Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata nafasi hii ili niweze kuchangia hii Wizara muhimu ya Ardhi. Napenda kwanza kuanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kazi nzuri waliyoifanya na pia, kwa kuangalia hata orodha ya migogoro ambayo ametupa, inaonesha ni namna gani amejikita kuhakikisha kuwa, matatizo yote ya ardhi atayatatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hii orodha ambayo ametupa leo, katika Wilaya ya Mbeya kuna mgogoro wa muda mrefu sana kati ya Kijiji cha Kikondo na Hifadhi ya TANAPA. Waziri alitoa maelekezo kuwa wakae, ili waweze kuitatua na Serikali ya Wilaya walikaa pamoja na hifadhi kwa ajili ya kulitatua hilo tatizo, lakini tatizo linaelekea ni kwa hawa TANAPA, wamekataa kuwalipa wananchi! Wanapiga danadana! Namwomba Mheshimiwa Waziri, ajaribu kuongea na Waziri mwenzake wa Maliasili ili walitatue hili tatizo! Wananchi wako tayari kuwaachia TANAPA eneo hilo kwa ajili ya hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wenyewe sasa hivi wanasema kabla ya bajeti hii kwisha waambiwe watapata fidia au hawatapata fidia ili waweze kuendelea na shughuli zao za kilimo! Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aje na hilo na kama haiwezekani kupata fidia, ile ardhi ni mali kwetu tunahitaji kwa ajili ya kuendeleza kilimo. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hilo kwa umuhimu mkubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lingine ni kwenye mgogoro wa Wilaya ya Mbozi na Wilaya ya Mbeya kwenye Kitongoji cha Mtakuja kilichopo Kijiji cha Mjele. Hili ni tatizo la muda mrefu, naomba sana Mheshimiwa Waziri, hujaorodhesha kwenye hii orodha yako na kuna matatizo ambayo ni makubwa! Vilevile kuna hifadhi ambayo haieleweki kama ni hifadhi! Kwa vile wananchi walivamiwa pale, ng’ombe wao wakachukuliwa, nyumba zao zikachomwa moto na mpaka leo hatuelewi nini kinachoendelea!
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tatizo waliolishughulikia ni Wilaya nyingine, Serikali ya Wilaya ya Mbozi badala ya Wilaya ya Mbeya! Hilo ni tatizo kubwa. Kitongoji kizima wananchi walishachomewa nyumba! Ng’ombe wao hawajarudishiwa mpaka leo! Naomba Wizara iangalie, hilo ni tatizo kubwa linavuruga sana Wizara, inaonekana kama nayo ni sehemu ya migogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la Mipango Miji. Kama Mheshimiwa Waziri alivyoelezea kwenye Kitabu chake cha Hotuba, ameelezea vizuri sana ni mipango gani ambayo wanayo kuhakikisha kuwa wanaendeleza mipango miji na vijijini. Kuna suala la miji midogo, naomba liangaliwe sana liwekwe msisitizo kwa vile hii ndiyo Wizara Mama ya kuangalia hayo masuala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna upungufu sasa hivi wa ardhi, Mji Mdogo wa Mbalizi umepanuka kiasi kikubwa mno kutoka wananchi chini ya 10,000 sasa hivi ni zaidi ya 100,000. Sehemu hata ya kujenga shule, huduma mbalimbali hakuna! Vituo vya Huduma za afya hatuna, lakini kuna eneo kubwa karibu hekta 2,000 ambayo ilikuwa ni eneo la Tanganyika Packers. Naomba hilo nalo Mheshimiwa Waziri alitatue haraka. Uzuri wake katika Sheria alizotupa leo nimeangalia katika Sheria ya mwaka 2007, hili shamba halitakiwi likae mjini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Halmashauri ya Mbeya wametenga eneo lingine mahususi kwa ajili ya kunenepeshea ng’ombe. Tunaomba hili eneo ipewe Halmashauri ya Mbeya ili waliendeleze na waweze kuwalipa wale wananchi ambao walikuwa hawajalipwa malipo yao ya fidia. Hili liwe la haraka, hili ni eneo muhimu kwa vile ndiyo linapakana na kiwanja chetu cha Songwe. Kwa usalama nafikiri ni eneo ambalo linahitaji liboreshwe, ili na mazingira vilevile ya kiwanja cha Songwe ambacho ni International Airport kiwe kimezungukwa na eneo ambalo linaleta sura nzuri ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la TAZARA; kama alivyosema mwenzangu ambaye hakumalizia, tuna tatizo la Sheria zetu ambazo wananchi hawaelimishwi. Mheshimiwa Waziri, TAZARA ilikuwa na hifadhi ya mita 30 kila upande, sasa hivi zimeongezwa 20 kila upande! Wananchi hawakuelimishwa! Wananchi hawajapewa fidia! TAZARA yenyewe iko hoi! Badala ya kufanya shughuli za usafirishaji wanafanya shughuli za kuonesha kwamba, wanawatishia wananchi kubomoa nyumba zao!
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kabla haya masuala ya kubomoa nyumba kutekelezwa wananchi kwanza waweze kupata fidia zao. Elimu kwanza itolewe, hii kusema ignorance of law is not defence! Kwa sisi wananchi wetu zaidi ya 80% wanaishi vijijini, unategemea hizi Sheria wataziona wapi? Hizi Sheria zimefichwa na sijui zimefichwa wapi? Siku ya kubomolewa ndiyo unaambiwa kuna Sheria ya mita 30. Naomba hilo liangaliwe na hatua zichukuliwe; kwanza ya kuwashughulikia watu wa TAZARA na hawa wananchi wapate fidia zao. Hayo maeneo ni ya Mji Mdogo wa Mbalizi na Kata ya Inyala, naomba hilo lishughulikiwe haraka iwezekanavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la mortgage finance. Hizi mortgage finance kwa sisi watu wa vijijini zitatufikia namna gani? Sisi asilimia 80 ya Watanzania tutapata vipi hii mikopo? Au nchi hii ni kwa ajili ya watu wachache wanaoishi mijini? Hatuoni hata siku moja tukaelimishwa kuwa kuna mikopo! Naomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuwapongeza National Housing Corporation, wanafanya kazi nzuri, ina management nzuri, ni mfano wa Watanzania ambao wanaweza ku-transform Shirika la Umma likafanya vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja.