Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na uzima, lakini kabla sijazungumza sana naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa namna ambavyo anatupelekea pesa nyingi sana za miradi ya maendeleo kwenye majimbo yetu. Pia ninampongeza Rais kwa namna ambavyo amekuwa akipeleka miradi hii kwa asilimia kubwa bila kubagua, hata sasa hivi sisi wa vijijini tumeanza kupata miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaelezea mfano mmoja wa mradi wa ujenzi kwa Kiingereza au tuseme Kisukuma ni Construction of Sports Center of Excellence katika Mji wa Malya katika Jimbo la Sumve. Mheshimiwa Rais alitupatia shilingi bilioni 31 kwa ajili ya mradi huo, Mheshimiwa Rais akiwa anaipokea timu ya Yanga alisisitiza kuhusu mradi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme kwamba nimezungumza mradi huo kwa kusudi moja, kila tunapokutana hapa kujadili ripoti ya CAG kazi yetu sisi hapa mara nyingi tumejikuta tukijadili madudu ambayo yamefanywa na watu tuliowaamini kusimamia mambo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya madudu yaliyosemwa na Kamati zote tatu, huwa yanatokana na mchakato, yaani watu huwa wanaanza kuzembea siku ya kwanza, siku ya pili, siku ya tatu mpaka linakuwa dudu, mwisho wa siku inakuwa hoja ya CAG tunakuja kujadili hapa.
Mheshimiwa Spika, nilitamani leo nitumie mradi huu kutengeneza utaratibu na kutengeneza mstari wa kuzuia hoja mpya za CAG. Ninazo documents hapa ambazo nilitamani niziweke mezani ambazo zitasaidia mimi katika kuchangia.

Mheshimiwa Spika, tarehe 06 Julai, 2023 Katibu Mkuu wa Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo, alisaini mkataba na kampuni ya CRJE East Africa wenye thamani ya shilingi bilioni 31 kwa ajili ya kujenga hiyo inaitwa Proposed Construction of Sports Center of Excellence to be building on plot Number 30, 31 and 32 at Malya Kwimba District. Katibu Mkuu akiwa hajafungwa pingu, akiwa na akili timamu na baada ya Serikali kupitia organs zake zote kufanya kila kilichotakiwa kufanyika alisaini huu mkataba.

Mheshimiwa Spika, tarehe 27, siku 21 baada ya kusaini huu mkataba Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela ikamwandikia Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ikimwambia kwamba; “Tunajibu barua yako ya tarehe 02 Juni, 2023 ya kutuomba eneo kwa ajili ya ujenzi wa hii sports…” mimi Kiingereza nilisoma mpaka Chuo Kikuu lakini kinanisumbuwa, yaani hii... (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, elimu yetu huko sisi tumesoma shule za ngumbaru, kwa hiyo… (Makofi)

SPIKA: Sema tu mradi.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, huu mradi wakieleza kwamba tunajibu barua yako ya tarehe 02 Juni, 2023 ya kutuomba eneo kwa ajili ya ujenzi wa huu mradi ambao siku 21 zilizopita Katibu Mkuu ameusaini kuujenga Malya - Sumve na Mheshimiwa Rais aliusema unajengwa Malya Sumve, Mheshimiwa Waziri aliyekuwepo Mchengerwa aliusema na Katibu Mkuu aliyekuwepo Dkt. Abbas alisema, lakini siku 21 baada ya kusaini, Ilemela inajibu barua iliyoandikwa kabla mradi haujasainiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia milolongo hii baadaye kuna barua nimeiweka humu ya consultant, Kampuni ya ABE, akimuandikia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo akimwambia kwamba; Ninarejea barua yako ya Tarehe 07 Septemba ya kuniomba ushauri kuhusu kubadilisha eneo la mradi. Yaani wameomba eneo kabla hata consultant hawajamshirikisha. Baada ya kuomba eneo na wameshasaini mkataba, wanamuomba consultant sasa awashauri. Consultant yeye hakukaa muda na hiyo barua, alikaa nayo kama siku tano akawaambia hili jambo haliwezekani, hili jambo mnaenda kuongeza gharama ya mradi, kubadilisha site ni ku-complicate mradi.. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, movement zote hizi zisizofuata utaratibu ndizo huwa zinazaa hoja za CAG, watu wanawekwa kwenye ofisi za Serikali badala ya kumsaidia Mheshimiwa Rais, alichowaambia wakafanye, wanaenda kufanya wanayofikiria kichwani kwao.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais amewaambia wapiga kura wake wa Sumve kwenye TV live kwamba tunajenga Malya, Serikali imesaini, mradi umeanza, Wizara ipo serious kuhamisha mradi huu kuliko walivyo serious kuhakikisha tunashiriki Kombe la Afrika. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nimeongea na Mheshimiwa Waziri kwa simu, nimeongea na Naibu Waziri na Katibu Mkuu wababe vibaya, wanazingua. Watu wa Sumve wanataka kuhamishiwa mradi wao majibu yao ni kwamba eti sisi tunakaa kijijini, mradi kama huu hauwezi kwenda kijijini. Malya kuna Chuo cha Michezo cha muda mrefu, unajenga chuo cha michezo bila kuweka shule ya mazoezi, ile ni shule ya mazoezi na Mheshimiwa Rais alitumia akili kuweka ule mradi, lakini wapo busy kuuhamisha. Wanaangaika na consultant aongeze gharama za mradi ilimradi watu wa Sumve wakose mradi waupeleke Ilemela. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kule Sumve, mimi naingia kwenye kashfa kwa ajili ya hawa jamaa…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, ninaanza kuonekana kwamba lile eneo la Ilemela ni eneo la Kasalali, ameuza, anatafuta hela za kampeni! Watu lazima waseme pembeni, kwa nini mradi uhamishwe kihuni namna hii!

SPIKA: Mheshimiwa Kasalali, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Tabasam.

TAARIFA

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nampa taarifa msemaji kwamba mradi huo kuhamishwa kwake tu, kupelekwa Ilemela unahitaji uongezewe shilingi bilioni 13! Yaani ni upigaji wa dhahiri wa mchana kweupe. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Kasalali Mageni, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, naipokea kwa mikono miwili, na nilikuwa hapa busy natafuta ukubwa wa eneo la Malya.

Mheshimiwa Spika, eneo ambalo sasa mradi unatakiwa uhamishwe lina square meter zaidi ya 100,000, unakopelekwa ni square meter 67,000 yaani haliruhusu hata uendelezaji.

Mheshimiwa Spika, Kamati yako ya Bunge inayoshughulika na mambo haya ilikuja mpaka Sumve na ikaona mradi huu una maana na ikatuambia kwamba tuendelee, ikaiambia Serikali mnafanya vizuri endeleeni, leo Kamati ya Bunge inataka ionekane imesema uwongo kwa sababu kuna Waziri tu jeuri anataka awaoneshe yeye ni jeuri, anajua kufanya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuendelea namna hii, Kamati ya Bunge imekuja, Mheshimiwa Rais amesema, Mheshimiwa Waziri aliyekuwepo na Katibu Mkuu wamesema na sisi Wabunge tumezunguka tunawaambia watu kwamba hiki kinafanyika, halafu mtu mmoja anakuja anasema kule ni kijijini, hawawezi kuwekewa mradi, ifike wakati muelewe nchi hii tuna usawa, watu wa Sumve hatuna lami sawa, hatuna hata milimita moja ya lami sawa, tumekubali. Maji ya Ziwa Victoria yapo Mwanza lakini Sumve hayajafika, sawa tumekubali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna Kituo cha Michezo na chenyewe mnakipeleka Ilemela, this is not fair, haiwezekani! Kwa utashi wa mtu mmoja wanajifanya hapa wanashauriana na consultant, sijui kulikuwa kuna consultation team na nini, ni ujanja ujanja tu huu. Ndiyo mambo aliyokuwa anasema Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati anapokea Ripoti ya Ardhi Mwanza. Barua zina backdate watu wana-backdate barua ili kuweka mambo yasiyoeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naunga mkono hoja za Kamati zote tatu na naomba niongeze Azimio la kwamba hawa wanaotaka kuhamisha miradi na kutengeneza hoja za CAG, washughulikiwe kama wahalifu wengine na nipo tayari kuonesha ushirikiano kwenye hili. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, naomba kushukuru. (Makofi)