Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi, nami niweze kutoa mchango wangu katika Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Kwa mwaka wa fedha 2024/2025 Pamoja na Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka huo 2024/2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya kwa Taifa letu pamoja na maono makubwa ikiwemo pia Mapendekezo haya ya Mpango wa Maendeleo kwa Mwaka wa Fedha unaokuja wa 2024/2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Mheshimiwa Profesa Kitila, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na uwekezaji pamoja na Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa taarifa nzuri ambazo wamewasilisha ndani ya Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, nimpongeze Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, Mheshimiwa Kigua pamoja na Wajumbe wa Kamati, kwa kazi kubwa waliyoifanya wakati wa uchambuzi wa Taarifa hizi ambazo leo zinawasilishwa mbele ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia maeneo machache. Jambo la kwanza ni ukusanyaji wa mapato. Tathmini ya ukuaji wa mapato ya ndani kwa maana ya vyanzo vyetu vya ndani kwa miaka mitano 2017/2018 hadi 2022/2023 inaonesha kwamba, mapato ya kodi yamekua kwa asilimia 10.5. mapato yasiyo ya kodi yalikua kwa asilimia 2.5. mapayo ya halmashauri yalikua kwa asilimia 14.9.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini makisio ya ukuaji wa jumla ya mapato yetu ya ndani kwa vyanzo vyote kwenye mpango unaopendekezwa wa 2024/2025 unatarajiwa kuwa ni asilimia 10.5. Hili linawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020/2025 Kifungu cha 18_B(3) Chama kinaielekeza Serikali. Naomba ninukuu; 18_B(1). “Kupunguza utegemezi wa kibajeti kwa kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato ya ndani ikiwemo kuibua vyanzo vipya vya mapato, kuongeza idadi ya walipa kodi, kuboresha mazingira ya uwekezaji na ufanyaji biashara na kukusanya maduhuli yote kwa kuitumia mifumo ya kielektroniki.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kufiklia malengo haya ya ukuaji wa mapato ya ndani kwa wastani wa asilimia 10.5 kwa Mwaka wa fedha 2024/2025, lakini ili mapato ya kodi yaweze kuchangia ile asilimia 12.4 kwenye mapato ya taifa kama ilivyowasilishwa kwenye mapendekezo. Vile vile, ili Pato la Taifa liweze kukua kwa asilimia 5.8 kama ambavyo imependekezwa kwenye Mpango. Pia, bajeti inayotarajiwa ya trilioni 47.4 kati ya hizo trilioni 34.4 Ikiwa ni mapato ya ndani kwa zaidi ya asilimia 70. Yako mambo ya msingi ambayo kama Taifa lazima tuyafanye: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuimarisha mifumo yote ya ukusanyaji mapato hapa nchini. Tuna mifumo mingi. Kwa mfano, Mfumo wa Kodi za Ndani ambao ni Integrated Domestic Revenue Administration System (IDRAS). Mfumo wa TRANCIS wa ushuru wa forodha. Tuna Mfumo wa Tausi ambao uko kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa kwa maana ya halmashauri zetu. Vile vile, tuna Mfumo wa Bandari ambao unaitwa Terminal operating system, tuna GEPG nakadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mifumo hii yote inafanya kazi kubwa ya kukusanya mapato ya Taifa letu. Jambo kubwa la kufanya hapa ni kuhakikisha mifumo hii yote inakuwa imara ili kufikia malengo ambayo tumejiwekea kama Taifa katika kulifikia Pato la Taifa pamoja na kukuza uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa, uimara wa mifumo hii ni pamoja na kuhakikisha kwamba mifumo yote hii inasomana, kwa maana ya kwamba mifumo ya Serikali za Mitaa isomane na mfumo wa TRA, Bandari na mifumo yote. Kwa hiyo, tukiwekeza kwenye mifumo hii yote ikasomana nina imani kubwa kabisa haya yote tunayoyatarajia kama Taifa tutayafikia katika mwaka wa fedha 2024/2025. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo ningependa kuchangia ni upande wa sekta ya utalii. Sekta ya utalii inachangia takribani asilimia 14 kwenye Pato la Taifa. Vile vile, inachangia asilimia 25 ya fedha za kigeni hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa huu wa miaka mitano ambao tunao, wa mwaka 2021/2022 hadi 2025/2026, ukisoma ule ukurasa wa 102, mpango katika sekta ya utalii umeelekeza kwamba, kuendeleza mazao mapya ya utalii kwa ajili ya ukuaji wa uchumi. Pili, kuendeleza Kanda ya utalii kusini mwa Tanzania. Lengo ni kukuza sekta hii muhimu sana katika ukuaji wa uchumi kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2020/2025 kifungu kile cha 67 kwenye ukurasa wa 11, kimeweka malengo kwamba, kufikia wastani wa watalii milioni tano ifikapo 2025 lakini pia mapato kutokana na sekta hii ya utalii kufikia dola bilioni sita ifikapo 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo haya si rahisi kuyafikia bila kuwa na mipango thabiti kwenye mipango yetu ya Taifa. Mambo ya kufanya: -

(i) Kuhakikisha kwamba tunatangaza vivutio vyote ndani na nje ya nchi yetu ili kuvutia watalii wa kutosha katika Taifa letu na kuongeza Pato la Taifa. (Makofi)

(ii) Kushirikisha sekta binafsi katika uwekezaji hasa kwenye sekta ndogo ya malazi. Tunapozungumza kwenye sekta ya malazi katika Taifa letu kwenye sekta hii ya utalii tuna vitanda chini ya 150,000. Hivi ni vichache sana ukilinganisha na hali ya utalii pamoja na fursa zilizopo katika Taifa letu. Lakini nchi Jirani ya Kenya kuna vitanda zaidi ya milioni moja. Kwa hiyo, utaona jinsi ambavyo tuko nyuma katika kuwekeza kwenye sekta hii ya utalii, hasa hoteli zenye hadhi mbalimbali za kuhakikisha kwamba watalii wanafika kwenye nchi yetu na kuchangia Pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii ikiwekewa mikakati mizuri katika Mpango tunaopendekeza, kwanza itachochea ukuaji wa sekta yenyewe, pili, itapunguza nakisi ya urali wa malipo ya huduma, tatu, itaongeza mchango katika Pato la Taifa, kukuza uchumi na utalii katika Bajeti yetu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana Serikali katika mpango huu tunaupendekeza, tuhakikishe tunaweka mikakati mizuri sana katika sekta hii ya utalii ambayo ukiwekeza unapata fedha za kigeni mara moja, na haichukui muda mrefu. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri wetu wa Mipango mtu makini sana (Profesa) na Waziri wetu wa Fedha, mhakikishe kwamba kwenye Mpango huu unaokuja tuweke mikakati mizuri sana katika sekta hii muhimu sana ya utalii hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ni tathmini ya Mpango wa Tatu wa Maendelo ya Taifa huu wa miaka mitano 2021/2022 hadi 2025/2026. Ili ujue unakokwenda ni lazima ujue ulipotoka, ulipo, ili ujipange vizuri kwa safari ya mbele. Mpango huu unaopendekezwa ni Mpango wa nne ambapo tayari tumekwishatengeneza mipango mitatu. Kwa kuwa tumekwishatekeleza mpango huu zaidi ya nusu, kwa maana tayari tumekwishatekeleza mipango miatatu, iko haja ya kufanya tathmini ya vipaumbele vyote tulivyovipanga kwa miaka mitatu katika kila sekta tumekeleza kwa kiasi gani ili tujipange kwa mipango inayokuja. Kwamba ni wapi tumefeli, wapi tumefanikiwa ili tujipange vizuri katika mipango iliyobaki, kwa maana ya mpango wa nne na mpango wa mwisho, ule wa tano, wa 2025/2026. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungefanya midterm revue ya Mpango huu itasaidia sana kuona ni nini tumefanya, nini tumekwama wapi na kwa sababu gani? Mpango huu ni wa Mwisho kwa maana ya Dira ya 2025. Kwa hiyo, tukifanya tathmini ya uhakika kwa Mpango huu unaokwisha tutakuwa tumejenga msingi imara wa kuweka dira mpya ya 2050.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninaamini kabisa kwamba tukijipanga vizuri, nchi yetu ina fursa nyingi sana na Watanzania wako tayari kufanya kazi. Kazi kubwa ni kupanga na kusimamia fedha zote za uchumi hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa fursa; naunga mkono hoja, ahsanteni sana. (Makofi)