Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru. Naomba nitoe mchango wangu kwa kunukuu maneno ya hekima kutoka katika Quran Takatifu na Biblia. Katika Quran tunaambiwa Mwenyezi Mungu anasema, “Tutawanyanyua wale waliomwamini Mwenyezi Mungu na wale wenye elimu.” Kwenye Biblia tunaelezwa, “Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mataifa yaliyo makini na yanayotamani maendeleo ya haraka yamefanya uamuzi wa kimapinduzi kuwekeza kiasi kikubwa cha fedha katika sekta ya elimu hasa elimu ya sayansi na teknolojia. Hili halishangazi, ndiyo maana nchi kama India, China, Singapore, Vietnam na Korea Kusini zimepata maendeleo ya kupigia mfano katika miaka ya karibuni kwa sababu wamewekeza sana katika sekta ya elimu hasa teknolojia na sayansi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo letu kubwa ninaloliona kama Taifa, ninapoangalia mipango yetu ya maendeleo, tumeweka kiasi kikubwa sana cha fedha katika kutekeleza miundombinu. Naomba samahani sana, nadhani kwenye sekta ya elimu hasa sayansi na teknolojia hatujawekeza kiasi cha kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine linalotukwamisha kama Taifa hatuna mpango madhubuti wa usimamizi wa wafanyakazi na rasilimali watu kwa ujumla (human resource planning and management). Nitalifafanua jambo hili. Kila mwaka tunatenga zaidi ya shilingi bilioni 400 na mwaka huu 2023/2024 tumetenga shilingi bilioni 731 kwa ajili ya mikopo ya elimu ya juu. Tunatayarisha madaktari, wahandisi, walimu, lakini kwa bahati mbaya tukishawatayarisha hatuwaajiri tunawaacha wanazagaa kwenye mitaa. Haya ni matumizi mabaya sana ya rasilimali ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hapa kuna tatizo, ama mafunzo yanayotolewa ya shahada hayana ubora unaotakiwa wa kuwawezesha vijana wetu kujiajiri ama vijana wanalazimishwa kuchukua course ambazo hawana passion nazo, hawazipendi, ama wazazi wao wanawalazimisha, kama mzazi ni daktari anatamani na mwanaye awe daktari; kama mzazi ni mhasibu anatamani mwanaye awe daktari. Pia kuna tatizo kwenye vyuo vyenyewe. Kuna uchache wa course za uchaguzi. Kwa maana hiyo wanafunzi wanalazimika kuchukua na masomo ambayo pengine hawayapendi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ushauri wangu, nafikiri wakati umefika Serikali ingefanya maamuzi mahususi, tukafanya ukaguzi wa idadi ya wafanyakazi tunaoweza kuwaajiri, human resource audit ili tukawasomesha watu tunaoweza kuwaajiri na fedha zinazobaki tukazielekeza kwenye mafunzo ya ufundi stadi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa mafunzo ya ufundi stadi, nilikuwa na mawazo kidogo. Kuna tatizo hapa, mafunzo yanatolewa, lakini tatizo letu kama Taifa, vijana wote wa nchi nzima kuna mtaala mmoja tu wa elimu ya ufundi stadi. Hii nadhani siyo sawa, kwa sababu mahitaji ya binadamu ni tofauti, mazingira ya mwanadamu ni tofauti, kazi kuu inayofanyika kwenye jamii ni tofauti kati jamii moja na nyingine; hata rasilimali ni tofauti. Kwa maana hiyo, hatulazimiki kwamba lazima tuwe na mtaala mmoja. Kila wilaya iwe na mtaala unaolingana na mazingira yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, jamii ya wafugaji kwa nini hatuwafundishi ufugaji wa kisasa, ujasiriamali na namna bora ya kuzalisha mazao bora ya ufugali kama vile uzalishaji wa maziwa, utengenezaji wa jibini, utengenezaji wa samli, mtindi, nyama choma na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa watu wanafundishwa mambo ya jumla jumla tu. Jamii ya wavuvi tungefanya hivyo hivyo na jamii ya wafugaji nyuki tungefanya hivyo hivyo. Nadhani tukifanya hivyo bila shaka tija itaonekana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, nadhani mbali nakuwa na vyuo hivi vya VETA kila Wilaya, Serikali inapaswa kuwa na vyuo vichache sana vunavyofundisha masomo maalumu. Kwa mfano, teknolojia ya habari, mitambo inayotumia akili za bandia, uhandisi, nishati ya jua, teknolojia ya kilimo cha umwagiliaji maji na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazo langu la mwisho, Mipango yetu ya Maendeleo haitafanikiwa kama tunavyotarajia kama hatujawekeza kiasi cha kutosha katika sekta ya elimu. Kwa maoni yangu, nadhani sekta ya elimu inapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza. Kwa sababu karne zilizopita utajiri na ustawi wa mataifa ulipimwa kwa kutumia nguvu ya misuli, utajiri wa mafuta, madini na gesi. Katika karne ya 21 ustawi wa mataifa utapimwa kwa kutumia nguvu ya akili, maarifa na sayansi. Naomba nirudie katika karne ya 21 mapambano makubwa na hasa vita kati ya Taifa moja na lingine hayatapiganwa sana kwa kutumia mizinga na silaha tunazoziona, bali mapambano makubwa yatakuwa katika kutumia cyber, yani kutumia teknolojia ya Habari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, sisi kama Taifa watu wetu tuwaelekeze huko tu. Nadhani wakati umefika sasa Vyuo vyetu Vikuu na hasa vinavyofundisha mambo ya teknolojia na sayansi kwa ujumla, vinapaswa kuanzisha course maalum za teknolojia ya kidigitali, artificial intelligence na data science kama tunataka kuingia kwenye karne ya 21 kwa mbwembwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Naomba kuunga mkono hoja.