mjadala wa bajeti nililazimika kuomba ufafanuzi kuhusiana na jambo hili na Naibu Waziri alikiri kuwa wananchi wa Segoma wanayo haki ya kupatiwa ardhi tajwa na kwamba atatembelea Mkinga ili kulipatia ufumbuzi jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tukiendelea kusubiri utekelezwaji wa ahadi ya Naibu Waziri kutembelea Mkinga kuja kuupatia ufumbuzi mgogoro huu, Halmashauri ilipokea barua toka kwa Katibu Tawala wa Mkoa yenye Kumb. Na. BF 174/314/02/35 ya tarehe 02/12/2015 ikiagiza eneo la ekari 518 likabidhiwe rasmi kwa kijiji na eneo la msitu lenye ukubwa wa ekari 2311 kuwa chini ya usimamizi wa Wakala wa Huduma za Misitu hadi hapo uamuzi mwingine utakapotolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maamuzi haya ya kuinyang‟anya Halmashauri ya Mkinga rasilimali yake siyo tu kwa nia ya uonevu mkubwa bali pia yanakinzana na Sheria ya Misitu ya mwaka 2002 ambayo inabainisha wazi kuwa jamii inaweza kulinda, kuhifadhi, kusimamia na kutumia kiuendelevu misitu katika ardhi ya kijiji ili kukidhi mahitaji yao ya kimaendeleo ya muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikimbukwe kuwa zaidi ya hekta milioni mbili za misitu hapa nchini zinasimamiwa na Serikali za vijiji zaidi ya 1000. Hivyo kijiji cha Segoma kukabidhiwa kusimamia msitu wao wa asili haitakuwa mara ya kwanza. Tungependa kuona busara iliyotumika mwaka 2015 kuruhusu Kata ya Enguserosambu katika Wilaya ya Ngorogoro kusimamia msitu wa Longido II ikitumika hata kwa msitu wa Segoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kutokana na ukweli kuwa wananchi hawa ndiyo wameutunza msitu wa Segoma na kuwajibika kuhakikisha msitu unabaki salama pasipo kuombwa wala kukukabidhiwa na Serikali. Inasikitisha kuona leo wananchi hawa wakiporwa rasilimali hii kwa mabavu, kejeli na udhalilishwaji kuwa wao ni wavamizi. Halmashauri ya Mkinga na wanakijiji wa Segoma wanataka kunufaika na umiliki wa rasilimali yao kupitia mapato yatokananyo na mavuno ya msitu huu ili kuboresha huduma za kijamii na kuleta maendeleo ya kijiji.
(vi) Kwamtili Estate - shamba hili lina ukubwa wa hekta 1,150 na lina milikiwa na Kwamtili Estate Ltd. yenye certificate of Incorporation No. 2649 iliyosajiliwa tarehe 09/01/1961 ikiwa na wanahisa wafuatao:

S/N JINA LA MWENYE HISA ANAPOISHI MAELEKEZO

1 Dennis Martin Fielder 4 Market Square Tenbury,Wells Worcestershine – UK Amerudi Uingereza
2 National Agriculture &
Food Corporation (NAFCO) Box 903 DSM Shirika limefutwa
3 Handrik Tjails Scheen C1/30 Algami nes Bank, Amsterdam, Netherland Amefariki
4 Louis Van Wagenburg Layscian Ag Vaghel, Holland Amefariki
5 Schoonmarkers Bart
Venderburg De Conqabsen, 163 Schlkher, Holland Amefariki
6 Tracey Elan Allison The Willos Terrigton, Herefordenshire, UK Amefariki
7 Juvent Magoggo 42 Block S. Mikanjuni Box 5855 Tanga Anaishi Tanga
8 W.J. Tame Ltd Box 118 Tanga Amefariki
9 Jacobus Cornelius Logtanburg Vaghel, Holland Amefariki
Josephus Moris


Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili lililopo katika eneo la Kwamtili, Kata ya Bosha, Wilaya ya Mkinga lilitumika kwa kilimo cha kibiashara cha zao Kakau. Hata hivyo kwa muda wa miaka takribani 26 saa shughuli za kilimo cha zao la Kakau zimesimama baada ya aliyokuwa Menejiment ya Kampuni chini ya Ndugu Dennis Fielder kutelekeza shamba. Aidha, baada ya shamba kutelekezwa, mmoja wa wanahisa Ndugu Juvent Magoggo amekuwa akifanya shughuli ndogo ndogo ikiwemo kuvuna miti ndani ya shamba hili kwa lengo la kupata fedha za kufanyia uzalishaji mdogo mdogo; na hali kadhalika kuruhusu wananchi wanaozunguka shamba hilo kulima mazao ambayo siyo ya kudumu. Hata hivyo, kwa sasa ndugu Magoggo ameshindwa kuendelea kufanya shughuli hizo baada ya kunyimwa vibali vya kuvuna miti na kusafirisha magogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kuwepo kwa ombwe la umiliki wa shamba hili yamezuka makundi ya watu yanayodai kuwa na haki ya kumiliki shamba hili na hivyo kuwakodisha wananchi wanaozunguka shamba hili maeneo ya kulima kwa kuwalipisha sehemu ya mavuno yatokanayo na matumizi ya ardhi hiyo. Aidha, kumekuwa na wimbi la kujitokeza raia wa kigeni kwa kutumia kivuli cha aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa shamba na kulitekeleza Ndugu Dennis Fielder kufanya uharibifu wa mali za kampuni, ikiwemo upasuaji wa mbao na kuanzisha michakato ya kujimilikisha ardhi hii. Katika hili, wananchi wanainyooshea kidole ofisi ya Wakala wa Hifadhi ya Misitu - Wilaya ya Mkinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kwamtili na Kata ya Bosha kwa ujumla wamebaki katika umaskini wa kutupa baada ya shughuli za kilimo cha Kakau katika shamba la Kwamtili ambacho kilitoa ajira kwao kusitishwa. Nusura kwa wananchi hawa ni kupatiwa maeneo katika shamba hili ili kwa kutumia utaratibu wa wakulima wadogo waweze kufanya shughuli ya kilimo na hivyo kujikimu kimaisha. Naiomba Serikali ifanye uamuzi wa kufuta hati ya shamba la Kwamtili na kisha kuligawa kwa wananchi kwa ajili ya kilimo, na sehemu nyingine kutengwa kuwa hifadhi ya msitu wa kijiji.
(vii) Mjesani Sisal Estate - shamba hili lenye hati Na. 48108 na ukubwa wa ekari 22,725 lilitelekezwa kwa muda mrefu na hali iliyosababisha ardhi kumegwa na kuanzishwa vijiji vinne ndani ya shamba ambalo ni Kwangena, Mchangani, Bomba Mavengero na Mnyenzani. Aidha, Kampuni ya Mohamed Ltd. ya S.L.P 20600 Dar es Salaam imejitokeza na kuanza kuendeleza baadhi ya maeneo ya shamba hili. Hali hii imeleta changamoto kubwa hasa ikizingatiwa kuwa tayari vijiji vilivyomo ndani ya shamba hili vimepatiwa usajili na TAMISEMI. Mfano kijiji cha Kwangena chenye ukubwa wa hekta 300 kimepewa hati ya kuandikishwa kwa kijiji Na. TA/KIJ/603 ya tarehe 03/01/1997, aidha, upimaji wa vijiji ulifanyika na ramani za upimaji kupata vibali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia mkanganyiko huu wa umiliki wa ardhi katika vijiji tajwa, wananchi wa vijiji husika wamekuwa na kilio cha muda mrefu kuiomba Serikali iingilie kati ili kuondoa utata wa umilikishwaji wa maeneo ya vijiji vyao. Mfano, Mkutano Mkuu wa Kijiji cha Kwangena ulikaa na kuomba kupewa ardhi kwa mujibu wa ramani ya kijiji aliyoidhinishwa. Baraza la Madiwani iliyobariki ombi hilo na Halmashauri kupitia barua yenye Kumb. Na. HW/MKG/D.35/138/5 ya tarehe 17/072012 iliwasilisha ombi hilo kwa Kamishina wa Ardhi, mnamo mwaka 2015 Wizara ilituma wataalam wake kuja kufufua mipaka ya shamba na kwa mshangao mkubwa wananchi wa Kwangena wakamegewa ekari 216 tu. Aidha, ndani ya kipindi kifupi sana ramani ya upimaji ikisajiliwa kwa namba 82741, na wakaandaliwa hati nyingine yenye LONO. 560486 na hati ikasajiliwa tarehe 26/11/2015. Tunaomba Serikali iangalie upya suala hili ili wananchi wa vijiji vya Kwangena, Mchangani, Bamba, Mavengero na Mnyenzani waweze kupatiwa ardhi itakayowawezesha kuishi kwa fahari katika nchi yao huku wakiweza kukidhi mahitaji yao ya kimaisha.
(viii) Mgogoro wa Kijiji cha Mkota na Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi - wananchi wa Kitongoji cha Kimuuni katika Kijiji cha Mkota Kata ya Mwakijembe wamekuwa wakiishi katika eneo hilo tangu kabla ya uhuru. Kitongoji hiki kina takribani kaya 170 na wakazi wapato 530. Wananchi hawa wa muda wote wamekuwa msaada mkubwa kwa ulinzi na rasilimali za nchi yetu hasa ikizingatiwa kuwa eneo hili linapakana na nchi jirani ya Kenya. Wananchi hawa wanalalamika kuwa eneo lao limechukuliwa na hifadhi ya Taifa ya Mkomazi na Pori Tengefu la Umba na kwamba sasa wanatakiwa kuondoka kwenye eneo hilo licha ya kufanya uwekezaji mkubwa kwa kutumia nguvu zao kuchimba mabwawa makubwa ya kunywesha mifugo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro huu nimeufikisha Serikalini na nimelizungumzia jambo hili mara nyingi sana katika Bunge la Kumi, lakini hadi sasa halijapatiwa ufumbuzi. Mheshimiwa Anna Tibaijuka wakati akiwa Waziri wa Ardhi akiongozana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, alifanya ziara katika Wilaya ya Mkinga na kufanya mkutano wa hadhara katika kijiji hiki. Katika mkutano ule, Mheshimiwa Waziri aliwaahidi wananchi kuushughulikia mgogoro huu. Aidha, aliyekuwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mheshimiwa Mahmood Mgimwa akiandamana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa naye alifanya ziara katika eneo la mgogoro (Kimuni) na kufanya mkutano wa hadhara ambapo alipokea ombi la wananchi kwa eneo hili kupewa hadhi ya kuwa Wildlife Management Area (WMA) na kuahidi Wizara kuanzisha mchakato wa kulitanga eneo hili kuwa WMA. Tunaamini kuwa suluhisho la mgogoro huu ni Serikali kukamilisha mchakato huu ili wananchi waweze kuishi kwa amani.
(ix) Manza Bay Sisal Estate - ni mkusanyiko wa mashamba manne yenye ukubwa wa jumla ya ekari 2,217.6 shamba na. 273 hati na. 7047 LONO. 124814 ekari 461, shamba Na. 196 hati Na. 14275 LONO. 12621 ekari 498.6, shamba Na. 272 hati Na. 3576 LONO. 642 ekari 507 na shamba hati Na. 14322 ekari 764. Mmiliki wa mashamba haya ni Mbegu Technologies Inc. Ltd. wa S.L.P 173 Moshi. Mashamba haya yote yameingia katika eneo la Mji wa Kasea ambao ndio Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga. Kwa muktadha huu naiomba Serikali ione umuhimu wa kufuta hati hizi ili eneo hili liweze kufanyiwa matumizi ya kuendeleza mji wa Kasera.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na migogoro hiyo hapo juu, ipo migogoro mingine iliyoibuka kutokana na zoezi la upimaji wa vijiji mwaka 2007 lililohusisha wataalam wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na wataalam wa Halmashauri ya Mkinga. Kiini cha migogoro hii ni zoezi kufanyika bila kuhakikisha ushiriki wa viongozi wa pande zote za vijiji husika katika kubainisha mipaka, jambao ambalo limepelekea vijiji ambavyo havikuwa na uwakilishi kugomea kutambua mipaka iliyowekwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti orodha ya vijiji vyenye migogoro hii ni kama ifuatavyo:-
(a) Kijiji cha Daluni Kibaoni na Kijiji cha Ng‟ombeni; (b) Kijiji cha Daluni Kibaoni, Kijiji cha Mgambo Shashui na Kijiji cha Movovo;
(c) Kijiji cha Mnyenzani na Kijiji cha Jirihini;
(d) Kijiji cha Magodi na Kijiji cha Mwanyumba;
(e) Kijiji cha Dima na Kijiji cha Mazola Kilifi;
(f) Kijiji cha Doda na Kijiji cha Magaoni;
(g) Kijiji cha Monga Vyeru na Kijiji cha Kichalikani;
(h) Kijiji cha Mwakijembe na Kijiji cha Mkota;
(i) Kijiji cha Msimbazi na Kijiji cha Dima; na
(j) Kijiji cha Bosha na Kijiji cha Churwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kuwa sasa changamoto za muda mrefu za uwepo wa migogoro ya mipaka ya vijiji umiliki wa ardhi na uwepo wa mashamba yaliyotelekezwa kwa muda mrefu katika Wilaya ya Mkinga yatapatiwa ufumbuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha hoja ya bajeti hii atueleze nini kauli ya Serikali kuhusiana na changamoto hizi, na tunamuomba atoe kipaumbele cha kuitembelea Mkinga ili kuja kutatua migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.