Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai. Kipekee, nampongeza sana na kumshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo ameendelea kuifanya kwenye Majimbo yetu yote. Ukiacha Elimu na Afya na maeneo mengine ya Miundombinu, tumeshuhudia upelekaji wa magari ya ufuatiliaji pamoja na Ambulance kwa siku za hivi karibuni. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nampongeza na kumshukuru sana Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Mchengerwa, tangia ameanza kuhudumu kwenye Wizara hii pamoja na wasaidizi wake, Waheshimiwa Manaibu Mawaziri, pamoja na Makatibu wote, Katibu Mkuu na Manaibu Makatibu Wakuu, wameendelea kuwa na kiwango cha 5G. Endeleeni kupiga kazi, mimi kama Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI, naendelea kuunga mkono kazi hii njema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kupitia Wizara ya TAMISEMI, kwa kuendelea kufanyia kazi Maazimio na Ushauri wa Kamati kuboresha Elimu Mtandao. Kwa sasa, Serikali inafanya majaribio ya kutoa elimu kwa njia ya mtandao. Tumeshuhudia kama Kamati, Mwalimu mmoja wa Kemia au Biology anafundisha kwenye shule tatu kwa wakati mmoja, yeye yuko Kibaha lakini darasa lingine liko Dodoma, na liko eneo lingine. Kwa hiyo, hii ni hatua nzuri na naendelea kuipongeza Serikali kwa kazi hii kubwa ya kuendelea kufanyia kazi maoni ya Kamati pamoja na ya Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, malengo ya kuanzishwa kwa Shirika la Kibaha, yalikuwa ni pamoja na kufanya Tafiti kwenye maeneo mbalimbali yakiwemo Elimu. Kazi hii kubwa na nzuri ambayo nimeipongeza hapa, ya kuendelea kuboresha Elimu Mtandao, imefanywa na Shirika letu la Kibaha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Elimu Kibaha ndiyo wamefanya kazi hii kubwa na nzuri. Kwa masikitiko, ni kwamba hili Shirika la Elimu Kibaha, tayari imeshatangazwa kuvunjwa. Mapendekezo na Ushauri wa Kamati kwa msimu uliopita, ilikuwa ni kuitaka Serikali iboreshe Shirika la Elimu Kibaha na siyo kuvunjwa. Kwa sababu bado malengo ya kuazishwa kwake yapo na tunayahitaji kama Watanzania. Tunakumbuka kuna Hospitali pale ya Tumbi, ilifanya kazi kubwa na nzuri kuanzia kipindi cha Mwalimu Nyerere, bado kazi ile ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Hospitali ile imerudi kuwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa na jambo hili kwa kweli kama Mjumbe wa Kamati, naona si sawasawa. Bado naiomba Serikali kupitia upya maamuzi yake hayo ya kuvunja Shirika la Elimu Kibaha ambalo kwa sasa tunaona ipo haja na iko sababu ya kuendelea kuliacha Shirika hili liendelee kufanya Tafiti za Elimu na maeneo mbalimbali kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Amandus, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Godwin Kunambi.

TAARIFA

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza mchangiaji kuhusiana na Shirika la Elimu Kibaha. Mimi ni mdau pale, nimewahi kupita pale Kibaha Folk Development College (Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Kibaha), kwa kweli Shirika la Elimu Kibaha ni muhimu sana na linatoa watu wengi. Mfano mzuri mimi Mheshimiwa Kunambi niko hapa, ni zao la Folk Development College pale Kibaha. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Amandus, Taarifa hiyo unaipokea?

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea Taarifa hii nzuri na inayoleta sasa kumbukumbu nzuri ya kazi njema ya Shirika la Elimu Kibaha. Bado naendelea kumuomba Mheshimiwa Mwenyekiti wakati wa kuhitimisha Hoja yake, aone namna atakavyoliweka vizuri ili tuitengeneze kama Azimio la Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najielekeza kwenye TARURA, sisi Waheshimiwa Wabunge tunaotokea vijijini, hali yetu kwa kweli ni mbaya. Kuna wakati unalazimika kutokufika Jimboni kwa kutumia gari maana yake lazima uvuke kwenye madaraja yaliyovunjika kwa kutumia namna nyingine ya usafiri kufika ndani ya jimbo lako. Taarifa iliyotolewa hapa, tumeona na tumesikia, Waheshimiwa Wabunge wote kwa ujumla wetu namna bajeti ilivyopelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuunga mkono Taarifa hii ya Kamati, Serikali iendelee kupeleka fedha kwa wakati. Hali ni ngumu na hasahasa karibu tunajiandaa kurudi kwenye Majimbo yetu, wanachi wanatamani kupata majibu kwa Waheshimiwa Wabunge, nini tumesikia kutoka kwa Serikali. Wakipeleka fedha kwa wakati, itaweza kutusaidia zaidi na mambo mengine na shughuli za kimaendeleo zitaendelea kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu la Nachingwea, siyo Barabara tu za TARURA, hata TANROADS. Ukitoka Ndanda, huwezi kufika Nachingwea barabara imekatika, ukitoka Masasi, huwezi kufika Nachingwea barabara imekatika, kwa hiyo, achilia mbali Barabara za TARURA. Sisi watu wa Nachingwea hatuna mbadala, jana nimepata taarifa basi linaishia Masasi, kutoka hapo wananchi wanavushwa kwenda upande wa pili kwa hiyo hii haileti picha nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwa Mheshimiwa Kuchauka kule Liwale, hali ni mbaya nayo, ukienda huko Mbarali hali ni hivyohivyo. Kwa hiyo niombe sana Serikali, jambo hili ni jambo la dharura na ni lazima tuchukue hatua sasa. Haina mbadala, Wananchi wa Tanzania wanahitaji huduma kila kona. (Makofi)

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Amandus, Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Lazaro Nyamoga.

TAARIFA

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza mchangiaji, wakati anaendelea kutaja, nilitaka tu kumtarifu kwamba, hata Kilolo kwenyewe, barabara hazipitiki kabisa maeneo yote na madaraja yamevunjika. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Amandus, Taarifa ya jirani yako unaipokea?

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kadhia hii, kwenye changamoto hii, hata ukienda Kiteto huko, hali ni hiyohiyo. Tunasema kwa uchungu na tunaiomba Serikali kuchukua hatua sasa, hali yetu siyo nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, najielekeza kwenye eneo lingine la maboma hasa ya Zahanati na Vituo vya Afya. Wananchi waliitikia wito na kuendelea kuhamasika kujenga majengo ya Zahanati wenyewe kwa nguvu zao lakini na Vituo vya Afya, majengo haya yako mengine yamekaa kwa zaidi ya miaka minne, miaka mitano, miaka miwili na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, hapa nguvu za wananchi zimekwenda, niombe Serikali kuweka Mpango Mahususi, Mpango wa haraka ambao unakwenda kufanya kazi ya kumalizia maboma haya kwa wakati. Zile ni nguvu za wananchi ambazo zimekwenda. Tukifanya hivi maana yake tunawavunja moyo wananchi wetu, hawawezi tena kufanya shughuli zingine, basi tuone nguvu hizi ambazo tayari wameshaziweka kwa kujenga haya majengo…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono Hoja za Kamati zote mbili. Nakushukuru sana. (Makofi)