Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii ya uhai ili na mimi niweze kushiriki katika kuchangia hotuba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi iliyowasilishwa hapa Bungeni leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ardhi ni kila kitu na ardhi ni ishara mojawapo ya uwepo wa dola. Hakuna nchi inayoweza kuwepo duniani isipokuwa na ardhi; na ardhi ndiyo inayotunza maisha ya kila kiumbe kilichopo katika dunia hii. Kwa maana hiyo, ardhi isipoendelezwa vizuri na isipopangwa inavyostahili, hakuna maendeleo. Ardhi inavyopimwa ni kipimo cha ustaarabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ulimwenguni pote ambapo tumetembea na wengine tumeona, wenzetu wamestaarabika baada ya kuwa na matumizi mazuri ya ardhi. Kwa maana hiyo, nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kuja na hotuba nzuri na mikakati mizuri ambayo kwa kweli inatia matumaini kwamba huenda sasa Taifa letu likazaliwa upya na sisi tukawa miongoni mwa watu watakaoweka historia ya kufanya kazi na wewe Mheshimiwa Waziri pamoja na Wataalamu wako ambao kwa kweli mtatuweka katika historia ya kukumbukwa. Kazi yetu sisi ni kuunga mkono hatua mbalimbali ambazo mnazichukua na pale ambapo mtahitaji msaada wa Bunge hili, msisite kuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa sheria na machapisho mbalimbali ambayo ametupa leo. Namuahidi kwamba kwa kweli tutachukua nyaraka hizi kwenda kuzifanyia kazi ili ziwe sasa ni kiongozi kwetu, tusiwe na kisingizo cha kwamba pengine labda ni kutokufahamu kwetu ndiko kumesababisha maeneo yetu mengine yasipangwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ardhi ndiyo kielelezo cha mipango yote ya maendeleo iwe katika kilimo, ufugaji, uwekezaji katika reli, barabara na makazi ya wanadamu. Kwa maana hiyo, uwepo wa harakati mbalimbali katika maisha ya mwanadamu na hasa tunapojikuta kwamba katika Taifa la Tanzania tunaendelea kuongezeka lakini ardhi inabaki pale pale. Kwa maana hiyo ni lazima tuwe sasa waangalifu kwa namna gani tunavyoweza kupanga matumizi endelevu ya hii rasilimali ambayo Mwenyezi Mungu ametujaalia kuwa nayo. Hii peke yake ndiyo rasilimali ambayo kila mmoja anakuwa nayo; masikini kwa tajiri, hata yule aliyekufa naye anahitaji ardhi kwa sababu atatakiwa ahifadhiwe katika nyumba yake ya milele ambayo ni ardhi. (Makofi)
Kwa hiyo, naomba kabisa kwamba mipango yote ambayo imo ndani ya hiki kitabu cha bajeti, ikitekelezwa ipasavyo na nina imani kabisa kwamba tutapiga hatua. Hatutakuwa na migogoro baina ya wafugaji na wakulima, baina ya wananchi na wawekezaji. Kwa maana hiyo niseme kwamba miji yetu itapangwa vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kama ambavyo mara nyingi nimeendelea kusema, kitu ambacho ni cha muhimu kama ardhi, kinatakiwa kuwa na wataalam kuanzia ngazi za kijiji, Maafisa Mipango Miji wawekwe huko. Hata kama ikionekana kwamba labda pengine ajira zao zinaweza zikawa ni nyingi sana, basi angalau wasogee mpaka hata kwenye ngazi ya kata; wawepo wawe wanaratibu na kuweza kutoa taarifa za wepesi na mapema kabisa juu ya maendeleo ya makazi kwenye maeneo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, hata Mabaraza haya ya Ardhi ya Vijiji na Kata wawepo wataalam. Sasa kwa sasa hivi unakuta tu kwamba watu wanawekwa pale kwa sababu mtu amekaa muda mrefu pale au ni mzee maarufu; sasa mzee maarufu na upangaji wa kitu muhimu kama ardhi, naona havihusiani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, natoa ombi na ni rai yangu kwa Wizara hii ambayo kwa kweli tunaitegemea sana, iwe ni chanzo cha ustaarabu katika Taifa letu. Miji mingi inakuwa kwa kasi, lakini ni kwa namna gani ambavyo Serikali na yenyewe imejipanga kwenda na hii kasi ya mabadiliko ya wananchi kuhamia kutoka vijijini na kwenda kwenye centres, Serikali inakuwa nyuma. Kwa hiyo, naomba sasa kwamba Wizara hii ya Ardhi pamoja na Serikali yenyewe itoe kipaumbele cha rasilimali kwa maana ya fedha, utaalamu na vifaa; kwa maana bila kuwapa vitendea kazi watumishi wetu hawa, tatizo hili litaendelea kuwa sugu.
Kwa maana hiyo, niseme tu kwamba ndugu yangu Mheshimiwa Lukuvi na Naibu wake, Mheshimiwa Angeline Mabula, wameonyesha dhahiri kwamba katika awamu hii ya Serikali ya Awamu ya Tano wameanza vizuri na ninaomba tu kwamba mipango yote ambayo mmeileta hapa Bungeni, tunaipa baraka zote mwende mkaitekelezeā€¦.
MWENYEKITI: Ahsante.