Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii kwa mara nyingine niweze kutoa mawazo yangu katika kuunga mkono hotuba nzuri ya Waziri wetu wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mheshimiwa William Lukuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu Waziri Lukuvi aingie katika Wizara hii tumeona mabadiliko makubwa na tuna matarajio makubwa ya kuona mambo mengi yakiwekwa sawa hasa suala zima la maandalizi ya kuipanga upya nchi yetu. Nchi yetu imeingiwa na tatizo moja ambalo kimsingi tulikuwa tumeepukana nalo la mapigano ya sisi kwa sisi. Suala la ardhi limeonekana kuwa ni chanzo cha migongano baina ya wananchi, wafugaji na wakulima. Jambo hili lisiposhughulikiwa vizuri linaweza likawa chanzo cha vurugu nchini, chanzo cha kutoweka kwa amani iliyojengeka kwa muda mrefu katika nchi yetu. Kwa hiyo, ndugu yangu Mheshimiwa Lukuvi na wataalam wako nashauri kwa kweli speed uliyoanza nayo endelea nayo. Kwa wale watu ambao wanakuwa na ardhi ambayo wanaimiliki bila kuiendeleza basi hatua unazochukua za kuwanyang‟anya ardhi na kuwapatia wananchi ambao hawana ardhi uendelee nazo na kasi yako isirudi nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba yapo maeneo mapya ya utawala, tuna Mikoa mipya ya Geita, Katavi, Simiyu na sasa Njombe pamoja na Mkoa mpya wa Songwe. Naomba maeneo haya ambayo yameanza upya pamoja na Wilaya zake mpya basi Wizara iyatazame kwa upya ili kusudi yawezeshwe kuwa na master plan pamoja na upimaji wa kisasa, tusije tukajikuta tena kwamba maeneo haya yameanza upya lakini yakapata athari ile ile ambayo imeikuta mikoa mingi kabla ya utaratibu huu mzuri ambao umekuja nao wa kuwa na hii unayosema ni Integrated Land Management Information System. Jambo hili ni la kisasa ina maana kwamba kutakuwa na takwimu nzuri kabisa za matumizi mazuri ya ardhi ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana kusema tu wazi kwamba Wizara hii ni mama ambapo kila Wizara na Idara ya Serikali haiwezi ikafanya kazi zake bila kushirikiana na Wizara hii ya Ardhi. Iwe Wizara ya Ujenzi, Wizara ya Miundombinu, Wizara ya Mazingira, zote zinategemea uwepo wa mipango mizuri ya matumizi ya ardhi inayofanywa na Wizara yetu hii ya Ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba nchi yetu sasa imekuwa ni kitovu cha wawekezaji, watu wengi wanavutiwa kuja katika nchi yetu. Ni jambo jema na ni la kheri lakini kheri inaweza ikapata tena kikwazo pale inapotokea mwekezaji amekuja kama mgeni wetu lakini anafika mahali anaanza kuwa ni chanzo cha ugomvi baina yake na wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili naomba sasa Serikali yetu kupitia Wizara yetu ya Ardhi ilitilie maanani kwa kuanzisha utaratibu wa kuwa na benki ardhi kwamba kuwepo na maeneo ambayo yametunzwa kama Special Economic Zones ambapo mwekezaji yeyote anayekuja aelekezwe mahali ambapo atafanya kazi zake kwa amani. Hali hiyo itatujengea heshima kwa wageni wetu na kwa mataifa mengine ya nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo niishie hapo, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Niwapongeze tu ndugu zangu Mawaziri na sisi kama Wabunge tuko pamoja na tuko nyuma yao. Mungu akubariki sana.