Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Sixtus Raphael Mapunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia asubuhi ya leo. Awali ya yote, nichukue fursa hii kama walivyosema waliotangulia kumshukuru sana na kumpongeza Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Comrade William Vangimembe Lukuvi. Kwa kweli ukiitazama Wizara yake, ukitazama majukumu yaliyopo katika Wizara hiyo na jinsi anavyofanya kazi na ile flexibility yake ya kwenda kwenye migogoro ya ardhi, kwenye masuala yanayohusu ardhi kila kona ya nchi yetu, kwa kweli inatupatia matumaini makubwa. Huenda mwarobaini wa migogoro ya ardhi ndani ya nchi yetu umeshapatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya ya utangulizi, naomba nijielekeze kwa kifupi kwenye mambo matano ambayo naomba Serikali iyatazame kwa kiwango cha hali ya juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ardhi ya nchi yetu ipo vile vile ila inapungua kutokana na shughuli za bahari, size inapungua, lakini binadamu wanaongezeka kila kukicha. Kwa hiyo, watu wanazaliana, wanaongezeka, lakini ardhi bado ipo vile vile. Tusipokuwa na mpango mahususi wa kuitazama Tanzania ya leo, ya kesho na ya miaka 50 ijayo, tutakuja kuzalisha migogoro ya ardhi ambayo tutashindwa kabisa kuja kuituliza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona miji inakua, sasa hivi Jiji la Dar es Salaam limekua katika kiwango cha hali ya juu, sasa linatusumbua jinsi ya kupanga. Wapi upitishe barabara, ni shughuli! Wapi upitishe maji safi, ni shughuli! Wapi upitishe maji taka, ni shughuli! Wapi upitishe nguzo ya umeme, ni shughuli! Hata sasa tunapotaka kwenda kwenye huo mpango wa gesi ambapo inapita kama mtandao wa maji, tutashindwa kwa sababu kila utakayemgusa, utalazimika kumlipa fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea Dar es Salaam lingekuwa ni kosa letu la mwisho kufanya kwenye miji mikubwa na miji inayofuata yote isiwe na matatizo ambayo yametukuta Dar es Salaam. Sasa tunaona majiji yanayokuja tena, yanapita kwenye matatizo yale yale ya Dar es Salaam. Nenda kaangalie Tanga, matatizo ni yale yale; Arusha inakuja kwa kasi, matatizo ni yale yale; Mwanza ndiyo kabisa, tena itafungana kuliko Dar es Salaam; nenda kaangalie Mbeya, matatizo ni yale yale. Sasa namwomba Mheshimiwa Waziri na Serikali, hii miji inayokua na ambayo mingine tuna-predict baada ya miaka 10 itakuwa miji mikubwa, tumalize mpango wa ramani ya miji. Miji ijulikane itakuwa na sura hii, tusirudi tena kwenye migogoro iliyopita huko nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii unaenda kutatua mgogoro wa Kigamboni; Kigamboni imekuwa darasa zuri sana kwenye mipango miji. Tupange mji, barabara itapita wapi, nyumba itakuwa wapi, uwanja utakuwa wapi na ikiwezekana twende kwenye hatua ya pili; na ramani ya nyumba pale iweje? Sasa atakapofika mtu apate kiwanja chake ajenge nyumba kwa mujibu wa ramani jinsi ilivyo. Tunazunguka nchi za watu, tunaona haya mambo yapo, siyo mageni. Namwomba Mheshimiwa Waziri alipe kipaumbele hili suala, litaweza kuja kutusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, hii Wizara ina changamoto kutokana na centers nyingi za decision making kwenye ardhi. Kijiji kina mamlaka, Halmashauri ina mamlaka, Wizara ina mamlaka. Ukiondoka kwa upande mwingine, unakwenda kwenye Wizara nyingine, ina mamlaka vile vile kwa mujibu wa sheria kwenye ardhi hiyo hiyo. Sasa matatizo ya Wizara moja au matatizo ya sehemu moja yenye mamlaka kisheria, yanaweza yakapelekea madhara kwenye eneo lingine.
Kwa mfano, migogoro ya ardhi kati ya wakulima, wafugaji na hifadhi, unakutana na Wizara tatu ziko kwenye sakata moja; unakutana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, unakutana na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi; unakutana na Wizara ya Maliasili na Utalii; unakutana na TAMISEMI tena nao wapo humu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi Wizara nne zisipokaa zikajadili kwa kina, zikaona baadhi ya sheria nyingine ambazo tunaona zinaleta migongano ya kimaslahi, migongano ya kimadaraka zifutwe, hatutatoka hapa. Leo hii ninavyoongea, kule Mbinga tuna mgogoro wa ardhi. Halmashauri inamiliki ardhi ina mamlaka ya kupima kama kawaida kwa mujibu wa sheria; kijiji kimemkaribisha mwekezaji kwenye ardhi ambayo wapo pale wanakijiji. Baadhi ya wanakijiji wamekubali kumpokea mwekezaji, wengine hawataki. Imekuwa ni mivutano mikubwa. Sasa Wizara huku juu wanaweza wakadhani kule chini mambo yanakwenda sawasawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Kigonsera, Kijiji cha Mihango, Waziri anaweza akaja akapatiwa maafa ambayo kwa kweli yatakuwa hayawezi kuelezeka kwa sababu pale wanakijiji wapo juu wanakasirika kwa nini mwekezaji anakuja? Tunatambua kwamba wawekezaji ni muhimu sana katika Sekta ya Kilimo, nami na-encourage sana waendelee kuwepo kwa sababu kweli kuna mambo mengi tunayapata kupitia hawa watu, isipokuwa uelewa wa watu wetu, ukoje. Hii mifumo ya mamlaka katika ardhi inakuwa ni kikwazo kikubwa sana kuiwezesha Wizara yako kufanya kazi smoothly katika speed ya Mheshimiwa Waziri. Nawaomba wafanyeni watakaloweza kulifanya, hao wanne ambao ni wadau wakubwa wa ardhi, wakae, wapange mpango mzuri, tukitoka hapo mambo yatakwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, migogoro mingi ya ardhi ndani ya nchi yetu ina uhusiano na nani mmiliki? Nani kapima? Kapima wapi? Kwenye Halmashauri zetu, wana mamlaka ya kupima ardhi, lakini uwezo wao wa kupima ardhi ni mdogo. Naiomba Wizara itengeneze program maalum ya kutafuta vifaa vya upimaji kwa nchi nzima. Ikishapata hivyo vifaa vya upimaji kwa nchi nzima, kwa sababu kila Halmashauri tuna Maafisa wa Mipango Miji, waende wapime ardhi yote kusiwe na mgogoro, eneo la makazi mtu akitaka kununua kiwanja aende sehemu tayari kimeshapimwa, akalipie apate hati yake, ajenge aendelee na maisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwangu pale maeneo ya Lusonga, Mji sasa unakua ardhi haijapimwa. Ukienda Lusewa, Mji wa Mbinga unakua, hakuna kupima. Ukienda Mateka, Kilimani, Tanga, Luwaita, haya maeneo yote ya miji hayajapimwa. Kesho mji utakuwa mkubwa, tutakuja kwenye migogoro mikubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nadhani litakuwa la mwisho, nisemee kuhusu ujenzi wa hizi nyumba za bei nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, naipongeza Serikali kwa kuifufua sasa National Housing Corporation i-operate katika kiwango cha hali ya juu. Tunaona nyumba zinajengwa lakini zile nyumba hazinunuliki. Mtu wa kawaida hawezi akanunua kabisa, ni ghali! Mbaya zaidi, tumeingia katika mortgage financing, mtu anakwenda kukopa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba akajisitiri, anaenda kwenye mkopo wa riba kwenye hiyo nyumba; yaani unanunua nyumba una riba, Nationa Housing Corporation wamechukua vifaa kwa ajili ya ujenzi wa ile nyumba, wanakatwa Value Added Tax kwenye yale mambo, ukiyaweka yale yote gharama zinakuwa kubwa sana. Hii siyo njia sahihi ya kumsaidia mtu kwenye ujenzi wa nyumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kitu kimoja kifanyike. Kama Serikali, tumeamua sasa tujenge nyumba za bei nafuu, twende kwenye mambo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, tuiwezeshe National Housing Corporation ijenge kwa pesa zake, iuze na ipangishe. Zile nyumba zilizokuwepo miaka ya 1960 na 1970 mbona ilikuwa hakuna mambo kama haya tunayoyaona leo! Tuna flats zipo kila sehemu, ukiuliza wanasema hii ya National Housing Corporation, kila Mkoa zilikuwepo! Namwomba Mheshimiwa Waziri, najua haya mambo anayaweza. Kaa na National Housing Corporation, wasikilize changamoto zao, waweke vizuri wajenge nyumba za bei nafuu ili kila Mtanzania sehemu ya kulala isiwe tatizo tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja.