Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie Kanuni ya 60(11), kwa idhini yako naomba nizungumze nikiwa nimekaa.
NAIBU SPIKA: Endelea Mheshimiwa.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunifikisha mahali nilipofika, kwa kupitia watumishi wake mbalimbali ambao wamekuwa wakiniombea mchana na usiku.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda niwashukuru sana wazazi wangu Alex na Anitha Mwabusega kwa jinsi ambavyo walinilea kwa mapenzi makubwa na hata kunifikisha mahali nimefika leo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitakuwa ni mpungufu wa fadhila nisipowashukuru mama zangu UWT, Mkoa wa Dar es Salaam, ambao wameniwezesha kufika mahali nimefika leo pamoja na mama zangu UWT taifa. Mungu awabariki sana. (Makofi)
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanza kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa hotuba yake nzuri ambayo aliitoa katika Bunge hili Tukufu tarehe 20 Novemba, 2015. Hotuba hii
ilijitosheleza kila eneo kwa maana iligusa maeneo yote ya Mtanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kumpongeza maana hotuba yake imeanza kutekelezeka haraka sana. Tumeona matunda mengi ambayo yametokana na hotuba hii, tumeona jinsi ambavyo matumizi ya siyo lazima yamepunguzwa, tumeona jinsi ambavyo mapato yameongezeka lakini pia tumeona jinsi ambavyo majipu yameendelea kutumbuliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais na Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa jinsi ambavyo imeweka uwakilishaji kwa kundi la watu wenye ulemavu. Uwakilishaji ni wa jinsi gani? Ni ule uwakilishaji wa kutupatia nafasi kubwa za ngazi ya juu ikiwemo Unaibu Waziri pamoja na Unaibu Katibu Mkuu. Mungu awabariki sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sitaongea mengi, naomba nijikite kwenye ukurasa wa 9 ambapo Mheshimiwa Rais aliongelea makundi maalumu kwa kusema kwamba haki za makundi maalumu zimekuwa zikikiukwa, walemavu, wazee, wanawake na watoto na kadhalika.
Nitajikita kuchangia kwa upande wa watu wenye ulemavu pamoja na wazee.
Mheshimiwa Naibu Spika, kweli kumekuwa na ukiukwaji wa haki za watu wenye ulemavu ikiwemo haki ya kuishi. Tumeshuhudia jinsi ambavyo wenzetu wenye ulemavu wa nguzo wamekuwa wakitendewa vitendo vya ukatili ikiwa ni pamoja na kukatwa viungo vyao na
kuuwawa. Ni juzi tu hapa mwezi Disemba kuna mama mmoja kutoka Tanga alikatwa kidole, ni mtu mwenye u-albinism. Kwa kweli ni vitendo ambavyo havistahili na ni vitendo ambavyo kiukweli vinatakiwa kupigiwa kelele sana. Pia Watanzania ambao muda huu wanatutazama
wavikemee kwa hali na nguvu zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ambacho kimekuwa kikikiukwa kwa upande wa kundi hili ni haki ya ajira. Kuna sheria kabisa ambayo inawataka waajiri wawe na asilimia tatu ya wafanyakazi wao ambao ni watu wenye ulemavu lakini sheria hii imekuwa haitekelezeki.
Niombe Serikali Tukufu ya Chama cha Mapinduzi ifuatilie utekelezaji wa sheria hii kwa kufuatilia kila mwajiri na kuhakikisha wana asilimia hii ambayo imewekwa katika sheria hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo halitekelezeki ni haki ya habari. Kwa upande wa wenzetu ambao ni viziwi wanahitaji kupata habari. Kwa mfano tu wa haraka haraka na mfano halisi hata sisi Wabunge wakati tunaendesha kampeni zetu, ni nani ambaye katika kampeni zake alikuwa akizunguka na mkalimani wa lugha ya alama, hayupo! Mtu huyu unategemea akupigie kura, atapigaje kura na wakati hajajua kitu ambacho umekiongelea katika sera zako? Kwa hiyo, hili pia ni jambo la kuangalia sana. Pia ni endelee kuiomba Serikali
ya Chama changu cha Mapinduzi kutoa agizo kwa wamiliki wa vyombo vya habari ikiwemo television waajiri haraka sana wakalimani wa lugha za alama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu ambacho pia napenda kukiongelea ni haki ya elimu kwa watu wenye ulemavu. Tunashukuru kwamba tuna shule chache lakini hazitoshelezi kwa sababu si wazazi wote ambao wanauelewa wa kuwapeleka watoto katika shule hizi. Kwa hiyo, mimi
niombe Serikali zilezile shule za kawaida iziboreshe kwa kuweka mazingira ambayo yataweza kufikika ama yatakuwa ni rafiki kwa wanafunzi wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niongelee suala la uandaaji wa shughuli za Kitaifa. Katika uandaaji wa shughuli za Kitaifa pia umekuwa hauzingatii mahitaji maalumu. Naomba nitolee mfano mmoja ambao mimi mwenyewe niliguswa. Samahani, ilikuwa ni kipindi kile cha
msiba wa Mheshimiwa Celina Kombani, tulipofika mahali pale hakukuwa na mkalimani wa lugha za alama, ufinyu wa nafasi lakini ule mwili uliwekwa juu inakubidi upande kitu ambacho mimi niliogopa naweza nikasukumwa kidogo nikaanguka wakati nilihitaji kwenda kumuaga yule Mheshimiwa. Kwa hiyo, naomba panapokuwa pana uandaaji wa shughuli za Kitaifa hivi vitu vizingatiwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda niongelee haki za wazee. Tumeona wazee wetu ambao wamestaafu miaka ya nyuma wamekuwa wakilipwa pensheni ndogo sana. Kwa hiyo, niioombe Serikali iangalie ni jinsi gani ambavyo inaweza ikawapandishia pensheni wastaafu
hawa ili waweze kufaidi matunda yao ya utumishi wao katika nchi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha, naunga mkono hoja, ahsante sana.
(Makofi)