Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kuchangia Wizara hii kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, upungufu wa Maafisa Ardhi katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ni mkubwa sana kiasi kwamba inasababisha maeneo mengi kutokupimwa kwa wakati na watu kujenga holela. Hata hivyo, wafanyakazi waliokuwepo wanashiriki kwa namna moja au nyingine na kujihusisha na rushwa kwa kupima maeneo ya wazi hata maeneo ya hifadhi ya barabara kama ilivyojitokeza kwa mwekezaji mmoja anayeitwa Cross Road Petrol Station kujenga petrol station eneo la barabara. Kwa mujibu wa mchoro wa awali sehemu hiyo iliwekwa kwa ajili ya kutengeneza junction ya barabara kuu ya Masasi - Tunduru - Songea na barabara ya Bomani jambo ambalo limesababisha mgogoro mkubwa na mkandarasi anayejenga kwa lami barabara ya Tunduru - Matemanga ambapo mwekezaji huyo anadai fidia kwa vile ana hati miliki ya eneo hilo ingawa ni sehemu ya hifadhi ya barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ucheleweshaji wa michoro/ramani za viwanja vilivyopimwa ni kero kubwa sana. Tangu mwaka 2012 mchoro wa viwanja vilivyopimwa bado haujarudi kutoka Wizarani ili walionunua viwanja waanze kutafuta hati ya viwanja vyao. Kwa hiyo, ni kero kubwa sana kwa wananchi wa Tunduru. Mimi nikiwa mmojawapo nimeshindwa kupata mkopo kwa kukosa hati ya nyumba yangu kwa vile mchoro bado haujapitishwa na Wizara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, tatizo la viwanja vilivyopimwa kupewa watumishi badala ya wananchi wa kawaida. Watumishi hao baadaye huviuza viwanja hivyo kwa bei ya juu kwa wananchi wa kawaida wakati wao wamevinunua kwa bei nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, mipaka ya vijiji inavunjwa sana na watumishi wa ardhi kwa kusogeza na kutoa beacon zilizowekwa wakati vijiji hivyo vimeanzishwa na kusababisha migogoro ya kijiji na kijiji. Kwa mfano kijiji cha Namasalau na Kitando, Semli na Chikomo/Mchesi/Muungano suala hili limeleta ugomvi wa wakulima kwa wakulima kutokana na Ofisi ya Ardhi kutotoa ramani za awali za vijiji hivyo. Hivyo, ni vyema Ofisi ya Ardhi wakatoa ramani ya Wilaya ya Tunduru kwa kila kijiji ili wajue mipaka yao ya awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, mikopo ya nyumba kwa wafanyakazi. Mikopo mingi ya mabenki kwa wafanyakazi inatolewa kwa walio Dar es Salaam tu, wa mikoani ni wachache sana ambao wanafanikiwa kupata mikopo hiyo. Hivyo ni vyema Serikali ikasimamia mabenki waweze kukopesha wafanyakazi waliopo mikoani na wilayani ili waweze kujenga sehemu za kuishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, Shirika la Nyumba ya Taifa lijielekeze kujenga nyumba wilayani na mikoani ambako mahitaji ya makazi kwa ajili ya wafanyakazi ni makubwa sana. Shirika lijielekeze huko badala ya kuendelea kujenga nyumba Dar es Salaam na miji mikuu ya majiji na manispaa pekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, saba, nashauri Wizara iondoe wafanyakazi wasio waadilifu wanaotoa hati mbili katika kiwanja kimoja; wanaopima maeneo ya wazi na kubadilisha matumizi bila utaratibu; wanaodai rushwa ili kuwapa huduma wananchi ya kupatiwa hati ya viwanja vyao kwa mkoani na wilayani. Pia kupata hati ya kiwanja ni gharama kubwa sana na inachukua muda mrefu sana, naomba nalo liangaliwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nane, maeneo yanayochukuliwa na Halmashauri wananchi walipwe kutokana na thamani ya ardhi kwa wakati huo badala ya kuangalia mazao pekee yaliyoko kwenye kiwanja hicho.