Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii kutoa mchango wangu mdogo. Niseme tu jambo moja kwamba nimepitia hotuba ya Bajeti ya Wizara hii, nimepitia hili begi ambalo tumepewa, nilikesha, nimesoma vizuri sana. Nimepata matumaini makubwa sana kama mtaalam wa ardhi tumetukanwa kwa miaka mingi kwamba hatufanyi chochote, kazi zetu ni kusababisha migogoro, kuuza viwanja na kadhalika, lakini nimepata matumaini makubwa niliposoma makabrasha haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kitu kimoja kwamba nimeridhika sana na kitabu hiki cha Mpango wa Taifa wa Matumizi ya Ardhi. Hili ndilo suluhisho pekee, hiki kitabu ndilo suluhisho pekee la migogoro na kila mmoja sasa tukitekeleza hili tutaishi kwa amani katika nchi hii na kila mmoja atafaidi kipande cha Ardhi ambacho atapewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kushauri yafuatayo ili kutekeleza mpango huu:-
Kwanza, naomba tutunge sheria moja tu inayo-govern suala la ardhi. Hatuhitaji Sheria ya Ardhi namba tano ya Vijiji, sheria namba tano ya vijiji tunaomba tuifute, inaleta migogoro mingi na ardhi ya vijiji ni sehemu kubwa kuliko hata ile nyingine iliyobaki. Hatuwezi kusema ardhi ya vijiji, ya mjini ardhi ni ardhi tu, tafadhali sana tukishatunga sheria hii utekelezaji wa sheria ufuatwe. Kila mmoja wetu, Mbunge, watendaji, wale watu wa vijijini naomba tutekeleze Sheria ya Ardhi, tusimamie utekelezaji wa ardhi. Sheria nyingi nzuri zimetungwa ziko kwenye makabrasha, sheria nyingi nzuri lakini bila utekelezaji, ni kazi bure, naomba hili mlishike sana wenzetu mliopewa dhamana hii kwa maana ya Wizara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye mpango huu, tuajiri wataalam wa kutosha wanaoshughulikia mambo haya. Vyuo vyetu vimetoa watu wa kutosha, Chuo Kikuu cha Ardhi, Morogoro, Tabora wametoa wataalam wa kutosha, wako mitaani tunawaona. Ajirini wataalam hawa waje kusimamia mpango huu. Inatia mashaka na inasikitisha sana mnapounda mabaraza vijijini mnakamata tu wazee pale kwamba wewe mzee ndiyo utakuwa Mwenyekiti. Hivi unaweza ukaenda dispensary pale ukakuta tu mzee anatibu hajasomea uganga?
Mheshimiwa Mwenyekiti, unakwenda kule mahakamani unakuta tu mtu anatoa hukumu hajasoma mambo ya Sheria? Kwa nini tunakabidhi suala hili zito la ardhi watu ambao hawajasoma? Yaani ardhi tunaidharau kiasi hiki? Ardhi ambayo ni muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wataalam wa-play kila mahali kuanzia vijijini mpaka huku Taifa. Watu wamesoma, hii ardhi ni taaluma hatuwezi kucheza na ardhi, hatuwezi kukabidhi mtu ambaye hana ajira na hana liability yoyote yaani hatuwezi kumbana. Unapomwajiri mtu ambaye ni mtaalam atakuwa anasema mimi ni mtaalam, lakini pia nimeajiriwa, nalinda kibarua changu. Sasa unampa tu mtu unamkamata barabarani wewe utakuwa mshauri kwenye Baraza la Ardhi haiwezekani, liability iko wapi, lazima atavuruga tu ndiyo maana ya kwenda shule, naomba tulizingatie hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukishakwenda kwenye mpango huu maana yake ni kwamba, sasa tukapime ardhi ya nchi nzima. Nimepitia kwenye mpango huu nadhani kuna pilot project kwenye wilaya karibu 63, mmeweka mipango hii, lakini nasema hivi tukapime nchi nzima, siyo wilaya kadhaa, wala manispaa kadhaa , wala halmashauri kadhaa, twendeni tukapime nchi nzima, tutumie wataalam wetu kwenye halmashauri zetu, wapo wataalam, kama hawapo tuajiri kama nilivyosema tukaipime nchi nzima ipimwe sasa siyo kupima maeneo mengine na maeneo mengine kuachwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimefurahishwa kwenye mpango huu, jambo ambalo litatuondolea migogoro ni kwamba, tupime ardhi kwa uwiano hasa ardhi ya kilimo na ardhi ya ufugaji ipimwe kwa uwiano. Fanya sensa ya mifugo mahali, angalia ardhi iliyopo pima ile ardhi wagawiwe wafugaji kwa mujibu wa idadi yao na idadi ya mifugo na ardhi iliyopo. Hesabu wakulima wako wangapi, pima ardhi iliyopo kwa ajili ya kilimo kwenye eneo husika kama ni wilaya kama ni kijiji igawe ardhi kwa uwiano wa idadi ya wakulima waliopo hilo litaondoa migogoro, tugawe ardhi kwa uwiano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo nadhani tukienda hivyo migogoro haitakuwepo na iwekwe kwenye sheria hii ambayo tunakwenda kuitunga hasa kwenye kilimo na ufugaji kumekuwa na mgogoro mkubwa sana, gaweni ardhi kwa uwiano. Siyo mfugaji mmoja anayemiliki maekari na maekari na wengine hawana ardhi. Mkulima mmoja anamiliki maekari na maekari wengine hawana ardhi katika kijiji, tugawe ardhi sasa kwa uwiano, kwa mujibu wa sheria na tusimamie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, change of land use, hasa nazungumzia eneo ambalo limepimwa. Suala hili limekuwa na mgogoro mkubwa sana, sheria zimetenga kabisa upimaji ule kwa mfano kwenye miji umetenga maeneo mazuri, maeneo ya makazi, ya biashara, ya viwanda na ya kumwaga takataka. Zile plan zinakuwa vizuri mnapoanza. Kwa mfano, mradi wa viwanja 20,000 ukiuangalia zile ramani ziko vizuri lakini ukienda sasa hivi kwenye utekelezaji yaani ile plan imeshavurugika tayari watu wanabadilisha matumizi ya ardhi bila utaratibu. Sheria ipo ya kubadilisha matumizi kwa kufuata sheria na kanuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi nenda kwenye makazi ya watu miziki inadundwa mpaka saa nane, saa tisa za usiku kwenye maeneo ya makazi. Petrol station zinajengwa kwenye maeneo ya makazi kinyume na ile plan ya zamani. Watu wabadilishe matumizi ya ardhi kutokana na sheria na sheria ipo tulinde plan zetu maeneo ya wazi yameshajengwa, yanavamiwa hovyo. Eneo lilitengwa kwa ajili ya shule, watu wamejenga maeneo ya biashara tunakwenda wapi, mbona sheria zipo? Enforcement of laws ni jambo la muhimu sana katika ku-plan mambo ya ardhi, naomba sana tuzingatie.
Mheshimiwa Mwenyekitii, mwisho, kule kwangu Manyoni kuna mgogoro wa ardhi, kati ya wananchi na Hifadhi ya Muhesi-Kizigo, ndiyo haya mambo niliyokuwa nayazungumza. Mgogoro wetu ni tofauti kidogo na maeneo mengine, sisi tunagombana na hifadhi kwa sababu ile hifadhi walitunyanganya lile eneo wakapanua ule mpaka wakala kijiji, wakala maeneo ya malisho ya mifugo, wakala maeneo ya kilimo kule Manyoni. Huo ndiyo mgogoro wetu, sisi hatuombi kuongezewa kumega hifadhi hapana, tunaomba mpaka wetu ule wa zamani urudishwe, hilo tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana wakati Mheshimiwa Waziri anahitimisha huu mgogoro wa Muhesi Kizigo na wananchi wa Manyoni wanaoishi pembezoni mwa ule mpaka, wanaomba sana warudishieni ule mpaka wa zamani, yale mashamba yao yamebanwa, hawana pia maeneo ya kulisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna unyama mkubwa sana wa hawa wenzetu wanaolinda yale maeneo, nadhani hili linamhusu Profesa Maghembe, hili eneo Wizara ya Maliasili na Utalii kile kikosi wanaenda kinyume kabisa na sheria za kibinadamu. Unakuta mtu amejenga nyumba, ameweka makenchi yake, wanapanda juu wanashusha makenchi, hizo kenchi unajuaje kama mtu alinunua mbao zimegongwa mihuri wa kibali au hapana mtu amepandisha kenchi wewe unaenda unashusha, kweli? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu ameshachonga madirisha mnakwenda mnachukua yale madirisha mnapiga watu, mama tu ameingia kuchukua kuni pale anapigwa mpaka anazimia na anakwenda kufunguliwa kesi. Ninazo kesi nyingi pale Manyoni yaani kuna watu wamejaa pale kwenye mahabusu ya Manyoni. Hivi ni balaa kupakana na hifadhi? Naomba tafadhali sana hebu tufuate sheria na toeni pia elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ule mpaka haujulikani, yaani ukienda nionesheni mpaka hifadhi ni wapi inapoanzia na kile kijiji kinapoanzia hawawezi kuonesha. Kwa hiyo, naomba sana wana Manyoni wanasema rudisheni ule mpaka wa zamani kule ambako ulikuwepo, muwaachie mashamba yao na eneo lao la kulima. Pia wekeni ule mpaka unaoonekana, pandeni hata miti, kule Bukoba wanaita bilamla, kule Manyoni tunaita machito, weka mpaka hata chimbia hata miti, hata vile vinguzo, panda hata minyaa angalau kuwe na mpaka unaoonekana kwamba hapa ndiyo mwisho, hii itapunguza sana migogoro.
Mheshimiwa Mweyekiti, mwisho kabisa, nirudie kwa kutoa wito kwamba mpango huu ni mzuri tujipange vizuri kama nchi twendeni tukaipime Tanzania, tuiweke kwenye ramani, tuepushe migogoro, mpango huu unatekelezeka na ni mzuri sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.