Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. MAFTAH A. NACHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nguvu, uzima na afya njema ili niweze kuchangia hotuba ya Waziri wa Nishati na Madini kwa maandishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka Waziri wa Nishati na Madini afahamu kuwa mwaka 2012 Mtwara na viunga vyake kulitokea vuguvugu la gesi na wananchi wakidai haki ya ajira kupitia sekta hii muhimu, lakini kwa makusudi kabisa Serikali ilitumia nguvu kubwa kuwapiga wana Mtwara na hata kuwaua kwa risasi akiwemo mama mjamzito eneo la Mkanaled. Wapo waliovunjwa viungo vya miili yao na wapo waliochomewa nyumba moto na wapo waliopoteza mali na rasilimali ambako kulifanywa na vyombo vya dola.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali baadaye iliunda tume ya kuchunguza athari za vurugu hizo ambayo iliongozwa na Chara Mwijage, lakini cha ajabu mpaka leo hawajaleta mrejesho na wananchi pamoja na askari kadhaa pia wameathirika sana. Je, ni lini Serikali italipa athari hizi kama ilivyoahidi?
Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa kutumia gesi majumbani ambao utaanza Dar es Salaam, Mwanza, Tanga na maeneo mengine, tayari mchakato wake umekamilika maeneo hayo isipokuwa Lindi na Mtwara ambako gesi yenyewe inatoka, wanasema watafanya upembuzi yakinifu. Ni jambo la ajabu sana Bomba la gesi limejengwa kwa miezi 18 tu limekamilika ila kuleta maendeleo Kusini Serikali inaleta kigugumizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri aseme ni tarehe ngapi huo upembuzi umefanyika maana mimi ni Mbunge wa Jimbo sina taarifa yoyote Mtwara? Je, ni lini gesi itasambazwa majumbani Mtwara na Lindi na ni kwa nini Waziri asianze Mtwara na Lindi ambako gesi inatoka na ipo karibu?
Mheshimiwa Naibu Spika, Mtwara mjini kuna mitaa mingi sana kama vile Chipuputa, Kihoro, Komoro, Mbawala Chini, Lwelu, Dimbuzi, Kata ya Mtawanya, Likombe, Mitengo na Naliendele maeneo mengi nguzo za umeme hazijafika.
Mheshimiwa Naibu Spika, umeme unatoka Mtwara mjini ambapo kuna plant ya kufua umeme, Makao Makuu ya TANESCO Mkoa umeme hakuna. Wananchi wanauziwa nguzo kwa pesa nyingi ambayo hawana uwezo kutokana na hali ngumu kiuchumi kwa kuwa fursa za ajira hakuna.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Wizara kwa niaba ya wananchi wa Mtwara, kupeleka nguzo kata zote za Mtwara mjini na wasiwape wananchi mzigo wa kulipia nguzo kwa kuwa wanatakiwa kunufaika na rasilimali ya gesi ikizingatiwa ndiyo waangalizi wa miradi yote ya gesi ambayo ni muhimu kwa Taifa hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia pesa ya kuunganisha umeme hii iliyosemwa imepunguzwa hadi 99,000, bado ni nyingi, wananchi wengi hali zao ni mbaya kiuchumi, hivyo wanashindwa kumudu gharama hizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba gharama hii ya 99,000 iondolewe kwa wananchi wa Mtwara na Lindi kwa kuwa rasilimali hii muhimu inalindwa na wananchi hawa, hivyo ni vyema wakalipa gharama za umeme na siyo kupewa mzigo mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, bomba la gesi liko nje sana, mimi kama Mbunge nimekuwa nawaasa wananchi walinde rasilimali hii muhimu kila siku, hivyo Wizara ihakikishe inafunika Bomba hili na hasa maeneo yaliyoathirika na mvua. Nimeeleza hili kwenye Kamati (TPDC) na leo naiomba Wizara bomba lipo nje sana Mtwara.
Mheshimiwa Naibu Spika, Msimbati inakotoka gesi yenyewe Serikali inashindwa kujenga barabara ya lami ya kutoka mjini. Ni jambo la ajabu sana hakuna kituo cha afya, maana ni kata kwa mujibu wa maeneo ya kiutawala, kwa nini Serikali isijenge kituo cha afya? Jengeni tafadhali.
Sambamba na hilo, Mtwara nzima hakuna hata shule moja au hospitali ambayo imejengwa kwa rasilimali hii inayotoka mkoani humo. Hivi naomba kuuliza, wananchi wa Mtwara wakidai haki hii ni dhambi?
Mheshimiwa Naibu Spika, namsihi sana Waziri katika hotuba yake kueleza asilimia 94 ni maendeleo, basi aiangalie Mtwara kwa namna ya kipekee kabisa ili malalamiko yaweze kwisha na Watanzania wanufaike na rasilimali hii muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mrabaha ni muhimu sana kwa wana Mtwara, mwekezaji wa kiwanda cha Mbolea anaomba gesi kwa kununua Msanga Mkuu apewe ili wana Mtwara wapate ajira, Dangote apewe gesi maana anaagiza makaa ya mawe Afrika Kusini. Pia Wizara ijenge shule ya gesi Mtwara ili kuondoa malalamiko.