Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Mohammed Said Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Konde

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. MOHAMMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenifanya leo hapa nikasimama mbele ya Bunge lako Tukufu na kuweza kupata nafasi hii ya kuchangia. Pia, nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika wasilisho letu hili la Wizara ya Elimu pamoja na Mihezo na Sanaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na elimu na nitachangia sehemu zote mbili. Mchango wangu, lolote lile nitakalolizungumza litaelekea kwenye bajeti ndogo lakini pia hata hiyo ndogo kutokufikia kwa wakati na wakati mwingine hata kutokufikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Elimu pamoja na Michezo. Katika kuhudumu katika Kamati hii, nilikuwa kwenye Wizara nyingi. Nilianzia kwenye Nishati na Madini kule mambo ni safi, Wizara ya Biashara, Kilimo na Mifugo, kule bajeti zao zinakwenda vizuri. Huku kwenye Elimu, huku kwenye Michezo, kwa kweli hali ni mbaya. Kama Mheshimiwa Spika, alitaka nije kuangalia Wizara ambazo zinapokea fedha hizi na kuweza kuzifanyia kazi, basi huku kwa kweli fedha haiendi na hiyo inayokwenda ni ndogo mno. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuangalia hapa, naanzia kwa upande wa elimu ya watu wenye mahitaji maalum. Nimeona hapa sisi tunajikaza kupeleka mahitaji ya wanafunzi wote, mashuleni kote, vyuoni kote lakini kuna kundi muhimu la watu wenye mahitaji maalum, hili tumelisahau. Kundi hili ni muhimu sana kwa sababu tunataka twende nao kwa pamoja. Sasa jambo la kusikitisha, mambo yaliyoko huko kwa watu wenye mahitaji maalum, unaweza kulia wakati unapokea mawasilisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapungufu yaliyopo kwa upande wa vifaa vya kufundishia, vitabu hakuna walimu wanalalamika. Jana nilikuwa naangalia TBC hapa nikamuona mwalimu ambaye anafundisha watu wenye mahitaji maalum na yeye mwenyewe akiwa anahitaji hayo mahitaji maalum, analalamika kupata yale material ya kufundishia. Zile karatasi ambazo zinafaa kwa nukta nundu kufundishia, vitabu hamna, nikashangaa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati hii nikaona hii nayo ni point. Wanalalamika hawa hawana vitabu, hawana printer, hawapati yale mafunzo ya kitaalamu. Kwa hiyo, wao kama alikuja na utalaamu wake ndiyo wamebakia hivyo. Mimi natoa hayo lakini lengo langu Wizara iongezewe bajeti ili vitu hivi vipatikane. Kwa sababu tukiuliza Wizara wanasema bajeti ni ndogo na hiyo hiyo ndogo yenyewe bado haijafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa wanafunzi, kwanza hawa walimu, walimu hawa wenye mahitaji maalum naamini wana kazi kubwa. Tumchukulie mtu ambaye anafundisha mtu ambaye hasikii, hivi ni sawa na mtu ambaye anamfundisha anayesikia? Ana kazi kubwa huyu kubwa lazima tumhurumie leo tunauliza hapa, hana posho lakini ana mshahara sawa na yule anayefundisha mtu wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu fikirini kama unamfundisha mtu mwenye mahitaji maalumu, mtu asiyesikia, mtu asiyeona, kazi yake ikoje?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa namna anavyochangia lakini nilitaka nirekebishe kidogo maneno; haitwi mtu asiyesikia, anaitwa Kiziwi, mtu asiyesikia kwa tafsiri ya Kiswahili ni mtukutu au mjeuri.

Vilevile unaposema mtu mzima na huyu kwa tafsiri mtu mzima ana umri wa miaka 18 kwenda juu lakini kuna mtu aliyehai na aliyekufa, sasa, tafsiri hapa usiseme mtu mzima na huyu siyo, ni mtu asiye na ulemavu na huyu ni mtu mwenye ulemavu. Nashukuru. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mohammed Issa, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. MOHAMMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru mtoa taarifa kwa kunielimisha, sijabobea kwenye hizi lugha ambazo ni za kuficha ukakasi. Lengo langu ni kupeleka ujumbe, sasa nimepokea taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili hilo Serikali ilitakiwa ilizingatie kwa sababu hawa wanafundisha watu ambao wana mahitaji maalum. Kwa hiyo, ni lazima wawe na ziada kazi yao ni kubwa na ni tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini upande wa wale wanafunzi, mimi nilitamani wawe na vile vitu ambavyo vinasaidia. Tumeuliza hapa wheelchair tu hawana, zile fimbo za kutembelea hawana. Watafikaje shuleni? Pia, hawana wasaidizi wa kuwafikisha pale. Inachukua wiki haji shuleni, wiki anakuja, anasomaje huyu? Kwa nini hatuwapi nafasi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza bajeti yao hawa, walimu wapandishiwe mishahara ama posho lakini wale wanafunzi wapewe hivi vitu vya kusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa upande wa Wizara ya Michezo. Mimi nilibahatika kufika kule Ivory coast, lengo kubwa ni kwenda kuangalia miundombinu ili kuja kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuko nyuma kwa asilimia karibu 80, wenzetu wamewekeza kwenye miundombinu hii. Sisi tunajiandaa kufanya hii AFCON 2027 lakini naona bado hatuko serious. Hatuko serious kabisa kwa sababu mpaka sasa hivi tunacho kiwanja kimoja tu ambacho tunakikarabati. Lakini viwanja viwili ambavyo tayari kule bajeti imetengwa havijaanza mpaka leo mwaka wa fedha unakwisha, sijui tuko serious kiasi gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nishauri juu ya yale ambayo nimeyaona kule. Wenzetu kule kwanza katika maandalizi yale wamejenga Kijiji cha Michezo ili kuepuka gharama za timu zile kuziweka kwenye mahoteli pamoja na Maafisa wale. Kwa hiyo kuna kijiji cha michezo maalum ambacho baada ya kumaliza michezo hii kitafanyiwa shughuli nyingine; pengine ni nyumba zitauzwa kwa watu binafsi ama kwa mashirika. Napendekeza ipatikane bajeti maalum kwa ajili ya kufanya miundombinu itumike kwa ajili ya kufanya mashindano yetu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala hili la mapato, huu Mfuko wa Maendeleo ya Michezo tumekwenda kutenga five percent kwenye sport betting wakati hilo ilikuwa tupate sehemu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba dakika moja nimalizie kwa sababu ni muhimu sana. Hii hata Mheshimiwa Rais anakuwa na ukakasi wa kutoa fedha huku kwa sababu fedha hizi zinakwenda kwenye miundombinu ya Serikali. Sheria zetu hazionyeshi kwamba tunapata vipi mapato, BMT hawa wanapata huku lakini ukija kwenye TFF hawapati. Kwa hiyo sheria hizi zote zingaliwe upya. TFF wachangie kule, michezo ile ya kukimbia wachangie kule na kila sehemu ili Mheshimiwa Rais awe na nguvu ya kutupa fedha. Tunamuona Mheshimiwa Rais ana nia ya dhati, ametoa bilioni 31 kwa kukarabati Uwanja wa Taifa na ninaamini atatoa nyingi zaidi ya hizo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, ahsante. (Makofi)