Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, naanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuhakikisha nishati ya umeme inapatikana. Nawapongeza Makatibu Wakuu wa Wizara na Wakurugenzi wa taasisi zote zilizopo ndani ya Wizara kwa jinsi wanavyojituma kuhakikisha nchi yetu inaenda vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kutuwekea jiwe la msingi mradi wa Kinyerezi ambao utakapokamilika utakuwa msaada mkubwa kwa wananchi wa Tanzania. Pia nipongeze Serikali kwa kupata fursa ya ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Uganda kwenda Tanga. Ni jambo jema na lenye tija kubwa kwa Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza EWURA kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma mbalimbali. Hata hivyo, kila panapo mazuri hapakosi changamoto zake. Kwa kweli kumekuwa na lawama nyingine ambazo haziwahusu EWURA, lakini kwa kuwa EWURA ndiyo wanaotoa leseni za mafuta basi lawama zote zitawaendea wao na lazima wazipokee, kwa mfano, ukaguzi wa mazingira. NEMC ni tatizo kubwa kwa wafanyabiashara wa mafuta. Gharama ni kubwa sana kwa watu wa mkoani.
Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kukaa pamoja na NEMC kuona utaratibu gani mzuri ambao utaifaa kwa kuwasaidia wafanyabiashara. Nami naweka maslahi yangu wazi kuwa ni mdau wa mafuta.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukaguzi wa mafuta ni jambo jema sana, naipongeza EWURA kwa kuwa makini na kazi yao. Kwa uzoefu wangu wa sekta ya mafuta sijaona wakipokea rushwa na hawana mazungumzo na mtu yeyote. Bado nawashauri, EWURA wamezidi kuwa kama mapolisi wapunguze misimamo, watoe elimu kwa wafanyabiashara, tukielimika tutafuata sheria za nchi na mambo yatakwenda vizuri tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa TPDC nitazungumzia juu ya mauzo ya gas. Tumekuwa tukitumia gesi kama chanzo cha umeme peke yake, ni vyema tukaongeza vyanzo vingine vya umeme kama mkaa wa mawe na maji tupate kuuza gesi yetu nchi za nje. Gesi inatakiwa na nchi nyingi za Afrika Mashariki, tungeweza kuiuza nchi ingepata pesa za kigeni zingesaidia kukuza uchumi wetu. Tumepata bomba la mafuta kutoka Uganda mpaka Tanga, basi bomba hilo lingekwenda sambamba na bomba la gesi.
Mheshimiwa Naibu Spika, REA. Nawapongeza sana kwa kazi nzuri ya kusambaza umeme vijijini. Naomba katika Mkoa wa Dar es Salaam wakamilishe umeme maeneo ya Mianzini, Vikunai, Vijibweni na Kisarawe II.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuweke transformer katika maeneo ambayo umeme mkubwa wa kutoka Kigamboni kwenda Pemba Mnazi umepita juu kwa baadhi ya vijiji na wananchi wanaangalia kwa kuwa hakuna transformer.
Mheshimiwa Naibu Spika, TANESCO. Nawapongeza sana kwa kuwa tatizo la kukatika umeme mara kwa mara limepungua kwa kiasi kikubwa sana. Endeleeni hivyo. Mameneja wa TANESCO Wilaya ya Temeke wanafanya kazi nzuri sana na ni wepesi kujibu pale panapotokea hitilafu za umeme. Nampongeza Mkurugenzi na timu yake yote wanajitahidi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.