Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Halima Ali Mohammed

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. HALIMA ALI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ni dhahiri kwamba kipimo cha mtu yeyote kinapimwa kutokana na makazi yake anayoishi na hatopimwa kwa mlo wake kwani hii inakuwa ni siri yake mwenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu usajili wa hati na nyaraka za kisheria; kumekuwepo na malalamiko makubwa ya kukatisha tamaa kuhusiana na urasimu katika Halmashauri zetu hususani katika Mji Mkuu kama vile Dar es Salaam. Tatizo la njoo kesho, njoo kesho kutwa linakatisha tamaa kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, fikiria kwanza mtu atakwenda Halmashauri kufuatilia kiwanja chake anatumia zaidi ya saa sita linatafutwa faili halionekani, kwa siku ile anakosa kazi nyingine kutafuta riziki ya chakula. Siku nyingine akienda atapewa ahadi ya kuwa anatakiwa afike mwezi ujao, mwezi ukiisha ataambiwa kila kiwanja kimeongezeka ukubwa unatakiwa ulipe fedha ya ziada ili utengenezewe hati au sehemu ile iko katika shamba la mzungu! Mheshimiwa Waziri nina ushahidi naomba Serikali iwaangalie sana watendaji ambao wanataka kukwamisha juhudi za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upangaji wa makazi ya vijiji. Mheshimiwa Waziri hili ni jambo zuri la mradi huu wa MKURABITA lakini bado jamii/wananchi hawajaelimishwa kuhusiana na jambo hili. Hivyo MKURABITA watoe elimu ya kutosha hasa kwa akina mama ambao bado wanatawaliwa na mila na desturi potofu zinazowagandamiza wanawake. Kwa mfano, katika makabila mengine wanawake hawawezi kuongea mbele ya wanaume na wala hawawezi kujiamulia kitu chochote wala kumiliki mali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali itilie mkazo MKURABITA watoe elimu stahiki kuhusiana na malengo yao. Hatimiliki ziwe na hadhi ya kuwafanya waweze kukopa katika mabenki kama zilivyo hati nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake wafikiriwe kupunguziwa bei ya ardhi kulingana na vipato vyao, kwani wanawake ndiyo maskini wa mwisho, wanawake wana watoto na wao ndiyo walezi wa watoto hao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu udalali wa Maafisa Ardhi hili ni tatizo, ukitaka kiwanja maeneo ya mji ukifuata utaratibu wa kisheria huwezi kupata kiwanja, utaandika barua ya maombi lakini kupata kiwanja haiwezekani ila ununue barua kutoka kwa Maafisa wa Ardhi ndiyo uweze kuendelea na utaratibu. Serikali iangalie suala hili ili kuweza kuwafanya Watanzania wawe na imani na Serikali yao. Naomba kuwasilisha.