Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia katika Mpango huu wa Maendeleo wa mwaka mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuzungumza lolote, naomba kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kuwa Mbunge …
MWENYEKITI: Nataka tu Jimbo Mheshimiwa.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mtwara Mjini.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru kwa kunibariki kuwa Mbunge wao. Pili, naomba niwashukuru wananchi wangu wa Mtwara Mjini kwa kuniamini na nawaambia waendelee kuniamini nitawawakilisha vyema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia hoja, naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Mtwara Mjini kumetokea maafa, mvua imenyesha, kuna mafuriko na jana nilitoa taarifa hii kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba Waziri husika ashughulikie suala hili, kuna nyumba zaidi ya 500 zimeharibika. Nachukua fursa hii pia kuwapa pole wananchi wote walioathirika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuchangia kama ifuatavyo. Mpango huu umezungumzia suala zima la viwanda na Mheshimiwa Waziri wakati anatoa hoja alisema kuna utaratibu wa kuhakikisha inatawanya viwanda kila eneo la nchi. Pia alisema kuna maeneo ni special investment zone kwa maana kwamba ni ukanda maalumu wa uwekezaji na akataja Mtwara, Bagamoyo na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Mtwara Mjini kuna Kiwanda cha Dangote. Kiwanda hiki kina wafanyakazi wengi lakini kwa masikitiko makubwa kabisa mle ndani kuna kampuni tatu za Wahindi na Wachina, kuna AYOK, UCC na CYNOMA. Naomba nimpe taarifa Waziri husika kwamba kampuni hizi zilizopo mle ndani zinanyanyasa wafanyakazi. Sijui ni utaratibu gani huu wa kwamba tunajenga viwanda badala ya kuwanufaisha Watanzania vinawanyanyasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine katika Kiwanda hiki cha Dangote, lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba inaondoa umaskini kwa wananchi wa maeneo husika. Kwa kiasi kikubwa kiwanda hiki kinaajiri watu lakini wenyeji wa Mtwara wengi hawapati nafasi. Mimi kama Mbunge nimejaribu kutembelea kiwanda hiki zaidi ya mara mbili kwenda kuzungumza na Maafisa Masuuli lakini kuna manyanyaso makubwa ya wafanyakazi mle ndani. Mishahara inatoka kiasi kikubwa lakini wale vibarua na wafanyakazi wanapewa pesa ndogo sana. Nimuombe Waziri husika atembelee Kiwanda cha Dangote - Mtwara kuona manyanyaso yanayofanywa na Wahindi pamoja na Wachina lakini manyanyaso yanayofanywa kwa wananchi wa Mtwara Mjini, Mtwara Vijijini na maeneo ya Kusini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia suala zima la bandari. Katika hoja hii limeelezwa suala zima la kuboresha bandari, lakini Bandari ya Mtwara imetajwa tu kwamba kuna mpango na mkakati wa kujenga magati. Mimi kama Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini nimetembelea Bandari ile ya Mtwara. Pale kuna gati moja limechukuliwa na watu wa gesi wanaitwa BG, lakini ile gati kwa muda mrefu zile meli za BG hazipo. Sasa hivi tumebakiwa na gati mbili tu ambapo tunataka tusafirishe korosho lakini ile gati iko empty na wanasema kwamba pale meli nyingine yoyote hairuhusiwi kutia nanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba katika mpango huu wa kuendeleza bandari wahakikishe Bandari ya Mtwara ambayo ina kina kirefu Afrika Mashariki na Kati, wala haihitaji kutumia gharama kubwa kama ilivyo ujenzi wa Bandari mpya ya Bagamoyo, Wizara husika irekebishe Bandari ya Mtwara na ijenge yale magati manne. Sambamba na hilo ihakikishe inamwezesha yule mwekezaji ambaye ameomba eneo, Mheshimiwa Aliko Dangote kuweza kumaliza mchakato wake ili tuweze kuongeza magati kwa ajili ya Bandari ile ya Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nazungumzie suala zima la miundombinu. Kule Mtwara tuna barabara inaitwa barabara ya Ulinzi, ni miaka mingi barabara hii haizungumziwi kabisa. Naomba Wizara husika ihakishe inashughulikia barabara ya kutoka Mtwara Mjini – Kitaya - Newala na maeneo mengine kwani ni barabara ya Ulinzi ambapo mwaka 1972, mashujaa wetu au wanajeshi wetu walikuwa wanaitumia barabara ile kulinda mipaka ya Tanzania Ukanda huu wa Kusini lakini imesahaulika kabisa. Kwa hiyo, naomba Mpango huu uhakikishe barabara hii ya Ulinzi inajengwa kwa kiwango cha lami, inapita Kitaya - Mahulunga na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine naomba barabara hii ambayo ni kitovu kikubwa cha uchumi wa korosho inayoanzia Mtwara Mjini kuelekea Majimbo yote ya Mkoa wa Mtwara kwa maana ya Mtwara Vijijini, Nanyamba, Newala, Tandahimba hadi Masasi iwekwe kwenye Mpango ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Mimi kabla sijazaliwa naisikia barabara hii inazungumziwa kila siku. Mheshimiwa Nandonde alishawahi kuzungumza kwa miaka mingi sana katika Bunge hili lakini mpaka leo bado barabara hii inasahaulika, kwa hiyo, tunaomba iwekwe kwenye Mpango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala zima la utalii. Pale Mtwara Mikindani kuna magofu ya kihistoria lakini Serikali imeyaacha na haina mkakati wowote wa kuhakikisha kwamba tunatangaza vivutio vile ili viweze kutoa ajira na kuingiza kipato kwa Serikali hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Maeneo yale ya Mikindani kuna vivutio kuliko hata maeneo mengine ya Tanzania, naomba Serikali ianze kuyatangaza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kusema mambo machache. Ilizungumzwa hapa kwamba amani na utulivu ndiyo chachu ya maendeleo katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ndiyo chachu itakayowavutia wawekezaji kuja kuwekeza Tanzania. Kila mmoja ni shahidi, hata Waheshimiwa wazee wetu wa Chama cha Mapinduzi wanafahamu kabisa tarehe 25 Oktoba, 2015 kule Zanzibar chama kilichoshinda ni Chama cha Wananchi - CUF lakini Tume ya Uchaguzi na yule aliyeshindwa hawakutaka kumtangaza aliyeshinda. Kwa hiyo, niombe tu mshindi wa Zanzibar atangazwe ili nchi yetu iendelee kuwa na amani na utulivu na ili wawekezaji waweze kuja kuwekeza Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema kwamba usafirishaji wa reli ni muhimu sana. Kama ilivyokuwa kwenye reli ya kati na kule Kusini pia kuna reli, lakini kwenye Mpango huu sijaona sehemu yoyote iliyoandikwa kwamba reli hii ya kutoka Mtwara – Liganga - Mchuchuma itajengwa lini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la usafiri wa ndege, niungane na wenzangu kusema kwamba ATC ina ndege moja tu tena ni ya kukodi, tuna ubia na wale watu wa South Africa. Naomba ndege ziongezwe kwa sababu ni za Serikali lakini pili gharama yake ni nafuu sana. Nilienda kuulizia tiketi ya ndege kutoka Dar es Salaam kwenda Mtwara...
MWENYEKITI: Ahsante.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru sana. (Makofi)