Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi ya kuchangia katika hoja hii ya Waziri wa Nishati na Madini.
Awali ya yote niungane na Waheshimiwa Wabunge kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo anaifanya yeye pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na viongozi wote wa Wizara kwa juhudi kubwa ambayo wameionyesha kulitumikia Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali yangu kwa kusimamia vizuri Mradi huu wa Umeme Vijijini. Mradi huu ni ukombozi wa wananchi na katika vijiji vile ambavyo umeme umefika wananchi wamepata maana nyingine kabisa ya maisha. Wanafurahia maisha yao, wameanzisha miradi ya uzalishaji, wameanzisha biashara, huduma za elimu na za afya zimeboreka, kwa kila namna mradi huu ndiyo ukombozi wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuongeza bajeti ya wa umeme vijijini mwaka huu kwa asilimia 50. Hii ni hatua kubwa, hatua adhimu na nina imani kwamba Mheshimiwa Waziri akiendelea kusimamia hivi basi ndani ya miaka hii mitano Serikali ya Awamu ya Tano itamudu kufikisha umeme katika vijiji vyote vilivyobaki 10,000 katika nchi yetu na kwa maana hiyo nchi yetu itakuwa katika hali nyingine kabisa ambayo tunasema kwamba tutakuwa tumejipanga kwa ajili ya kufika mwaka 2025 kama nchi inayoelekea uchumi wa kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuombea Waziri na Wizara na Serikali yetu Tukufu ili wamudu kulitekeleza ndani ya miaka mitano kusibaki kijiji ndani ya nchi yetu ambacho hakina umeme. Najua kwamba hilo litaambatana pia na uzalishaji mkubwa zaidi.
Nimuunge mkono Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu ambaye amesisitiza mradi wa Stigler’s Gorge ambao una uwezo mkubwa, tumeuzungumzia kwa muda mrefu, Marehemu Baba wa Taifa aliufikiria katika Awamu ya Kwanza, Awamu ya Pili haikuwezekana pia, ya Tatu, nina imani Awamu hii ya Tano chini ya uongozi wako Waziri mradi huu utawezekana ili ndoto ya kufikisha umeme katika vijiji vyote Tanzania ndani ya miaka mitano hii iwezekane. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika REA Awamu ya Pili Jimbo la Bagamoyo lilipata miradi kumi tu, vijiji kumi ndiyo ambavyo vilipata umeme wa REA lakini kinachonisikitisha au kinachotupa tatizo katika Jimbo la Bagamoyo ni kwamba katika miradi hiyo kumi, minne mpaka hivi sasa haijamalizika na mmoja umefutwa. Sasa miradi minne ambayo ilitegemewa ilipofika Juni mwaka jana 2015 iwe imemalizika mpaka hivi sasa haijamalizika, wananchi wana hasira, hawaelewi, hakuna ambacho wanaweza wakasikiliza kutoka kwa Mbunge, wanashindwa kuelewa kwamba wao wanaishi katika nchi gani kama siyo hii hii nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kijiji cha Buma nguzo zimesimamishwa lakini nyaya hazijafungwa. Kwa hivyo kunguru nao wanatembea pale wanafanya ndiyo viotea wanakaa kule, wananiuliza Mbunge, sasa hawa kunguru tutawafanya nini, tuwafuge majumbani kwetu au iweje? Katika kijiji cha Kondo hivi karibuni nguzo zimeenda.
Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana kwa sauti yako ya wiki iliyopita ambayo imefanya kijiji cha Kondo sasa hivi mkandarasi yule ndiyo anajitahidi ameweka juhudi kubwa ya kuweza kufikiza umeme. Lakini kabla ya hapo kila tulilolisema lilikuwa haliwezekani. Kijiji cha Kondo na mradi wenyewe haujaanza mpaka hivi sasa. REA wamejichanganya kwamba Kondo kuna bandari ambayo haijengwi Kondo, bandari inajengwa Pande na inajengwa Mlingotini. kijiji ambacho kimefutwa kwa ajili ya mradi wa bandari ni kijiji cha Pande na wao siyo kwa utashi wao isipokuwa ni mradi wa Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kijiji cha Kondo Mheshimiwa Waziri naomba utumie juhudi yako yote kuweza kuhakikisha kwamba mkandarasi huyu anaanza kufanyaazi mapema iwezekanavyo. Kijiji cha nne ni Matimbwa ambacho sehemu ya umeme imekamilika lakini kuna nguzo 20 ambazo bado hazijafungwa nyanya. Nguzo hizi bahati mbaya ni eneo hilo ndilo ambalo tuna zahanati mpya ya kijiji cha Matimbo. Wenzetu NGO ya Korea imejitolea kutujengea zahanati nzuri ya kisasa katika kijiji kile cha Matimbwa, wanatushangaa kwamba nguzo ziko pale zimesimama, sehemu nyingine umeme unawaka lakini pale hapawaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba REA ihakikishe kwamba mkandarasi huyu anamsimamiwa vizuri ili kijiji hiki nacho cha Matimbwa mradi wake ukamilike. Pande imefutwa sawa kwa sababu mnatengemea kujenga bandari pale, lakini mradi huu ulishakabidhiwa kwa mkandarasi, imani yangu ni kwamba basi mradi huu ungehamishiwa katika kijiji kingine. Nimezungumza REA bado hatujapata mafanikio, nina imani kwamba kwa juhudi zako Mheshimiwa Waziri bila shaka REA watapata maelekezo ya kuweza kusaidia kuhamisha mradi ule kuupeleka katika kijiji kingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimwa Waziri naomba atakaposimama kufanya majumuisho basi ututhibitishie wana Bagamoyo kwamba miradi hii michache itapewa kipaumbele kuweza kumalizwa ndani ya mwaka huu wa 2016. Ni miradi michache tumeipata basi nayo iweze kukamilishwa wananchi waweze kupata huduma hii adhimu ya umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile hatukufaidika kiasi hicho katika REA Awamu ya Pili, mategemeo yangu sasa baada ya mimi kama Mheshimiwa Mbunge pamoja na Madiwani kuwasilisha REA miradi 29 katika Jimbo hili la Bagamoyo kwa ajili ya REA III, nina imani kwamba safari hii tutaonewa huruma na miradi hii yote 29 ambayo tumeiwasilisha itaweza kuingizwa katika utekelezaji katika Awamu hii ya Tatu ya Umeme Vijijini. Mheshimwa Waziri najua kwamba kwenye REA II kulikuwa na tofauti kubwa sana kati ya Majimbo na Majimbo, Wilaya na Wilaya, bila shaka Wilaya zile ambazo hazikuweza kufaidika sana katika REA II basi safari hii utaziangalia kwa jicho la huruma ili nazo ziweze kupiga hatua nzuri zaidi na kuweza kuwakaribia Wilaya zingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwa na umeme vijijini ni jambo moja, lakini umeme wa uhakika nalo ni jambo muhimu sana. Katika Mji wa Bagamoyo na Kata za jirani kama vile Magomeni na Kiromo kumekuzuka tabia kubwa sana ya ukatikaji wa umeme mara kwa mara. Hukai siku mbili umeme umekatika mara kidogo umeme umekatika. Mheshimiwa Waziri nadhani jambo hili linafanya wananchi nao wanakosa faida zile ambazo walikuwa wakizitegemea wazipate kutokana na uwepo wa umeme, naomba Mheshimiwa Waziri Shirika la TANESCO waliangalie jambo hili kwa umakini, kama ni vipuri, kama ni mitambo ambayo imechakaa iwe transfoma au viunganishi vingine, mitambo hii iweze kushughulikiwa kwa umakini, ukarabati na ukarafati uwe mila na desturi ya Shirika letu la TANESCO ili wananchi waweze kupata huduma bora katika upatikanaji huo wa umeme usiwe unakatika mara kwa mara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie jambo moja la mwisho na hili ni kuhusu nishati ya gesi. Katika Wilaya yetu ya Bagamoyo watafiti wameendelea kufanya kazi kutafuta gesi, wakitarajia kupata gesi katika Jimbo langu Bagamoyo, Kata ya Fukayosi wamefanya kazi sana pale na katika Jimbo la Chalinze Kata ya Vigwaza wamefanya kazi sana pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepewa fununu kwamba kuna gesi lakini hatujapata taarifa rasmi naomba…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana.