Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mhehsimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kupongeza Wizara hii ya Ardhi ambayo kwa kweli imeonyesha umahiri katika utendaji wake wa kazi, naipongeza sana. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, nitazungumzia zaidi Jimbo la Njombe. Katika Mji wa Njombe kuna tatizo moja kubwa sana, wakati wa Wizara ya Ujenzi niliongea na leo Wizara ya Ardhi naomba niongee. Ninaloliongelea mimi ni zile alama za „X‟, zimewekwa alama za „X‟ kwenye nyumba ambazo Wizara ya Ardhi imetoa hati halali kwa wale wananchi. Matokeo yake ni kwamba zile hati walizonazo wale wananchi wanaendelea kuzilipia na kodi ya ardhi wanalipa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililopo ni kwamba mji ule sasa hivi ni mchafu kwa maana ya kwamba majengo yamechakaa na watu wanashindwa kuziendeleza zile nyumba zao. Kama tunavyofahamu kila mahali penye mji maana yake ndiyo mahali pa biashara, zile nyumba nyingi ni za wafanyabiashara, wanashindwa kutumia zile nyumba kama dhamana katika mabenki kwa sababu tu zina alama za „X‟.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Wizara ya Ardhi kwa kuwa na yeye ni mnufaika na kodi ya ardhi ambayo wananchi wale wanalipa, waone ni namna gani watafanya kutatua tatizo hilo wakishirikiana na Wizara ya Ujenzi. Vinginevyo tukubaliane, barabara ile pale mjini ipunguzwe size, zile alama za „X‟ zifutwe ili wale wananchi waendelee kuzitumia zile nyumba zao kama dhamana katika mabenki kwa ajili ya maendeleo yao na Taifa kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi nyingi kwa Wizara ya Ardhi, liko tatizo la asilimia 30 za Halmashauri ambazo hazirudishwi. Halmashauri yangu ya Mji wa Njombe inadai zadi ya shilingi milioni 60 haijawahi kurudishiwa. Niombe sana Wizara hii iangalie na iweze kurudisha hiyo fedha ambayo Halmashauri imekusanya imeipelekea Wizara na Wizara haijarudisha ile asilimia 30 kwa Halmashauri. Tatizo tunalolipata pale ni kwamba hata kuwahamasisha wananchi waweze kuendelea kulipia kodi hiyo haiwezekani kwa sababu Mkurugenzi hayuko tayari kutoa fedha yake nyingine ili tuhamasishe wananchi walipe kodi ya ardhi ni kwa sababu tu Ardhi wenyewe kama Wizara hawarudishi ile asilimia 30. Kwa hiyo, nikuombe sana kaka yangu Mheshimiwa Lukuvi turudishie hiyo asilimia 30 ili ndugu zako tujenge zahanati kule na wadogo zako waendelee kutibiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lingine tulilonalo Njombe ni bustani za mabondeni maarufu kwa jina la vinyungu. Nafikiri kaka yangu Mheshimiwa Lukuvi unafahamu vizuri sana sheria hii ya mita 60 Njombe inatuathiri sana kwa sababu kwanza mji wenyewe uko milimani halafu wananchi wale walio wengi ni wakulima wanatumia bustani kama sehemu ya kipato kwao. Kwa hiyo, tunapokuja kuwaambia wasilime tayari tunawaathiri kiuchumi na tunavuruga kabisa utaratibu wao wa maisha. Najua hii ni sheria lakini naomba tuangalie jinsi ya kuitekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sababu zinazotolewa wakati mwingine zinakosa mantiki ya kisayansi. Watalaam wanatuambia tusilime mabondeni kwa sababu tunavuruga mfumo wa maji, tunasababisha maji sijui yafanye nini lakini tukumbuke kwamba tumekuwa tukilima kwa muda mrefu, sisi tumezaliwa tumekuta wazazi wanalima maji yale hayajawahi kukauka na yapo vilevile. Sasa hiyo hoja ya kuambiwa tunapungaza maji, tunapunguzaje maji? Kama kuna mahali yamepungua maji ni huko yalikopungua lakini siyo Njombe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine ambalo ni la kitalaam kwamba maji yanatunzwa mlimani, zamani Maafisa Ugani walihamasisha wananchi walime kwa matuta ili kutunza maji kusudi mvua ikinyesha maji yakifika kwenye tuta yatulie yaweze kuzama kwenda chini. Kwa hiyo, yakizama kwenda chini yale maji ndiyo baadaye yanakuja kutoka kule bondeni. Sasa leo tunaambiwa huku juu tulime kwenye sesa au tambarare lakini kule mtoni tusilime, kisayansi hiyo haikubaliki. Naona watalaam wa sayansi warudie tena kufanya utafiti wao ili sisi watu wa Njombe Mjini watuache tuendelee kulima vinyungu kwa ndiyo vinasababisha watu wa mjini mle chipsi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Njombe Mjini tuna tatizo lingine linalohusiana na ardhi. Uwanja wa ndege wa Njombe Mjini uko mjini kabisa. Katika lile eneo la uwanja wa ndege wako wananchi wana nyumba zao pale na wanashindwa kuendeleza nyumba zao kwa sababu tu wanaambiwa wako eneo la uwanja wa ndege na hawalipi maduhuli yoyote ya ardhi.
Naomba Wizara hii ifanye utaratibu tuone kama wale wananchi ni kweli wako ndani ya eneo la uwanja wa ndege waambiwe rasmi wako ndani ya uwanja wa ndege na kama kuna fidia walipwe waondoke. Kama hawapo ndani ya eneo la uwanja wa ndege basi wapewe hati za ardhi ili kusudi waendeleze yale makazi yao na wazitumie zile nyumba zao kwa ajili ya uchumi. Kinyume cha hapo wale watu tunawafanya wanakuwa maskini, nyumba zinachakaa, wanaishi maisha ya wasiwasi wakiamini kwamba kuna uwanja wa ndege pale na wenyewe watu wa uwanja wa ndege hawasemi lolote juu ya maendeleo ya ardhi ile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo na mimi niseme kidogo kuhusu Shirika la Nyumba la Taifa. Shirika la Nyumba la Taifa walifika Njombe kutafuta eneo la kujenga nyumba na wakaonyeshwa eneo lakini kwa bahati mbaya sana ninasikitika kwamba Shirika la Nyumba hawajarudi tena Njombe. Taarifa niliyonayo ni kwamba walihitaji wapewe eneo la bure sasa Njombe eneo la kutoa bure halipo. Kwa hiyo, niwaombe sana Shirika la Nyumba, wakiona eneo lina thamani maana yake hata nyumba watakazojenga zitakuwa na thamani hivyo hivyo. Naomba waje tena Njombe wachukue lile eneo ambalo tumelitenga kwa ajili yao lakini watulipe fidia kwa sababu eneo la bure halipo na wao kwa upande mwingine zile nyumba si wanaziuza, kwa hiyo ni biashara. Kwa hiyo, wasione kwamba wanatakiwa wapewe eneo la bure kama fidia ya gharama za uendeshaji wa shirika lao, hapana, wasifanye namna hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Shirika la Nyumba hilo hilo wengi wamesema kwamba nyumba zao ni za ghali sana, ni kweli nyumba zao ni ghali sana. Hatufahamu sana ni gharama gani wanaingia lakini nafikiri shirika lijipange vizuri tu ifike mahali liwe na mifuko miwili, mfuko wa kuuza hizo nyumba za gharama lakini liwe na mfuko kwa ajili ya nyumba za wanyonge. Kwa hiyo, lijenge nyumba za wanyonge ili wanyonge wapate nyumba. Tusipofanya hivyo shirika litaendelea kulaumiwa lakini na lenyewe linashindwa kufanya vinginevyo. Niwaombe sana Shirika la Nyumba wasife moyo, wajitahidi lakini wasisahau kufika Njombe tuwape eneo lile lakini watulipe fidia ili waweze kujenga nyumba zile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niseme na mimi naunga mkono hoja, ahsante sana.