Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kuwapongeza viongozi wetu kuanzia kwa Mheshimiwa Rais wetu mpendwa John Pombe Magufuli. Nachukua nafasi hii kumpongeza Waziri Mkuu Mheshimiwa Majaliwa na Baraza zima la Waheshimiwa Mawaziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii pia kuwapongeza viongozi wetu wa Bunge letu kuanzia kwa Mheshimiwa Spika, kwako wewe Mheshimiwa Naibu Spika na Wasaidizi wote wa Bunge. Naendelea kumwomba Mungu aijalie nchi yetu amani, mshikamano na utulivu; kwake yeye yote yawezekana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali ya Awamu ya Nne kwa mpango wake wa Wakala wa Umeme Vijijini. Kwa kweli kazi iliyofanyika ni nzuri sana na inatia moyo. Nachukua nafasi hii kumpongeza sana Profesa Sospeter Muhongo kwa moyo wake wa kujituma kwa nia njema ya kuwa mzalendo na moyo wa kupenda kuifanya nchi yetu kuwa ya umeme hadi 2025.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii pia kuwaombea wafanyakazi wa Wizara ya Nishati na Madini kuanzia Taifa mpaka ngazi ya chini. Mungu awape uzima na maisha marefu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Mbulu katika mpango wa REA Awamu ya Kwanza na ya pili, imebahatika kupata umeme katika Majimbo yote mawili, vijiji 18 kati ya 123. Hivyo naomba sana Wizara hii iwatendee haki wananchi wa Mbulu. Maombi yangu ya kumwomba Mheshimiwa Waziri afanye ziara Wilayani Mbulu kutembelea miradi ya REA Awamu ya Kwanza na pili ili kujiridhisha na hali mbaya ya miradi hiyo hususan Vijiji vya Jaranjar Kata ya Tlawi na Guneneda Kata ya Tlawi na Kata ya Ayamohe.
Mheshimiwa Naibu Spika, barua yangu yenye dodoso la vijiji 33 niliyotuma kwa Mheshimiwa Waziri mwezi Februari, 2016 ifanyiwe kazi kwa kuwa Mbulu tumepunjika sana. Kwa Wilaya ya Mbulu imepata vijiji 18, naomba nijibiwe kwa barua ni lini Mheshimiwa Waziri atafanya ziara Wilayani Mbulu?
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri elimu itolewe na ngazi zote za TANESCO katika maeneo ambayo umeme unatarajiwa kutolewa au kupelekwa kwa wadau/wananchi wa maeneo husika. Wizara itoe elimu kwa wachimbaji wadodo wadogo wa madini ya dhahabu katika Kata za Nahasena, Aehandu ili kuondoa mgogoro katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sheria za kupata mrabaha katika machimbo kati ya HLW na wachimbaji itazamwe. Elimu itolewe kwa watumiaji wadogo wa umeme majumbani kwa kuondolewa kwa VAT na Service Charge ili kuleta hamasa ya matumizi makubwa ya umeme. Pia, watendaji wachache waliopo katika ngazi za Wilaya wadhibitiwe wanaotumia urasimu, ubabaishaji kwa wateja wanaohitaji kuunganishwa na umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, mazingira mazuri ya Tanzania katika kutumia umeme wa gesi yaandaliwe kwa kufanya tafiti za kitaalam ili umeme huu wa gesi uwe na tija kwa uchumi wa nchi yetu. Watazania wahamasishwe kutumia gesi kwa matumizi ya majumbani ili kupunguza matumizi makubwa ya mkaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri EWURA iwe na sekta mbili; moja, isimamie maji na nyingine isimamie mafuta na nishati ili kuleta tija.
Pia, utafiti ufanyike haraka kama Tanzania tumenufaika na asilimia nzuri ya mrahaba katika upatikanaji wa madini nchini. Pia, Sekta ya Mafuta itazamwe upya ili VAT irudishwe katika mafuta kuongeza mapato ya Serikali kwa kuwa mwenye kuhitaji mafuta ana uwezo, kwa hiyo, anastahili kulipa kodi.