Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona na kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Awali ya yote na mimi niunge mkono maazimio yote yaliyowasilishwa hapa na Wenyeviti kwani ni maazimio yaliyolenga kuiboresha na kuisimamia Serikali yetu vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishie hapo alipoishia dada yangu Mheshimiwa Salome Makamba, kipengele hiki cha TARURA. Kwanza niwape pole ma-engineer wetu nchi nzima. Wataalamu wetu hawa wako tayari kufanya kazi na wanaipenda kazi yao vizuri sana; na namna unavyoona mnavyoongozana nao mnapokagua matatizo unaona nyuso zao zinavyoumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shida ni kubwa sana kwenye maeneo yetu. Shida hii si mvua tu hizi, yapo maeneo yana mvua karibu msimu mzima wa mwaka. Kwa hiyo maeneo haya yana uharibifu kwa muda mrefu, na ma-engineer wetu hawa mara kadhaa wanaandika maandiko kupeleka TARURA makao makuu ili wapate fedha kunusuru hali iliyopo kwenye maeneo yetu huku lakini kwa bahati mbaya sana fedha hizo hazitoki, na kama zinatoka zinatoka kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii inatupa wakati mgumu sana sisi Wabunge kwa sababu ni ukweli kabisa tunakaa hapa ndani, tunapitisha bajeti na tunapata ahadi nzuri nzuri lakini utekelezaji unakuwa haupo kabisa. Jambo hili si zuri kwa sababu baada ya vikao hivi sisi Wabunge tunaenda kuwaambia wananchi kule ni nini kinakuja kutekelezwa. Hatimaye bajeti ya mwaka inaisha hali ya barabara zetu inabaki vile vile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niombe maazimio haya ya Bunge sisi kama Wabunge tunapaswa tuyasimamie kweli kweli pasipo kuoneana aibu, pasipo kuona nani ataniona mimi nasema nini. Lazima tuisimamie Serikali yetu kwa sababu ni Serikali yetu hii. Hakuna mtu mwingine atakayekuja kuisimamia na kuisemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niseme kama walivyosema wenzangu, suala la TARURA kupata fedha lisiwe suala la kusema kwamba sasa ni shukrani, Hapana, ni wajibu wa Serikali. Taasisi hii tumeiunda wenyewe kwa sababu tunataka itusaidie, tuipe fedha ifanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee mfano kwenye Jimbo langu la Mbinga Vijijini. Jimbo hili lina mvua nyingi sana, Jimbo hili lina madaraja mengi sana. Nishukuru kwa awamu hii kidogo barabara zinapitika kwa sababu madaraja yamejengwa. Lakini uko ukanda mmoja bado barabara hazipitiki, mvua ikinyesha tu ujue simu kwako. Mbunge huku kuna shida hii, Mbunge hatupiti. Sasa unashindwa kuelewa hii hali itaenda hadi lini? Ifike sehemu, taasisi yetu hii ni kubwa sana, tuipe fedha. Najua uwezo wa kutekeleza na kutatua matatizo yetu wanayo. Kwa hiyo niombe sana fedha tunazotenga hapa Serikali izipeleke kama zilivyopitishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine ambayo nataka kuiongelea ni namna tunavyotatua migogoro. Nchi yetu imepangwa vizuri sana; tunaanza kwa mwenyekiti wa kijiji, tunakwenda kata, tunakwenda wilaya, tunaenda mkoa na mpaka huko Wizarani. Maeneo haya yote yalivyotengwa maana yake yana uwezo wa kutatua migogoro. Hata hivyo inashangaza sana, hii migogoro mingine ni ya kawaida sana, lakini wenzetu waliopo kwenye maeneo haya kama walivyoaminiwa hawatatui migogoro hii. Wanasubiri mpaka mtu mwingine atoke huko juu anakuja kutatua ule mgogoro ambao sasa unasababisha mpaka matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mgogoro kwangu kule, maarufu unaitwa “ndika.” Nimeuzungumza hapa mara nyingi sana, ni mgogoro wa ardhi. Mgogoro huu chanzo chake ilikuwa panda miti kibiashara. Pale tuna Mkuu wa Wilaya amehangaika sana kuutatua huu mgogoro sana, ukaja haujaisha. Umefika ngazi ya mkoa haujaisha. Lakini cha kushukuru hivi karibuni Mwenyekiti wetu wa Chama aliingia kati tukaenda mimi, yeye Mwenyekiti, Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya tukaumaliza huu mgogoro. Tukaumaliza kwa kusema wananchi warudishiwe maeneo yao wawe tayari kupanda miti hiyo ya kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni wako viongozi wamerudi, wananchi wale wamejipanga kupanda miti kibiashara, viongozi wale wanaenda wanapiga danadana tena ule mgogoro uanze upya. Sasa wewe kiongozi uko hapa umewekwa kufanya nini? Umewekwa ili uendelee kusumbua hao wananchi? Kwa nini usimalize huu mgogoro ambao Mwenyekiti wa Chama wa Mkoa amesema uishe na tumekubaliana wananchi warudishiwe maeneo yao; kwa nini sasa leo hii wewe pekeyako unasumbua wananchi unaleta danadana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo halikubaliki, halikubaliki kabisa. Viongozi hawa waliopewa dhamana na Serikali ni wajibu wao kumaliza migogoro kwenye maeneo yao. Wasimsubiri Katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi aende akamalize migogoro kule, wao wana nafasi zao pale. Wamepewa dhamana na Serikali hii, wamepewa dhamana na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia kumaliza ile migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili jambo kwangu linanisikitisha sana. Ilifika mahali hawa wananchi wako zaidi ya 400 wanasema tunataka kurudisha kadi, tunataka kurudisha kadi za CCM kwa sababu Chama hiki hakitusikilizi. Sasa tumeenda tumewasikiliza, yuko kiongozi mmoja analeta danadana anasema hapana, wasirudishiwe maeneo yao wapewe maeneo mengine. Sasa kwa nini yuko pale? Kwa nini aseme hivi? Kwa nini hakusema wakati tuko pamoja pale? Amesubiri watu tumewaaminisha wananchi kwamba maeneo yenu mnapewa halafu sisi tunaondoka yeye anageuza Kiswahili kule, anamuongopea nani? Nani anayemuongopea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili halikubaliki na ninalisema leo hapa tukirudi huko lazima tutagombana sana, lazima tutagombana kwa sababu hatutaki kuwa waswahili kiasi hicho. Mgogoro umeonekana wananchi wamechukuliwa maeneo yao si maeneo ya mtu mwingine yaani shamba langu mimi amepewa mtu mwingine. Sasa kwa nini unapata kigugumizi kunirudishia shamba langu? Kwa hiyo hawa viongozi kwa sababu wamepangwa kiutaratibu watimize wajibu wao, wasisubiri watu kuja kuwafanyia kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka nilizungumzie hapa ni suala la ujenzi wa vituo vya afya. Nashukuru sana Serikali hii ya Awamu ya Sita kwa sababu kwa upande wa jimbo langu mimi mpaka tunaingia awamu ya sita hatukuwa na kituo cha afya, lakini leo hii nashukuru sana, sana, sana, tuna vituo vya afya tulivyovikamilisha vitano. Viko vituo vya afya vile vya tozo viwili lakini tuna vituo vingine tumejenga kupitia mapato ya ndani vitatu tayari tumevikamilisha lakini uhitaji bado ni mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhitaji ni mkubwa kwa sababu Jimbo lile limetawanyika sana lina kata kubwa 29; kwa hiyo kwa vituo vya afya ni vichache sana. Nishukuru kwa mpango wa Mheshimiwa Rais kwa ahadi ile aliyotupa kwamba kila jimbo litapewa kituo cha afya kimoja. Lakini hapa nataka tu kutoa tahadhari kidogo kwamba yako majimbo yana ukubwa tofauti tofauti. Yako majimbo madogo pengine vituo vilivyopo sasa hivi vimeshatosheleza. Hii kauli ya ujumla ya kwamba kila jimbo linaenda kupewa kituo kimoja kimoja pengine tungeitazama kwa jicho jingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana kabisa tunaweza kurundika sasa vituo vya afya kijiji kwa kijiji kwenye hayo majimbo mengine. Kwa hiyo ningeomba hapa, na ninapendekeza, wazo kama hilo kwenye majimbo yale makubwa makubwa basi tupeleke hata vituo vya afya viwili badala ya kituo cha afya kimoja. Vivyo hivyo hata pamoja na zile shule za SEQUIP yako majimbo sasa hivi wala hawana shida ya shule hizo tayari wameshajitosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ushauri wangu katika maeneo kama hayo; kwa mfano kwa jimbo langu mimi tayari kuna kata tatu hazina shule za sekondari. Wananchi hawa wanakwenda kilometa nyingi sana kupata elimu. Kwa hiyo pengine maeneo kama haya najua kwa namna ilivyo yako majimbo yanayofanana na jimbo langu mimi…

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kapinga, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa; Mheshimiwa Jackson Kiswaga, taarifa.

TAARIFA

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, Mheshimiwa Kapinga ni rafiki yangu naomba nimshauri akazane kuomba kwenye jimbo lake asitaje majimbo ya wengine na sisi tuna mahitaji yetu. Akazane kuomba vituo vingi kwake aache na sisi wengine tuendelee na ya kwetu, ni taarifa tu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kapinga, taarifa unaipokea? Malizia mchango wako.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi kuipokea taarifa kwa sababu hafanyi utafiti yule. Hafanyi utafiti kwa sababu nilivyomwambia yako majimbo makubwa makubwa. Jimbo lake ni dogo kweli kweli sasa unaipeleka tena shule pale inaenda kufanya nini? (Makofi)

MWENYEKITI: Malizia mchango wako.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo jimbo langu mimi ni kubwa ndiyo maana nimesema hapa sasa hivi nakosa shule tatu, yeye kwake zote zimetimia. Kwa hiyo Jimbo kama la Kalenga zile shule zinazopaswa kupelekwa kule zirudi kwenye jimbo la mimi. (Makofi/ Vicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ombi langu lilikuwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia, muda wako umeisha.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu lilikuwa hasa kwenye upande huu wa vituo vya afya na shule tuangalie ukubwa wa maeneo halafu tuvigawe hivyo vituo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)