Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza nichukue nafasi hii kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Kyerwa ambao wamenichagua kuwa Mbunge wao. Nachowaahidi wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa sitawaangusha.
Nimejipanga vizuri na najua yanayoendelea kule Jimboni lakini mimi ndiye Mbunge wa Jimbo la Kyerwa hakuna mwingine. Hao wanaojipanga wanasema wanasubiri siku mbili, sijui miezi miwili hakuna lolote mimi ndiye Mbunge wa Jimbo la Kyerwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kwanza kupongeza hotuba ya Waziri na niipongeze hotuba ya Mheshimiwa Rais ambapo aligusia maeneo mengi mazuri yanayomlenga Mtanzania halisi. Kwa kweli mimi nasema Mpango huu ni mzuri na nauunga mkono lakini kuna maeneo ambayo nataka nijikite. Maeneo ambayo nataka kujikita, niiombe Serikali, Mpango huu umlenge mwananchi wa kawaida, twende kule chini. Tunaongelea kujenga viwanda lakini tunapoelekea kwenye kujenga viwanda vikubwa tusipoangalia huyu mwananchi wa chini ambaye hali yake ni mbaya hatutaweza kufikia malengo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema tunaenda kwenye uchumi wa kati lazima tuende huku chini, huyu mwananchi ambaye hali yake ni mbaya tunamuinuaje kwanza. Tuna vitu ambavyo lazima tuviangalie, kwa mfano, mimi natoka maeneo ya wakulima. Kule kwetu Mkoa wa Kagera na Jimbo langu la Kyerwa tuna uwezo wa kulima kwa mwaka mpaka mara tatu lakini hawa watu wanapolima hawana pa kuuza mazao, hawana soko la uhakika. Lazima tuwawekee mazingira rafiki wanapolima wapate mahali pa kuuza mazao yao, ndipo tutaweza kumuinua mwananchi na ndipo tutaweza kusema tunaingia kwenye uchumi wa kati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali na Wizara ya Kilimo, kwa mfano kule Kyerwa kuna masoko ya kimataifa yanajengwa pale Mkwenda na Mrongo mpakani na Uganda lakini masoko haya hayaendelei. Tulitegemea masoko haya yangekamilika mwananchi wa hali ya chini angeweza kuuza mazao yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia ni kuhusu miundombinu. Kwa kweli naomba niiambie Serikali ni kama kuna maeneo ya Watanzania na mengine labda siyo Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kule kwetu Kyerwa hakuna hata kilomita moja ya barabara iliyojengwa kwa kiwango cha lami, hali ni mbaya. Barabara inayotoka Murshaka - Nkwenda - Isingilo - Murongo ni mbaya sana haipitiki. Tulipotoka kwenye uchaguzi, nimefanya utafiti magari yote yanayopita kwenye barabara hii yote yamepasuka vioo kila baada ya wiki moja ni kwenda kufanya service, hali ni mbaya.
Naiomba sana Serikali kama wanaweza kutusaidia watusaidie barabara hii inayotoka Murshaka mpaka mpakani na Uganda. Hii ndiyo barabara muhimu na tunayoitegemea. Watu wanaotoka Uganda - Murshaka - Kayanga - Bukoba hii ndiyo barabara tunayotumia. Niombe sana Serikali na niwaombe hao wataalam mnaowatumia, kuna barabara inayotoka Mgakolongo - Kigalama - Bugomola – Uganda, mmesema itajengwa kwa kiwango cha lami, niiulize Serikali ni lini barabara hii itaanza kujengwa? Vilevile barabara hii ya Murshaka - Mulongo itaanza kujengwa lini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema tunataka kwenda kwenye uchumi wa kati lazima tuangalie, wananchi wa Jimbo langu la Kyerwa hawana maji safi na salama, hatufiki hata asilimia 10. Nimuombe Waziri wa Maji na Serikali yangu, najua hii ni Serikali sikivu, wananchi wa Kyerwa tuangaliwe na sisi ni sehemu ya Watanzania, kile kidogo tunachokipata wote tufaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tuna suala la afya, Wilaya yangu ya Kyerwa ni mpya hatuna Hospitali ya Wilaya. Wilaya hii tuna vituo vya afya vinne tu ambavyo havina dawa na hata kwenye zahanati hakuna dawa. Haya mambo ameyazungumzia sana Mheshimiwa Rais, niiombe sana Serikali tunapopeleka dawa ziwafikie wananchi. Naiomba sana Serikali katika hilo itufikirie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda niliongelee ni kuhusu hawa vijana wetu wa bodaboda. Serikali iliweka utaratibu wa kusajili pikipiki baadaye wamesema pikipiki hizi zitabadilishwa namba. Ninyi mwanzoni mmesema mmesajili kwa kutumia namba „T‟ leo mnasema mnataka kutumia namba nyingine, gharama hizi zinabebwa na nani? Leo wananchi wanapigwa, wananyanyaswa wakasajili pikipiki upya lakini makosa haya yalifanywa na nani? Niiombe sana Serikali tunapofanya makosa sisi kama gharama za kusajili pikipiki tukasajili sisi bila kuwabebesha mzigo hawa vijana wa bodaboda, hili siyo sawa. Lazima tuangalie hawa vijana wamejiajiri leo wako mitaani wananyanyaswa, wanapigwa, wanaambiwa sajili mara ya pili hili siyo sawa. Niiombe Serikali iliangalie suala hili na ilitolee ufafanuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ndugu zangu nataka kusema tumemaliza uchaguzi, kila chama kilipeleka Ilani kwa wananchi na chama walichoona ni bora ni Chama cha Mapinduzi. Hakuna chama kingine ambacho kimepewa kuongoza Tanzania ni Chama cha Mapinduzi. Sasa tusije hapa tukaleta mbwembwe, tukaanza kuitukana Serikali sisi ndiyo tunaotawala lazima muwe wapole. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema ndugu zangu hapa kuna maagizo, tunataka tuonekane mbele ya Watanzania kuwa sisi tunajua kupanga, tunajua kuongea lakini Watanzania wana akili. Tumekuwa tukisikiliza hapa Bungeni mkisema vitu mbalimbali, uovu ulio ndani ya Chama cha Mapinduzi ni kweli ulikuwepo lakini Chama cha Mapinduzi kimeamua kufanya mageuzi. Hao mliokuwa mnawataja leo wako kwenu. Sasa hivi ninyi mna ujasiri wa kusimama mbele ya Watanzania kusema mafisadi?
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Huo ujasiri mmeutoa wapi maana mmewabeba ninyi, mliwasema wako kwetu leo wako kwenu. Kwa hiyo, msije hapa kwa mbwembwe Watanzania wana akili, wanajua kinachofanyika na wamepima wameona hamfai.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Habari ndiyo hiyo. (Kicheko/Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niwaambie, hawa Watanzania wana macho wanaona, wana masikio wanasikia.
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umekwisha usiendelee.