Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi jioni hii kuchangia hoja iliyoko mezani. Kwanza naunga mkono hoja zote tatu, naomba Serikali ichukue hatua kwa sababu mengi yaliyoainishwa na Kamati zote ni ukiukwaji wa Sheria za Manunuzi na ukiukwaji wa taratibu za fedha kwa makusudi ili kujinufaisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili, nitaenda moja kwa moja kwenye Manunuzi ya Umma Sheria, Sheria Na. 410 ambayo kwa taarifa ya LAAC imeonesha Serikali kupata hasara ya zaidi ya shilingi 106,799,578,781. Ukitaka details nenda kwenye ukurasa wa 19 wa taarifa hii mpaka ukurasa wa 20. Kurasa hizo zinaeleza namna ya Serikali ilivyopoteza fedha hizi ambazo Dkt. Mama Samia Suluhu Hassan, ambaye ndiye Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ametoa fedha nyingi kupeleka kwa ajili ya miradi mbalimbali kwenye Halmashauri zetu, lakini watumishi ambao sio waadilifu wanataka kumuangusha kwa kuzitumia fedha hizi nje ya utaratibu na kazi zake nyingi hazijakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili hatuwezi kukwepa kwa kulaumu force account. Force Account kwenye maeneo mengi ya Halmashauri yetu imeshindwa kukidhi haja ya matumizi kwa makusudi na sio kwa bahati mbaya. Mwongozo unaeleza wazi kabisa namna force account inavyotakiwa kutumika; moja lazima Kamati ziundwe, Kamati zile na wataalam wapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya zile Kamati zimekuwa kama kiini macho katika maeneo mengi ambayo tumepita, kwa sababu majukumu yao hawafanyi kama ilivyoelekezwa kwenye mwongozo, kwa mfano, Serikali imepoteza zaidi ya shilingi 1,510,000,000 kwenye Halmashauri zetu kwa sababu ya kufanya malipo ya pesa taslimu kwenye mfumo huu wa force account bila kufuata utaratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo sio kwamba la bahati mbaya ni la makusudi kwa sababu Sheria ya Fedha inataka fedha yote ilipwe kupitia akaunti za wazabuni, lakini kwa kuwa wamekusudia kufanya hivyo basi wamelipa kwa taslimu ili kuepusha kutokupatikana fedha hizo kwa njia za vichochoroni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye force account wataalam wetu wanahusika na mara nyingi wanakwepa Kamati hizi ambazo zinahusishwa na wananchi wenyewe chini bila kufanya vikao ambavyo vinatakiwa kwa mujibu wa muongozo. Wakati mwingine wananchi Kamati zile wanaletewa bidhaa ambazo zimenunuliwa juu kwa juu, maana yake juu kwa juu wao wanaandika cheque huko huko, wanaandika muhtasari huko huko, wanasaini wenyewe kama Wajumbe wa Kamati, wananunua then wanaenda chini ambako ndiko waliko watekelezaji wa miradi wanawaambia andika check tunamlipa mtu fulani bila wao kuhusishwa kwenye mchakato mzima wa manunuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo limesababishia Serikali hasara kubwa sana kwenye force account kwa maana ya kwamba ukamilifu wa miradi hii matokeo yake haikamiliki kwa ukamilifu na utakuta miradi mingi imeacha bidhaa nyingi ambazo hazina matumizi. Cha ajabu TAMISEMI wanatoa muongozo wa namna ambavyo miradi ile inatakiwa kutekelezwa kwa maana ya BOQ ambayo imeandaliwa na TAMISEMI, ambako kuna ma-engineer na ma-professor.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda chini kwa watu wetu wa chini kuna Wahandisi ambao wamesoma zaidi, ambao wana-crush, wanaweka makisio ambayo yanazidi yale ambayo yametengenezwa na Wizara. Mfano mdogo sana, kwenye jimbo letu la Tunduru Kusini tukitumia mapato ya ndani, darasa moja tunajenga kwa milioni 12.5 pamoja na madawati, lakini Serikali inapeleka milioni 24. Darasa lile utakuta linafanana na lile la milioni 12.5, hakuna marumaru, hakuna kitu chochote. Hili jambo linafanya kwamba wenzetu Wahandisi wanaona kwamba pesa zinazoletwa na Mama ni kama zawadi kwa upande wao kwa kujinufaisha badala ya kuwanufaisha wananchi wetu kule chini ambao ndiyo wana shida kubwa ya madarasa, madawati, zahanati pamoja na vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili jambo, Halmashauri nyingi sana zimepata hasara katika mfumo wa ununuzi wa magari. Halmashauri zinaomba ununuzi wa magari GPSA, wanalipa pesa ambayo invoice yake inasoma kutoka original ya gari ni kutoka Japan, pesa wakilipa wanakaa zaidi ya mwaka mmoja au miaka miwili. CAG ameona namna ambavyo Halmashauri zinapata hasara, pesa ile inakaa kule haina riba lakini wanaenda kule kuletewa magari, magari yale badala ya kuwa original Japan, gari hili linakuwa original South Africa ambapo sisi wote tunanunua magari humu ndani, gari lililotengenezwa South Africa hata liwe Toyota na lililotengenezwa Japan bei zake ni tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya zaidi katika utofauti wa bei, hakuna Halmashauri yoyote ambayo imerejeshewa zile tofauti. Jambo hili Serikali iliangalie kuna jipu kwenye GPSA, kwa sababu ya manunuzi ya magari ya Halmashauri ambayo yanakaa kwa muda mrefu bila kurejeshewa na kupelekewa magari ambayo ni tofauti na ile invoice ambayo wameipeleka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine matumizi ya POS. POS ni nzuri sana katika kukusanya pesa bahati mbaya katika taarifa iliyotolewa na CAG, pesa nyingi zinakusanywa lakini hawazipeleki benki. Hili halifanywi kwa bahati mbaya, hawa wengi ni mawakala na wengine ni watumishi wa Halmashauri, lakini hawapeleki benki. Hili matokeo yake Wakurugenzi wanatumia kichaka hiki kuwapeleka PCCB hawa watu wanaokusanya hizi pesa ili kuendelea na mtindo wa kuchukua pesa bila kupeleka benki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatakiwa ichukue hatua kwenye jambo hili, kwa sababu limekuwa ni donda ndugu, sisi wataalam tunasema wanakula pesa mbichi. Matokeo yake Halmashauri inakusanya pesa nyingi, zinaishia mifukoni mwa watu na hazifanyi kazi zilizokusudiwa kwa ajili ya maendeleao ya watu wetu tunaowahudumia. Kwenye hili nalo Halmashauri zetu zimeshindwa kukusanya zaidi ya bilioni 37.34 kutokana na vyanzo vyao vya kila siku na vyanzo hivi vinaeleweka, kuna kodi ya vibanda vya masoko, stendi hizi zote zinakusanywa, lakini haziendi benki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine hata mikataba ya hivyo vibanda vya Halmashauri hawana na wakati mwingine mikataba hii imeisha na wakati mwingine mwenye leseni na mwenye mkataba kwenye vibanda hawaeleweki, kumbe wakati mwingine wafanyakazi pamoja na Madiwani wetu ndiyo wanaomiliki hivi vibanda, matokeo yake anapangishwa mtu mwingine, Halmashauri inapata hela kidogo. Mbaya zaidi kuna Halmashauri zimekosa hata rekodi ya vibanda walivyokuwa navyo, kwamba wana vibanda 100 wanatakiwa kukusanya Sh.50,000 kwa mwezi utapata milioni tano, lakini wao hizo taarifa hawana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa CAG ameliona hili, Serikali kwa maana ya TAMISEMI tulichukulie very serious kwa kuwachukulia hatua hawa wote ambao wanafanya mitindo hii, sio kwa bahati mbaya ni kwa makusudi ili wajinufaishe na Halmashauri zetu zinabaki kuwa tegemezi kutokana na mapato yao kuliwa na watu ambao sio watarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache naunga mkono hoja na naiomba Serikali, wote waliohusika kwenye hizi takataka zinazoonekana huku ndani [Maneno haya siyo sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

...wachukuliwe hatua, hiki kitendo cha kutokuwachukulia hatua ndiyo maana kila siku CAG anaandika yaleyale.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Daimu, naomba ufute maneno ya takataka.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nafuta kauli hiyo, ni kwamba hivi vitu ambavyo vinafanyika vya hovyo. (Kicheko)

MWENYEKITI: Malizia, muda wako umeisha.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, Ahsante sana. (Makofi)