Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Stephen Julius Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. STEPHEN J. MASELE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii ya Wizara ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri ambayo anafanya ya kujenga nidhamu ya nchi yetu na kurejesha nidhamu ya Utumishi wa Umma na nidhamu ya wananchi kutii sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia kumpongeza sana Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuteuliwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nimpongeze Waziri wa Nishati na Madini, Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo kwa kazi nzuri ambayo anaifanya ya kusukuma mbele Sekta ya Nishati na Madini nchini.
Mheshimiwa Spika, wote sisi ni mashahidi, Wizara hii ina changamoto nyingi sana kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamezieleza, lakini wizara hii haihitaji malaika wa kwenda kufanya kazi pale. Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo ameonesha ubora na anastahili kupewa support, anastahili kuungwa mkono na Waheshimiwa Wabunge na tutakuwa tumelitendea haki Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimefanya kazi na Mheshimiwa Muhongo, namwelewa, tunapozungumzia moja ya Mawaziri makini nchi hii ni mmojawapo. Waswahili wanasema mnyonge mnyongeni haki yake mpeni. Leo Mheshimiwa Rais ameeleza wazi anataka Tanzania iwe nchi ya viwanda, Mheshimiwa Rais ameeleza wazi, anataka asilimia 30 ya ajira za vijana zitokane na viwanda. Sasa Wizara hii na Hotuba ya Mheshimiwa Muhongo ndiyo ambayo itatupeleka kwenye kuwa na Tanzania ya viwanda.
Mheshimiwa Spika, leo Waziri wa Viwanda na Biashara hata aseme ataleta viwanda elfu ngapi, kama hakuna nishati ya umeme ni sawa na kazi bure na Waziri ameonyesha kwa vitendo kwa kutenga asilimia 94 ya bajeti yake kwenye maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na niseme tu kwamba kwenye REA kila mtu anafahamu kazi inayofanywa ni nzuri, lakini changamoto zipo, najua ataendelea kuzitatua. Nimpongeze pia kwa kuteremsha gharama za umeme, Watanzania wengi wanalia gharama za umeme ziko juu na nakumbuka aliahidi kwamba atalifanyia kazi atapunguza gharama za umeme leo ametekeleza.
Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, kwenye viwanda nchini moja ya changamoto kubwa ambayo wanahangaika nayo ni bill zisizoeleweka ambazo wanapelekewa na TANESCO kwenye maeneo husika. Ziko charge nyingi ambazo viwanda vinapelekewa ambazo zinakatisha tamaa uwekezaji wa viwanda vilivyopo na hata hivyo vinavyokuja. Nina hakika kama bili hizi zitaendelea kuwa hivyo, basi kutakuwa na changamoto kubwa ya bidhaa zinazozalishwa nchini kushindana na bidhaa za masoko za kutoka nchi za jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri aliahidi kwa Watanzania kwamba atafanya mahesabu na atahakikisha hata nguzo za umeme itafika mahali atatutangazia atazigawa bure, tunasubiri ahadi hiyo na nina uhakika anaweza.
Mheshimiwa Spika, leo Tanzania, Mheshimiwa ameeleza kwenye hotuba yake, inazalisha megawati 1,400. Ili tuweze kuwa nchi kweli ya kipato cha kati, ili tuweze kuwa Taifa la Viwanda ni lazima tuongeze speed ya uzalishaji wa umeme. Speed ya uzalishaji wa umeme ni kuwekeza kwenye miradi ya uzalishaji hasa kupitia gesi asilia. Leo Tanzania tunazalisha gesi yetu wenyewe na Mungu ametusaidia, tusingekuwa na hii gesi na tusingekuwa na uimara wa Mheshimiwa Profesa Muhongo kusimamia bomba la gesi likamilike kwa kutegemea mvua haya malengo yote tusingeweza kuyafikia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie, Taifa la Uturuki leo linaongoza kwa uzalishaji wa bidhaa mbalimbali kwenye soko la Ulaya, ni kwa sababu wana umeme wa kutosha na hata hiyo gesi yenyewe hawana, wanaagiza kutoka kwenye Mataifa yenye gesi. Uturuki peke yake inazalisha megawatt 60,000 za umeme. Afrika Kusini inazalisha megawati 80,000 za umeme. Unapokwenda kule kama Waziri unamwambia mwekezaji kama Toyota njoo uwekeze kiwanda cha ku-assemble magari Tanzania atakuomba megawati 5,000 peke yake, huna, safari yako haina maana.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Bunge hili litatenda haki kwa Watanzania endapo tutafikiri kimkakati namna gani Tanzania itazalisha umeme wa kutosha ili kuweza kukidhi mahitaji ya majumbani lakini pia tuweze kukidhi maendeleo ya viwanda tunayoyazungumza.
Mheshimiwa Spika, umeme tulionao huu vikiunganishwa migodi mitano tu Tanzania tutaingia kwenye mgao. Leo iko migodi hapa inazalisha yenyewe umeme. Tukiunganisha viwanda vikubwa tutaingia kwenye mgao. Kwa hiyo, bado tuna kazi ya kufanya, bado tuna kazi ya kumpa ushirikiano Waziri kwa jitihada ambazo amezionyesha kwenye bajeti hii ili tuweze kufikia hayo malengo tunayoyataka. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa leo Tanzania tunazalisha kupitia TANESCO, malengo yetu kama nilivyosikia kwenye hotuba tunatakiwa tuwe na megawatt 2,500, tunatakiwa tuwe na megawatt 10,000 ifikapo 2025. Tutafikishaje megawatt 10,000 kama hatuvutii uwekezaji binafsi kuja kuwekeza katika Sekta ya Umeme? Serikali peke yake kuzalisha megawatt 100 za umeme ni zaidi ya Dola za Marekani milioni mia moja na! Tukitaka megawatt 10,000 leo tunahitaji zaidi ya dola bilioni 10 za Marekani labda ni bajeti yetu hii ya miaka 10 ijayo tusifanye jambo lingine lolote. Kwa hiyo, lazima Serikali tuwe na mikakati ya kuhakikisha kwamba tunawekeza katika umeme sawa, lakini tuvutie pia sekta binafsi kuwekeza katika miradi hii.
Mheshimiwa Spika, nizungumzie kwenye Sekta ya Madini, zipo jitihada kubwa Wizara inafanya, niwapongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuendeleza jitihada za kuwainua wachimbaji wadogo Tanzania, nimpongeze Naibu Waziri kwa kazi kubwa ya kusuluhisha migogoro ya Nyamongo, lakini bado ziko changamoto ambazo tunatakiwa kuzishughulikia na bado katika uwekezaji mkubwa pia tunahitaji kuwa na migodi mipya.
Mheshimiwa Spika, tulipitisha miaka miwili iliyopita hapa sheria inayotoza kodi kwenye vifaa vya utafiti. Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri ni mjiolojia bingwa duniani, tunapoweka sheria hizi za fedha za kutoza kodi kwenye vifaa vya utafiti ni sawasawa unasema tunataka kilimo cha kisasa halafu tunakwenda kuweka kodi kwenye matrekta, tunakwenda kuweka kodi kwenye mbegu.
Mheshimiwa Spika, kwenye uzalishaji wa migodi mipya haiwezi kutokea migodi mipya Tanzania endapo utafiti utakufa, endapo makampuni yanayofanya utafiti yatapunguza bajeti ya kufanya utafiti. Mheshimiwa Waziri naomba hili alifanyie kazi tupitie upya hizi sheria hasa kwenye eneo hili la utafiti ili kuweka unafuu wa utafiti na hatimaye nchi yetu iweze kupata viwanda vipya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuiwezesha Tanzania kupata mradi mkubwa wa kujenga bomba la mafuta kutoka Uganda. Nafahamu jitihada zako, nafahamu jitihada za Serikali. Miradi hii itasaidia sana kukuza uchumi wa Taifa letu. Nimwombe aendelee na jitihada, natambua Uganda imetuomba Tanzania tupeleke bomba la gesi, natambua Kenya tume-sign makubaliano nao ya kuwauzia megawatt 1,000. Leo wapo Watanzania wanajiuliza kwa nini shilingi haina nguvu? Wachumi wanasema unapoingiza zaidi kuliko kupeleka nje zaidi maana yake unadhoofisha shilingi yetu. Tukiweza kuuza megawatt 1,000 za umeme Kenya tutaingiza mapato ya kigeni mengi ambayo yatasaidia hata kuimarisha shilingi yetu.
Mheshimiwa Spika, miaka mingi tangu uhuru tumetegemea mazao ya mashambani; pamba, tumbaku, madini kidogo bei imeshuka, uzalishaji umeshuka; lakini tuna bidhaa, tuna zao jipya la gesi ambayo tunaweza tukazalisha megawati 1,000 ambazo Kenya wanazihitaji na tuka- export megawatt 1,000 tukapata mapato mengi ya kigeni. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.