Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii adhimu ya kuweza kuchangia katika hotuba hii ya Waziri wa Nishati na Madini.
Ninapenda kuendelea kupongeza juhudi za Serikali katika kuleta maendeleo kwa Taifa hili, pia ninapenda kupongeza jitihada za Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sosthenes Muhongo kwa kazi kubwa anayoifanya. Vijana wa Tanzania tuna imani kubwa sana na Waziri huyu wa Nishati na Madini kwa kazi kubwa anayoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunatambua kazi kubwa iliyofanywa na Wizara hii ya Nishati na Madini katika kuongeza kiwango cha uzalishaji wa nishati ya umeme kutoka kiwango cha megawatts 1226.24 mpaka kufika kiwango cha 1491.69 megawatts ndani ya kipindi kifupi cha mwaka mmoja, kutoka Aprili, 2015 mpaka Aprili, 2016 ambayo ni ongezeko la uzalishaji wa umeme kwa kiwango cha asilimia 19. Sasa kama Wizara hii imeweza kuleta ongezeko la asilimia 19 ndani ya mwaka mmoja tu, basi tuna imani mpaka itakapofika kipindi cha miaka mitano watakuwa wameweza kuongeza uzalishaji wa umeme kwa zaidi ya asilimia 95. Kwa hiyo, ningependa kupongeza jitihada hizi, lakini ningependa Watanzania wote waweze kutambua jitihada zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa pia kupongeza jitihada za Wizara hii za kuongeza kiwango cha usambazaji wa umeme yaani access level kutoka asilimia 36 mpaka asilimia 40. Hili ni ongezeko ambalo limepatikana ndani ya kipindi kifupi tu Machi, 2014 mpaka Machi, 2015. Kwa hiyo, tuna imani kubwa sana na Wizara hii, tuna imani kubwa sana na Waziri Profesa Sosthenes Muhongo, tuna imani ku…
MWENYEKITI: Siyo Sosthenes, ni Sospeter Muhongo!
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna imani kubwa sana na Waziri Sospeter Muhongo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana tunashukuru sana kwa jitihada za Serikali, jitihada za Wizara za kupunguza gharama ya umeme. Kumekuwa na punguzo la umeme kwa asilimia 1.4 mpaka asilimia 2.4 ndani ya kipindi kifupi cha uongozi wa Wizara hii katika mwaka mmoja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru sana kwa Serikali kufuta tozo ya service charge ambayo ilikuwa ni shilingi 5,250; pia tunashukuru sana kwa Serikali kupunguza tozo la kuwasilisha maombi ya kuunganishwa umeme (application fee) ambayo ilikuwa ni shilingi 5,000, tunaiomba sana Serikali iweze kuongeza au kupunguza gharama za umeme katika umeme unaotumiwa katika viwanda, kwa sababu imepunguza umeme kwa wateja wa grade T1 na D1 ambayo ni matumizi ya nyumbani. Sasa tunaomba Serikali iweke pia mkakati wa kupunguza gharama ya nishati hii kwa matumizi ya viwandani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa sana kutoa msisitizo kwamba, nishati ya umeme ni nishati ambayo inategemewa sana katika kukuza uchumi wa Taifa hili, kwa sababu ukizungumzia maendeleo ya viwanda unazungumzia upatikanaji wa nishati ya umeme, lakini ukizungumzia mawasiliano unazungumzia upatikanaji wa nishati ya umeme! Ukizungumzia sekta nyingi za uchumi, hata ukizungumzia kilimo cha kisasa (mechanized agriculture), unazungumzia upatikanaji muhimu wa nishati hii ya umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi sekta nyingi za uchumi katika Taifa hili zinategemea nishati muhimu ya umeme. Ukizungumzia pia ajira kwa vijana utazungumzia nishati ya umeme kwa sababu sekta nyingi za uchumi ambazo ndiyo chanzo cha ajira kwa vijana zinategemea nishati ya umeme. Hivyo, tunaiomba sana Serikali iendelee na juhudi kubwa inazozifanya, vijana wa Kitanzania tunatambua jitihada hizi na tunawaunga mkono na tunawaomba wazidi kuziendeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwetu Kigoma tunatumia umeme unaozalishwa na mitambo maalum na mitambo hiyo inatumia nishati ya mafuta. Kusema kweli inagharimu Serikali fedha nyingi sana, tunatambua Serikali kupitia mradi wake wa Malagarasi unatengeneza mfumo au utaratibu wa upatikanaji wa umeme wa megawatts 44.8 ambao mradi huo utaweza kuzalisha umeme unaotokana na nguvu ya maji (hydro electric power). Kwa hiyo, tunaomba sana mradi huu wa Malagarasi Igamba II uweze kutekelezwa kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua Serikali ina mpango kwamba, mpaka itakapofika 2019 mradi huu utakuwa umekamilika. Kwa hiyo, tunaomba Serikali iweke usimamizi mahiri, ili itakapofika 2019 mradi huu uwe umeweza kukamilika kwa sababu, utawanufaisha vijana wa Kigoma. vijana wa Kigoma wanajishughulisha na biashara, wanajishughulisha na uvuvi, vijana wa Kigoma wanajishughulisha na viwanda vidogo vidogo, pia Kigoma tayari tuko katika utekelezaji wa mpango wa kuanzisha kiwanda cha kuzalisha mafuta kwa kutumia michikichi. Tunafahamu kwamba ili mradi huo na kiwanda hicho kiweze kufanikiwa tunahitaji nishati ya umeme, hivyo tungeomba sana Serikali iweze kutekeleza mpango huu ili uweze kukamilika kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya yote ningependa sana kuiomba Serikali katika mkakati wake wa kuongeza uzalishaji wa nishati ya umeme basi, jitihada hizo ziende sanjari na usambazaji wa umeme huu kwa sababu kama kukiwa kuna uzalishaji lakini usipowafikia watumiaji basi ina maana jitihada hizi zinakuwa hazina tija. Ninaomba sana Serikali iweze kuzingatia haya yote ili Watanzania waweze kunufaika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema machache hayo napenda kuwapa nguvu sana na kusisitiza kwamba Watanzania, vijana na wanawake wa Tanzania tunatambua mchango wa Wizara hii na tuna imani kwamba itatusaidia kwa sababu, katika kipindi kifupi tumeona mambo makubwa ambayo yamefanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.