Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza katika hotuba ya bajeti iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu, katika Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitangulie kutoa taarifa za masikitiko makubwa. Katika Jimbo letu la Kilwa Kaskazini, siku nne zilizopita tulipatwa na maafa makubwa ya mafuriko kutokana na mvua kubwa za El-Nino zinazoendelea kunyesha katika Milima ya Matumbi zilizosababisha kupoteza maisha ya watoto wetu wawili waliokuwa wakisoma darasa la sita katika Kijiji cha Chumo. Tulimpoteza kijana wetu mdogo anaitwa Hawa Haji Kekarange, lakini pia tulimpoteza Abdul Aziz Kapanda. Mwenyezi Mungu aziweke roho zao marehemu hawa mahali pema peponi. Amina. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza kuchangia bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu moja kwa moja leo nitajikita katika upande wa sekta ya barabara ambayo imeathiriwa kwa kiasi kikubwa na uwepo wa mvua za El-Nino hapa nchini. Changamoto ni kubwa na tusipozifanyia kazi katika kipindi hiki, basi hata ile asilimia 5.4 ya ukuaji wa uchumi inaweza isifikiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa barabara hii ya Tingi - Kipatimu. barabara ile ambayo ipo katika Jimbo langu la Kilwa Kaskazini imeathirika sana. Barabara ile tangu tarehe 9 Desemba, 2023 ilipata changamoto kubwa za kutopitika. Vilevile, sababu siyo tu mvua za El-Nino bali pia kumekuwepo na malori yenye uzito mkubwa usiolingana na uwezo wa barabara, madaraja na makalavati yaliyopo kule ambao umesababisha madaraja yabomoke kabla hata ya mvua na mafuriko ya juzi na matokeo yake upitikaji wa barabara umekuwa mgumu. Tuzingatie kwamba yale malori yamekuwa yakifanya kazi kubwa ya kupeleka malighafi za ujenzi wa bandari ya uvuvi kule Kilwa Masoko (Mradi mkubwa wa kimkakati ambao Serikali yetu imewekeza kwa kiasi kikubwa). (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuzorota kwa barabara ile kumesababisha hata ule Mradi wa Kilwa Masoko wa Ujenzi wa Bandari ya Uvuvi nao umezorota kwa sababu hayapeleki ile malighafi ya mawe ya ujenzi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kutokana na El-Nino mambo ndiyo yamekuwa magumu zaidi, juzi tu yalipotokea yale mafuriko maeneo manne ya tuta la barabara yaliyo jirani kabisa na madaraja pamoja na makalavati yamekatika na sasa barabara ile haipitiki kabisa kwa asilimia mia moja pamoja na umuhimu wake huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kwamba barabara ile inakwenda kwenye kumbukumbu za Maji Maji ambazo zitatuongezea ufanisi katika utalii ambazo umepata GN hivi majuzi. Kwa hiyo, naiomba Serikali iiangalie ile barabara kwa jicho la pekee na kwa kuwa barabara ile ina milima mirefu ambayo inatiririsha maji kila siku. Kwanza Serikali ichukue hatua ya kurekebisha miundombinu ya barabara ile ili sehemu kubwa ya barabara ipite juu ya milima badala ya kupita bondeni. Kwa mfano, mafuriko yaliyotokea juzi yametokea katika Bonde la Chumo ambalo lina urefu wa zaidi ya kilometa tano na barabara imepita humo humo kwenye bonde. Kwa hiyo, nafikiri kwamba sasa wataalam wetu wabuni utaratibu ambao barabara hii isipite sehemu ya mabonde pale ambapo hakuna ulazima wa kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya pili ambayo napenda kuishauri Serikali ni kwamba, barabara ile katika maeneo yenye miinuko mikali, tutengeneze barabara za zege ili ziwe na uhakika wa kupitika muda wote wa mwaka. Pia wawepo wenzetu wa TARURA na TANROADS waweze kuhudumia ipasavyo kupitia bajeti ambayo tutaipitisha hapa keshokutwa na pia hata zile fedha za dharura zinazopelekwa kwa ajili ya barabara zetu za TANROADS na TARURA, nyingi zimekwenda katika maeneo ambayo siyo ya kipaumbele. Kwa mfano, kuna barabara ya kijijini kutoka Kipatimu kwenda Kibata makalavati na madaraja yalivunjika tangu tarehe 9 Desemba, mvua kubwa za El-Nino zilipokuwa zimepamba moto, mpaka wakati huu ile barabara ambayo ilipewa first priority na wenzetu wa TARURA haijashughulikiwa. Badala yake milioni 200 zilizoletwa kwa ajili ya dharura zimepelekwa kwenye barabara ambayo ni priority namba sita kwa mujibu wa ushauri wa wataalam wetu. Naomba priorities za wataalam zizingatiwe ili kule ambako kuna changamoto kubwa, basi solution iweze kupatikana mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nina ushauri wa kitaifa, janga la El-Nino limetokea nchi nzima na maafa yamekuwa makubwa. Kwa hiyo, tunahitaji uwekezaji mkubwa kwenye barabara zetu zote hapa nchini, kwamba bajeti ya Wizara yetu ya Ujenzi iweze kuongezwa hadi kufikia asilimia 30 ya bajeti nzima ya Serikali Kuu ili asilimia 60 za zabuni ziweze kutangazwa mapema mara tunapokuwa tumepitisha bajeti zinazohusika na barabara. Keshokutwa tukipitisha kuanzia TARURA basi wapewe ruhusa ya kuweza kutangaza zabuni. Pia TANROADS wapewe ruhusa angalau asilimia 60 itangazwe mara moja tutakapopitisha bajeti ili mwaka wa fedha unapoanza na kazi ya marekebisho makubwa ya barabara ambazo zimeathirika kwa kiasi kikubwa na mvua za El-Nino ianze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la nne ambalo ningependa kushauri ni kwamba, fedha za dharura pia zitengwe, tusisubiri mpaka dharura itokee. Hata kama zitakaa Makao Makuu ya TANROADS au Wizarani siyo mbaya ili dharura itakapotokea mara moja kazi ya kurekebisha miundombinu iliyoathirika iweze kwenda kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, vitengo vinavyohusika na technical audit kule TANROADS na kule TARURA pia viimarishwe kwa kupewa fedha za kutosha kwa ajili ya kumudu kufanya kazi zao. Kuongezewa vile vile watumishi au wataalam wa kutosha ili waweze kushughulika na changamoto zote zinazoendelea na waweze kupewa vitendea kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina hakika changamoto ambayo ilionekana Mkoani Lindi na Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi ya kukuta mtaalam wa falsafa anasimamia barabara na maeneo mengine inasemekana wapo wataalam wa minyororo baridi na wataalam wa saikolojia ambao wanasimamia barabara. Hili tatizo lingeweza kuonwa na technical auditors kama kitengo hiki kingefanya kazi zake sawasawa na marekebisho yangefanyika mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitengo hiki pia kipewe jukumu la kufanya utafiti wa barabara zetu zote, madaraja yetu yote, makalavati yetu yote ili kuhakikisha kwamba kabla athari kubwa hazijajitokeza, ziweze kushughulikiwa mapema. Kwa sababu miundombinu mingi ya barabara imeanza kujengwa tangu mwanzoni mwa mwaka 2000, kwa hiyo, lifespan ya hizi barabara, madaraja na makalavati sehemu kubwa zimekwishapitwa na wakati. Hata hivyo, kwa kuwatumia wataalam wetu hawa wa technical audit wanaweza wakatuwekea mambo sawasawa na tukaweza kufanya preventive maintenance na hatimaye hizi barabara zikapitika kwa kiwango kinachostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa licha ya Waziri na Naibu Waziri kuwa wanatutembelea katika maeneo mengi hata kama Barabara yangu ya Tingi – Kipatimu Mheshimiwa Waziri hajaweza kufika, basi ajitahidi afike kila maeneo. kwa sababu Mawaziri hawana uwezo wa kufika kila eneo wawatume Maafisa Waandamizi waje wakague hizo barabara ili waone uhalisia. Unaweza ukakuta unapokea taarifa mezani, mwisho wa siku hali sivyo ilivyo huko ambako barabara zinajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja namba saba ambayo ningependa kuishauri Serikali ni ujenzi wa mifereji pembezoni mwa barabara. Barabara zetu nyingi hasa zile za vumbi na hata zile za lami baadhi hazina mifereji. Unakuta barabara imejengwa tu mifereji ya kupitisha maji hakuna, mvua zikinyesha zinapita katikati ya barabara na kuharibu barabara vibaya sana. Kama mvua za El-Nino zilivyo mwaka huu, barabara zimegeuka kuwa mito na hatimaye zimekuwa na madhara kama haya ambayo nimeyasema. Kwa hiyo, naomba tuone namna ya kufanya ili ujenzi uweze kuimarishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia utafiti wa barabara zetu na namna ya ...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ndulane, muda wako umekwisha.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)