Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kwanza jioni hii ya leo kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Nishati na Madini. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, bado ananiwezesha kusimama kwenye Bunge lako Tukufu, nikitoa mchango wangu katika Wizara mbalimbali; ni kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu aliyenifanya nisimame hapa niwawakilishe Wanaliwale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema ukweli, sina wasiwasi na dhamira ya Waziri wa Nishati na Madini. Kwanza nakubaliana naye kwa taaluma yake, masuala ya uweledi na ufanisi hilo sina ujuzi nalo, lakini kwa taaluma yake namfahamu vizuri. Wasiwasi wangu ni kwenye utekelezaji, na uwezo wa kuyatekeleza haya ambayo yameanishwa kwenye hotuba hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuweka rekodi sawa nataka niwaeleze Waheshimiwa Wabunge walioko humu ndani, wasione Wabunge wa Kusini wamekuwa walalamikaji sana humu ndani, kwamba kila Mbunge wa Kusini akisimama analalamika kama vile tumeonewa! Kwa kuweka rekodi sawasawa nataka niwafahamishe Waheshimiwa Wabunge, Reli ya Tanga – Dar- es-Salaam iling‟olewa kutoka Mtwara– Nachingwea, wakati ule Mkoa wa Lindi tulikuwa tunalima pamba, mkonge, karanga pamoja na korosho. Wajerumani wakatuwekea ile reli, ili kuharakisha maendeleo, lakini tulivyopata uhuru reli ile ikang‟olewa, ndipo umaskini wa watu wa kusini ulianzia pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunapokuja kulalamika tumeona Mwenyezi Mungu ametupa neema hii ya gesi, sasa ni lazima watu ambao tumeshafanyiwa huko nyuma tuwe waoga. Ndio maana mtu wa Kusini akisimama leo hapa, haiamini hii Serikali ya Chama cha Mpinduzi kwa sababu, wameshatufanyia mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijielekeze kwenye madini. Sera ya Madini bado sijaielewa, hata wananchi wangu wa Liwale nafikiri bado hawajaielewa Sera hii imekaakaaje, hasa pale ambapo ardhi ya wanakijiji inapokuja kugundulika pana madini; hawa wananchi wa ardhi ile bado hawaelewi hatima yao na nafasi yao katika rasilimali ile iliyopatikana pale kwenye ardhi yao. Kwa sababu, ninavyofahamu mnufaika wa kwanza wa rasilimali inayopatikana ni lazima awe yule inayomzunguka pale alipo. Pamoja na kwamba, hizo rasilimali ni za kitaifa, lakini mnufaika wa kwanza anapaswa awe yule inayomzunguka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii kwa Liwale imekuwa ni kinyume chake, sisi Liwale tuna machimbo ya madini yako kwenye Kata ya Lilombe, katika Kijiji cha Kitowelo. Pale wanachimba madini ya sapphire na dhahabu, lakini Ofisi ya Madini iko Tunduru, ndiko mahali ambako kinapatikana kibali cha uchimbaji. Aidha, wachimbaji wadogo ili kupata leseni inabidi uende Tunduru, sasa unafikaje huko Tunduru, sielewi!
Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu ukishapata hicho kibali, unakwenda moja kwa moja msituni, machimbo, wanachimba, wakishachimba wanakwenda moja kwa moja Tunduru kwenye mauzo; Halmashauri ya Kijiji na Wilaya haina habari! Nilivyofika kule kwenye machimbo nikalazimika kumtuhumu hata Mkurugenzi wa Halmashauri, pengine naye anajua chochote. Haiwezekani madini yatoke pale Lilombe, wana Lilombe hawajui, Halmashauri haijui, haipati hata thumni! Sasa leo nimesikia ofisi hii imesogezwa imepelekwa Nachingwea!
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoka Lilombe mpaka Liwale Mjini ni kilometa 60, kwa hiyo, hayo yanayofanyika Lilombe Halmashauri haijui! Sasa hii Sera ya Madini, Mheshimiwa Waziri, atakapokuja nitaomba ufafanuzi kidogo, hii inakuwaje kuwaje? Hawa wachimbaji wadogo tunawasaidiaje? Kwa sababu, nimekwenda mimi kwenye yale machimbo nimemkuta mmiliki mmoja, mchimbaji mdogo, kuna bwana mmoja pale, nafikiri yule alikuwa IGP, Mheshimiwa Mahita! Yeye ana vitalu vyake pale, lakini yeye mwenyewe hayupo pale yupo Tunduru!
Mheshimiwa Mwenyekiti, ina maana wale wachimbaji wakipata madini wanampigia simu, anakuja kuchukua anakwenda au pengine wampelekea ananunua anakwenda, lakini Halmashauri pale haipati chochote, wala kijiji kile hawapati chochote, wanaachiwa mashimo tu na ile ardhi ipo pale! Sasa hapo Waziri atakapokuja naomba anisaidie, hii Sera ya Madini ikoje kwa sababu, sisi ndiyo kwanza tunaingia kwenye hiyo fani kwa sababu, mgodi wetu ule ni mdogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nirejee kwenye umeme. Wilaya ya Liwale ilibahatika kupata umeme miaka ya 77, ndiyo Wilaya ya kwanza kwenye Kanda za Kusini na Nyanda za Juu Kusini kupata umeme wakati ule Mzee Kawawa akaambiwa umeme amefunga kwenye mikorosho, lakini umeme wenyewe ni ule wa mwisho saa nne, mpaka leo miaka 40 bado umeme ni ule ule wa mafuta!
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi hapa wametuonea huruma wakachukua ile mashine kutoka Ikwiriri wakaipeleka Liwale, mashine kuukuu iliyotoka Ikwiriri wakaipeleka Liwale ku-subsdise ile mashine ya zamani ya Mzee Kawawa; lakini kulingana na jiografia ya Liwale, umeme ule wa mafuta, masika kama saa hizi Liwale hakufikiki na mafuta hakuna! Kwa hiyo, mafuta yanapokosekana Liwale inabaki giza, lakini siyo hivyo tu, kutoka Liwale kuja Nachingwea ni kilomita 120. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna hii Miradi ya REA; umeme wa REA katika Wilaya ya Liwale, ambayo ina vijiji 76 sisi tuna vijiji vitano tu! Tuna Mangirikiti, Kipule, Likolimbora, Mihumo na Darajani, hivi vipo ndani ya kilomita tano kutoka Liwale Mjini, lakini nje ya hivyo zaidi ya hapo hakuna kingine tena kinachopata umeme. Siyo hivyo tu, umeme huu wa gesi umeishia Nachingwea! Nachingwea Liwale kilomita 120, lakini mpaka leo sijaelewa huu mradi wa umeme wa kutoka Nachingwea kufika Liwale umefikia hatua gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetembea kutoka Liwale kuja Nachingwea katika Vijiji vya Kiangara, Vibutuka, Nagano mpaka Mikunya; nguzo zimewekwa pale, zingine zimechimbiwa, zingine huku zinaanguka huku zinachimbiwa, haieleweki, haielezeki, ukimuuliza meneja hakuna anachosema! Mara pesa bado, hajaleta mkandarasi, hapo alipofikia bado hajalipwa, sijui imekuwa kuwaje, haieleweki ile REA pale Liwale mwisho wake ni lini? Hivi sisi tutabaki gizani mpaka lini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nataka niseme, kama ingekuwa enzi zile za zamani kwamba, ukitoa shilingi inaleta reflection yoyote, ningekuwa natoa shilingi kila Wizara hapa, maana sioni Wizara hata moja ambayo nikasema Wizara hii ina nafuu kwa Liwale. Hata hivyo, hata nikitoa shilingi haina maana yoyote kwa sababu, tumeona hapa mambo yenyewe yanavyokwenda mwisho wa yote tunapiga kura wape, wape, basi; haina maana yoyote!
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, namwomba Mheshimiwa Waziri, kweli atutendee haki, atuondoe gizani; sisi umaskini wetu umechangiwa na haya mambo ya barabara na haya mambo ya umeme, huu ndio unatuletea umaskini, leo hii Liwale hakufikiki, huu umeme wa mafuta magari hayaendi! Hivi huu umeme wa mafuta utafika lini? Halafu umeme wenyewe mwisho saa nne!
MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, muda wetu ndiyo huo!