Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE.FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika taarifa ambazo zimetolewa leo katika Kamati zetu tatu za PAC, LAAC na PIC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu, tangu nimeingia hapa Bungeni nimeweza kutumika katika kamati hizi zote tatu. Kwa hiyo, ninao uelewa wa kutosha na nimezielewa vizuri taarifa ambazo zimetolewa leo, lakini kwenye taarifa zao zilizotolewa, nitachangia kidogo kwenye Kamati ya LAAC na nitachangia kwa upana zaidi kwenye Kamati ya PIC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kujikita kwenye eneo lile la matumizi yasiyo sahihi ya Force Account. Ni ukweli kwamba taratibu, kanuni na sheria zimekuwa hazizingatiwi katika matumizi ya Force Account.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna zile kamati ambazo huwa zinahusika na fedha, manunuzi na mapokezi ya vifaa. Zile Kamati zimekuwa dormant, hazifanyi kazi yake sawa sawa kama ambavyo Mheshimiwa Mpakate amezungumza muda mfupi uliopita. Kwa hiyo, zinatumika tu kuhalalisha mambo, lakini kazi yenyewe inafanywa kule Makao Makuu ya Halmashauri zetu. Kwa hiyo, kuna jambo hapa ambalo tunatakiwa tulifanye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ushauri uliotolewa na Kamati ya LAAC, nilikuwa nashauri kuwa Serikali yetu iangalie uwezekano wa kupanga viwango vya fedha zinazowekezwa kwenye mradi ambazo zitatumia aidha Force Account au wazabuni. Leo tumeona hata majengo ya Ofisi za Halmashauri zetu zenye thamani ya shilingi bilioni mbili, shilingi bilioni tatu na miradi mingine inaongezewa fedha, inakwenda mpaka shilingi bilioni nne hadi tano bado zinatumia Force Account. Hii ni hatari kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa napendekeza, mradi ambao unazidi shilingi milioni 200, usitumie utaratibu wa Force Account, kwa sababu zile fedha ni nyingi. Hizi fedha zikifika kule, fuatilieni tu, nakuomba Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na Waziri wa Fedha mweke utaratibu mzuri wa kuwa na zile technical audit kutoka Wizarani, mtashuhudia haya mambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zile shilingi milioni 470 ambazo tuliletewa kwenye miradi hii ya SEQUIP hazikumaliza ile miradi, na hata hizi zilizoletwa juzi za miradi ya BOOST shilingi milioni 331 kila jimbo hazijamaliza ile miradi. Unakuta mradi unatekelezwa asilimia 80 au 85 na ukizidi sana 95. Mwisho hii imekuwa ikitusumbua. Kipindi unapoenda kupanga matumizi ya fedha za Mfuko wa Jimbo, unakuta Mkurugenzi naye anakusogelea, analeta request ili akamalizie vyoo na huduma nyingine katika ile miradi. Kwa hiyo, imekuwa shida kweli kweli. Kwa hiyo, hapa tunapaswa kupaangalia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika yale marekebisho au maboresho ya utekelezaji wa miradi kupitia Force Account, nashauri kwamba tuzingatie viwango vya pesa vinavyowekezwa kwenye mradi, ikizidi shilingi milioni 200 tupeleke kwenye zabuni, na ikiwa chini ya hapo, kama ni kujenga madarasa, sijui kujenga ofisi za shule na vitu kama hivyo, hizo tunaweza kupeleka. Kujenga zahanati, tunaweza kutumia Force Account, lakini siyo miradi ambayo inagharimu fedha nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nije kwenye taarifa iliyotolewa na Kamati ya PAC. Nakwenda moja kwa moja kwenye ukurasa wa 31 na 46 kwenye kipengele Na. 2.4.7 na 3.2.10. Pale Kamati yetu ilizungumzia kutokamilika kwa miradi katika taasisi ambazo zinatumia mtaji wa umma kwa wakati. Jambo hili limejitokeza katika maeneo mengi na pale wame-cite mifano ya NSSF, katika ule mradi wa pale Mkulazi wamelazimika kuongeza fedha kiasi cha dola milioni 32, lakini kuna miradi ya RUWASA hasa ile inayotumia fedha za National Water Fund, imekuwa ni shida kweli kweli kumaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na shida kubwa na wakati mwingine fedha zinachelewa kuja na wakati mwingine mlolongo wa malipo unakuwa ni mrefu sana, hasa hizi fedha za wafadhili wa nje. Matokeo yake sasa mradi ukichelewa, unakuta bei ya vifaa inaongezeka, inflation inatokea, na riba inazaliwa kutoka kwa wakandarasi hasa wanapokuwa ni wa kutoka nje. Kwa hiyo, imekuwa ikileta shida kweli kweli na kufanya lile kusudio la Serikali la kuwekeza mitaji katika hizo taasisi kuwa halitekelezwi na mwisho wa siku ziada haizalishwi mapema kama ilivyokusudiwa, na mwisho wa siku kunakuwa na ufanisi mdogo katika utekelezaji wa ile miradi na vile vile tija inakuwa haipatikani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali iliangalie hili eneo ili tuweze kunasuka na hii hali ambayo imejitokeza. Pia naomba Serikali iongeze usimamizi wa hiyo miradi, lakini pale inapohitajika kupeleka fedha, basi zifike kwa wakati kwenye zile taasisi ili waweze kutekeleza hiyo miradi iliyokusudiwa ili ufanisi na tija viweze kupatikana katika uwekezaji wa hayo maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ambalo napenda kulizungumza ni suala la ongezeko la riba itokanayo na ucheleweshaji wa kulipa wakandarasi au wazabuni. Hili limekuwa jambo ambalo kama limezoeleka. Nataka nikwambie, jumla ya shilingi bilioni 63.77 ambazo zimeainishwa kwenye ukurasa wa 28 na 29 kwenye taarifa ya Kamati ya PIC, kama tungezinusuru kulipwa riba au tusingezigharamia kulipia riba, tungeweza kujenga vituo vya afya visivyopungua 127 kwa fedha zile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tungeweza kujenga zahanati zisizopungua 318 kwa thamani ya ile pesa ambayo inakwenda kutumika kwa ajili ya kulipa riba; tungeweza kujenga madarasa ya kisasa yenye thamani ya shilingi milioni 24 kila moja yasiyopungua 2,600; na pia tungeweza kujenga mabweni au maabara katika shule zetu za sekondari zisizopungua 1,822.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni fedha nyingi, lakini mwisho wa siku tumejikuta tunarudi nyuma kwa sababu tunatumia fedha nyingi kuwekeza katika maeneo ambayo tayari uwekezaji ulishafanyika kwa kuokoa hizo riba zinazotakiwa zilipwe na hazilipwi sasa. Kama tulikopa, unakuta hazilipwi na donors, inabidi tutafute chanzo kingine cha pesa kwa ajili ya kugharamia hayo malipo ya hao wakandarasi kutokana na kuchelewesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na sababu nyingi za ucheleweshaji, lakini leo hapa napenda nitanabahishe, niliwahi kufuatilia baada ya kuona ile hoja ya CAG na nikakuta kuna utaratibu ambao huwa unatumika katika malipo hasa kule kwenye upande wa barabara. TANROADS, wanatumia mfumo unaoitwa FIDIC, ule mfumo unataka malipo yakamilike ndani ya siku 56. Consultant na Mkandarasi wanatakiwa wafanye mambo yao ndani ya siku 28 na siku 28 inatakiwa taasisi zetu za Serikali kuanzia TANROADS pamoja na Wizara ya Kisekta, Wizara ya Ujenzi pamoja na Wizara ya Fedha waweze kufanya kazi zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANROADS ina mfumo wake mzuri wa malipo na udhibiti wa fedha na umekamilika kabisa, lakini utakuta TANROADS wanafanya procedure zao, lakini lazima iende Wizara ya Kisekta, Wizara ya Ujenzi. Pale kuna maafisa wasiopungua wawili, lazima wacheze na ule mfumo wa malipo. Ukienda Wizara ya Fedha utakuta zile transactions zinatakiwa zipite kwa Mkaguzi Mkuu wa Ndani, naye ana wasaidizi wasiopungua wawili; pia inatakiwa ipite kwa Kamishna wa Fedha za nje, naye ana wasaidizi wasiopungua watatu lazima wapitie hiyo transaction ya fedha; vile vile Kamishna wa bajeti naye lazima apitie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nasema hii milolongo imekuwa mirefu, naishauri Serikali ipunguze milolongo ya malipo ili tulipe kwa wakati, tupunguze hizi riba. Kama haitoshi, pia tuwe na mfumo wa kufuatilia kuona ni wapi kuna laxity katika kulipa haya malipo ambayo yanazalisha riba ili hizo fedha tuweze kuzi-save ziende zikafanye kazi nyingine kwa ajili ya maendeleo ya Taifa na ni fedha ambazo zinatokana na jasho la walipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja zote na taarifa zote zilizotolewa na Kamati zetu zote tatu za PIC, PAC pamoja na LAAC, ahsante sana.