Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Ardhi. Kwanza kabisa nimpongeze Rais wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kumchagua Mheshimiwa Lukuvi kuwa Waziri wa Ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais hakufanya makosa, amemchagua Mheshimiwa Waziri mwenye uzoefu mkubwa anayejiweza, yuko makini na tuna imani naye. Pia amemchagua Mheshimiwa Naibu Waziri ambaye ni mwanamama, dada yetu Angelina Mabulla tuna imani naye kubwa sana, tunamtambua vizuri na yeye yuko makini na tuna imani naye kwamba atatusaidia sana sisi wanawake katika matatizo yetu mbalimbali ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama Mbunge wa Viti Maalum ninayetokea katika Halmashauri ya Temeke, kwanza kabisa nitaanza kuzungumzia tatizo la Kurasini. Hii Kurasini hivi Serikali inatambua hayo maeneo ya Kurasini ambayo tunayapigia makelele humu ndani? Mimi ni Mbunge takribani sasa hivi ni miaka sita, kila tulipokuwa tunazungumza kwenye Wizara hii lazima tuizungumzie Kurasini. Kurasini wengine imetuchanganya, imetufanya tukose Diwani wa Chama cha Mapinduzi, imetufanya tukose Mbunge wa Chama cha Mapinduzi, kisa ni malalamiko ya watu wa Kurasini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kurasini watu wale wako kama wako kisiwani, wamezungukwa na magari, matakataka, sijui uchafu wa aina zote, lakini wananchi wale wenyewe kwa jitihada zao wamekwenda kutafuta mtu, wewe mwekezaji tuondoe, kama wananchi wale wamemtafuta wenyewe mwekezaji, hivi Serikali inaona kigugumizi gani kuwatoa wale watu pale, maisha yale ni hatarishi hayafai kuishi binadamu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali kweli ina mipango yake na mipango yake ni mizuri kwamba Kurasini liwe eneo ambalo la uendelezaji na uwekezaji tu wa kibiashara, sasa tunasita nini? Serikali imefanya jambo kubwa sana pale kuweka kile kituo cha biashara, wamewalipa watu mabilioni ya pesa wamekwenda vizuri sasa tumekula ngombe mzima, tunashindwaje mkia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Chama changu cha Mapinduzi, tutakapomaliza Bunge hili aende Kurasini akawaangalie wananchi wale na ayajue matatizo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nizungumzie suala zima la Keko, leo Mheshimiwa Mbunge wa Temeke amewabeba wananchi wa Keko amewaleta hapa, mimi kama Mbunge ambaye niko miaka sita sioni la ajabu, wananchi hawa tumewasemea kuanzia Halmashauri kuhusu ugomvi wao na National Housing. Wameambiwa watatolewa pale watafanyiwa hivi, yote yamekwenda hakuna kinachoendelea, leo linabebwa kundi la watu linaletwa Dodoma, Mheshimiwa Waziri anataka kuwaambia nini, nataka aseme hapa ndani leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watu wa Keko mgogoro wao Mheshimiwa Waziri auseme hapa ueleweke wazi, vinginevyo tunaonekana sisi tunaokaa humu hatufanyi kazi, kumbe kusema tunasema lakini majibu hayapo. Leo Mheshimiwa Mbunge ana miezi sita sijui ya kuingia humu Bungeni, amebeba kundi analileta hapa ndani, mimi kama Mbunge niliyekuwa humu ndani naona hiyo siyo ajabu. Leo Mheshimiwa Waziri wangu hapa nataka aeleze mgogoro huu National Housing na Keko, hapa ndani ya Bunge wala sitaki akasemee huko vichochoroni, aseme hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nichangie kwenye suala zima la kodi za ardhi. Mheshimiwa Mbunge mwenzangu pale amezungumzia, lakini nataka nirudie, hizi kodi za ardhi zimekuwa tatizo kwa wananchi. Mwananchi anakwenda kulipa anaambiwa sijui lipa premium fee shilingi ngapi sijui! Lipa sijui registration! Unaenda na pay slip sita! Serikali ileile jamani Eeh! Halmashauri, Serikali, Wizara, mtu anapewa vidude vile vya kulipia hata haelewi, wengine ni wazee, ni usumbufu wa hali ya juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri arekebishe. Hivi zile kodi zikilipwa pamoja hawa wahasibu wa Halmashauri na Wizara wanafanya kazi gani? Kwa nini wao wasije huko ndani wakazigawanya? Mtu anatumwa, yaani ni kuchanganyikiwa! Shilingi 1,000 peke yake! Shilingi 300 peke yake! Shilingi 3,000/= sijui peke yake! Hii si shida tu hii? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nizungumzie uendelezwaji wa Mji wa Kigamboni, Wabunge wenzangu wamesema, Mwenyekiti wa Kamati amesema na mimi inabidi niseme. Napata kigugumizi, hivi huu mji upo au haupo? Kama upo kwa nini, wanasema kwamba, ile ofisi iondolewe? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naelewa kabisa Mheshimiwa Waziri katika watu waliotusaidia kupata Wilaya ya Kigamboni na yeye anahusika kutokana na huu Mji wa Kigamboni. Kigezo kikubwa tuliona kwamba, ule Mji wa Kigamboni lazima upate Wilaya yake ili uweze kwenda vizuri. Sasa leo wanalolitenda, hivi Serikali kwa nini iliamua kutuambia kwamba, wanatuwekea Mji wa Kigamboni na sisi wananchi tunautaka, leo unasema ule mji ufutwe? Nataka maelezo ya kina uanzishwaji wa Mji wa Kigamboni umefikia wapi? Nataka Mheshimiwa akija hapa anieleze! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nije kwenye suala zima la National Housing na kodi zao. National Housing gharama za kodi ni kubwa! Unakuta nyumba moja Ilala, Buguruni, Temeke, Magomeni, Manzese, nyumba moja analipa mtu shilingi 320,000 kodi ya mwezi shilingi 280,000! Hivi kweli lengo la kuwekwa National Housing si ndiyo Mtanzania aweze kupata nyumba ya gharama nafuu! Leo Kariakoo majumba ya wananchi wa kawaida yameshuka bei yako chini kuliko ya National Haousing. Nataka nipate majibu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine wanatujengea nyumba National Haousing, ndiyo wanafanya vizuri, lakini zile nyumba ni ndogo sana, vyumba kama box, ni vidogo sana ukilinganisha na familia zetu za wananchi wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.