Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru wewe kwa kuniona na kunipa nafasi hii niweze kuchangia Hotuba ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa msomi, Mheshimiwa Muhongo ambaye kwa kweli, binafsi yangu kwa aliyonifanyia kipande cha Chalinze, sina shaka kusema Mungu azidi kumzidishia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika awamu iliyopita katika vijiji 67 vya Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze tumefanikiwa kupata umeme karibu vijiji vyote kupitia mpango wa REA isipokuwa vijiji 15 ambavyo vimebakia, ambavyo nina imani kabisa Mheshimiwa Waziri atakapokuja kusimama hapa na kueleza juu ya mkakati wake wa kuimarisha umeme vijijijini, basi Chalinze nina hakika kabisa ataviangalia hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanaoishi vijiji vya mbali kama kule Kwa Ruombo, Kibindu, Lugoba, Mkange, wanaonisikiliza wote katika Jimbo la Chalinze kule Pela, Msoga, Tonga na maeneo mengine mbalimbali hakika kabisa watakuwa wameyasikia haya. Kwa kweli Profesa najua kwamba, ramani ya eneo lile siyo mgeni nalo, basi atafanya mambo yale ambayo ametufanyia katika miaka mitano iliyopita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hilo, jambo la msingi nataka nimkumbushe Waziri na najua kwamba analifahamu, lakini sio mbaya nikatumia nafasi hii kumkumbusha. Pale Chalinze wakati wanaweka transformer, ile inaitwa power transformer, kwa ajili ya kuongeza nguvu za uzalishaji wa umeme Chalinze na maeneo yake walitufungia transformer yenye MVA 45.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu na takwimu za wasomi wa elimu ya umeme katika Jimbo letu la Chalinze wakiongozwa na ndugu yangu Mkuu wa TANESCO pale Chalinze inaonesha kwamba, matumizi ya sasa ya Jimbo la Chalinze ni almost karibu MVA 10, kwa hiyo, maana yake tunayo nafasi nyingine iliyobakia ya MVA 35 ambayo Mheshimiwa Profesa Muhongo akiiangalia vizuri hii anachotakiwa kufanya ni kuweka tu nyaya pale na wananchi wa Chalinze wale wapate umeme wa uhakika zaidi; hatuna tunalomdai zaidi ya umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo nataka nizungumzie pia tatizo kubwa ambalo nililizungumza katika Bunge lililopita juu ya tatizo lililoibuka katika Kijiji cha Kinzagu na Makombe juu ya hati alizopewa mwekezaji. Sisi tulilalamika sana, lakini tukaambiwa kwamba, kuna utaratibu Wizara inaweza ikatoa hati ya mtu kwenda kufanya uchimbaji wa madini katika vijiji hata kama hao wataalam wa Wizara hawajafika kijijini hapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikwambie ukweli na Bunge lako lisikie na Watanzania waamini hili ninalolisema. Hati iliyotolewa, aliyopewa mwekezaji katika Kijiji cha Kinzagu na Makombe imeacha kipande ambacho nafikiri kina ukubwa, labda wa jumba hili la Bunge! Kijiji chote kipo ndani ya ardhi ya mwekezaji! Wale watu wamezaliwa pale, wameishi pale, wamekulia pale na waliokufa wamezikwa pale! Leo hii wanapowaambia kijiji kizima kiondoke, nini maana ya mimi kuwa Mbunge pale kama sio kutetea watu wangu ambao wamenipigia kura. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie Profesa Muhongo, hata kama sheria hizo zipo nataka atambue kwamba, sheria hizo kwa watu wa Chalinze ni bad law na kwamba, tutazipigania kuhakikisha kwamba hizo sheria zinaondolewa, lakini muhimu yeye mwenyewe atakapokuja kufanya majumuisho, akatuambia ni mpango gani walionao katika hili. Kidogo nimepata nafasi ya kusoma sheria, natambua kwamba, hata kama mtu amepewa hati hiyo wanakijiji wanayo haki ya kukataa huyo mtu asipewe access ya kufanya uchimbaji wake na mwendelezo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwingine hapa tunazungumzia maendeleo, ninachokiona Serikali yangu inajaribu kunigombanisha nao pia, kwa sababu, mimi kama mwakilishi wa wananchi sitokubali! Nasema tena, sitokubali kuona watu wangu wa Kijiji cha Kinzagu na Makombe wanaondolewa ili kupisha bepari ambaye anataka kuja kuwekeza katika eneo lile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo nizungumzie pia, matatizo ambayo wanayo wananchi wa eneo la Kata ya Mandela. Niliwahi kusema hapa na leo narudia tena, tulimwomba Mheshimiwa Waziri aangalie sana kuna Kijiji kinaitwa Ondogo ni kijiji ambacho wanaishi watu wanaotegemea maisha yao katika ukulima. Kama unavyojua ukulima sio shughuli ambayo inafanyika muda wote, ni shughuli ambayo inafanyika, jua likizama watu wanarudi nyumbani.
Pale nataka nikuhakikishie Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Rais aliyemfanya yeye leo hii akawa Waziri alichaguliwa kwa asilimia 100 katika Kijiji cha Ondogo; Bwana John Pombe Magufuli alichaguliwa kwa nini, ni baada ya mimi na viongozi wenzangu wa chama, kwenda pale kuchapa maneno na kuwahakikishia wananchi wale kile kilio chao cha transformer tu ya KV 20 itapatikana na wale wananchi watapata umeme wa uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe taarifa Mheshimiwa Waziri kwamba, hapa nilipo nimeshapewa taarifa kwamba, kama hiyo transformer haitakuja pale, 2020 nikatafute sehemu nyingine za kuombea kura kwa sababu, pale sitopata hata moja. Kwa maana hiyo ya kwamba, sitopata hata moja, maana yake Mheshimiwa Rais pia naye hatopata hata moja! Mimi natokea Chama cha Mapinduzi, naomba ku-declare interest kukipigania chama changu ni wajibu wangu na nina imani katika jambo hilo. Nataka pia Mheshimiwa Waziri aangalie sana pale ambapo tulipata asilimia mia moja ya kura zote ili baadaye tusije kupata sifuri ya kura zote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Muhongo kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, lakini pia kwa juhudi kubwa ambazo Wizara yake inafanya. Tunao mradi pale, mkubwa, wa Bwala la Kidunda ambao katika bwawa hilo pia, tunatarajia kwamba, ipo sehemu ambayo itatoa umeme na umeme huo utafaidisha Vijiji vya Magindu, Kijiji cha Chalinze, kwa maana ya Bwilingu, lakini pia na maeneo mengine ya Mikoroshini na Kata ya Pera pia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachomwomba Mheshimiwa Waziri, yeye na Wizara ya Maji wanapokwenda kusimamia, kuhakikisha kwamba jambo hili wanalifanyia kazi, basi ningeomba jambo la umeme kwa wananchi wangu wa Chalinze nao pia muwaangalie kupitia mlango huo, kama ambavyo mipango thabiti ya Chama cha Mapinduzi tumeipanga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Naomba kumpongeza tena Mheshimiwa Waziri na kumtakia kila la heri katika safari yake ya kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Ahsante.