Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na afya na kutuwezesha kukusanyika katika Bunge hili la Kumi na Moja la Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa vile ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge hili la Kumi na Moja, naomba nichukue fursa hii kuwashukuru sana wapiga kura wa Jimbo la Bagamoyo kwa kunipa fursa nyingine ya kuwaongoza kama Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo. Niwaahidi tu kwamba nitawatumikia kwa juhudi zangu zote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchukua fursa hii kuipongeza sana Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango kwa hoja hii ambayo imewasilishwa ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa mwaka 2016/2017. Niipongeze Serikali kwa kutoa kipaumbele kwa ujenzi wa viwanda kama mkakati maalum wa kuendeleza ujenzi wa uchumi wa viwanda kwa nchi yetu. Huu ni mkakati sahihi ambao unajipanga moja kwa moja kupiga vita umaskini katika nchi yetu na mkakati ambao utawezesha kuzalisha ajira nyingi na kuwaondoshea kadhia vijana wetu wa kiume na wa kike ambao wanahitimu katika vyuo vyetu mbalimbali na shule mbalimbali, wanaingia katika soko la ajira na kukosa ajira. Niwapongeze kwa hilo, huu ni mkakati sahihi ambao tukienda kwa kasi hii kwa miaka mitano bila shaka nchi yetu itakuwa katika hali nyingine kabisa na kujenga maisha bora kwa kila Mtanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa viwanda huu utatumia malighafi za ndani za kilimo, mifugo, misitu na uvuvi lakini viwanda pia vitazalisha bidhaa kadha wa kadha ambazo tunazihitaji kwa ajili ya matumizi ya wananchi wetu. Pia zitazalisha ajira kama nilivyosema hapo awali lakini pia viwanda hivi vitawezesha kulipa ushuru na kodi mbalimbali ambazo ni fedha nyingi zitakazowezesha Serikali yetu kuwa na mapato makubwa zaidi na kuiwezesha Serikali kuweza kumudu huduma za jamii katika nchi yetu. Sina namna bali kuunga mkono na kupongeza juhudi hii katika Mpango huu wa Maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuikumbusha Serikali yangu kupitia Wizara ya Fedha na Mpango kwamba wakati tunaweka mkazo huu wa ujenzi wa viwanda, tufahamu kwamba viwanda hivi hivi vinajengwa ardhini. Kwa hiyo, jambo muhimu sana katika Mpango huu ni kuhakikisha kwamba Serikali inamiliki ardhi ili iweze kujenga viwanda hivi. Maeneo yote yale ambayo tunahitaji kujenga viwanda katika mwaka huu unaofuata wa fedha Serikali ijitahidi kuhakikisha kwamba ardhi ile imemilikiwa na Serikali ili mkakati mzima wa ujenzi wa viwanda usije ukaingia katika matatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimboni kwangu Bagamoyo tuna mpango maalum wa uwekezaji ama SEZ ambao unajumuisha ujenzi wa viwanda na Bandari ya Mbegani. Katika eneo hili, Serikali tayari imeshatambua eneo la ujenzi wa viwanda hivyo au eneo la uwekezaji. Mwaka 2008 uthamini wa ardhi umefanywa na jumla ya shilingi bilioni 60 zinahitajika kulipwa fidia, lakini hivi sasa mwaka 2016 katika shilingi bilioni 60 zile bado wananchi wanadai shilingi bilioni 47 kwa maana asilimia kubwa ya wananchi bado hawajalipwa fidia. Huu ni mwaka tisa wananchi hawajalipwa fidia lakini mwaka wa tisa pia tumepoteza fursa kadhaa za uwekezaji wa viwanda kwa vile wawekezaji hawatoweza kuweka viwanda ardhi haipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni miaka tisa ambayo tumepoteza ushuru na kodi mbalimbali lakini miaka tisa pia ambayo tulipoteza fursa za ajira mbalimbali kama viwanda vingekuwa vimejengwa. Kwa hiyo, naomba niikumbushe Serikali yangu katika mkakati huu na Mpango huu wa maendeleo kuweka mkazo wa kumaliza ulipaji wa fidia kwa wananchi wa Bagamoyo ambao wamekuwa tayari kutoa maeneo yao kwa ajili ya ujenzi wa viwanda na ujenzi wa bandari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo wezeshi la ujenzi wa viwanda ni ujenzi wa bandari. Nashukuru Serikali katika Mpango huu wa Maendeleo ukurasa wa 28 umeonyesha kwamba Serikali itajipanga kujenga bandari mpya ya Mwambani Tanga na Mbegani Bagamoyo. Hii ni fursa kubwa ya kiuchumi, bandari ni fursa pekee za kiuchumi ambazo mataifa mengine yametumia vizuri kama Singapore na nchi zingine na kuwawezesha kujenga uchumi mkubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niihamasishe Serikali yangu kwamba katika Mpango huu tusichukue muda mrefu na hasa pale ambapo mkataba wa ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo umeshasainiwa kati ya nchi yetu na nchi rafiki ya China na Oman. Wenzetu hawa hawatapenda kupoteza muda. Kwa hiyo, tujipange vizuri sana katika mwaka wa fedha unaofuata kuhakikisha kwamba maandalizi ya ujenzi wa bandari ya Bagamoyo yanakamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema awali kwamba viwanda hivi na bandari hizi zinajengwa katika ardhi, wananchi katika Jimbo langu la Bagamoyo eneo ambalo litajengwa bandari, wananchi wa Pande na Mlingotini wako tayari hivi kuhama ili kupisha ujenzi wa bandari hiyo. Haikuwa rahisi sana wao kukubali lakini kwa sababu ya maendeleo ya Taifa letu wamekubali wahame kwa ajili ya kupisha ujenzi huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari eneo limetengwa shamba la Kidagoni ambalo awali lilikuwa shamba la NAFCO lakini sasa lina mwekezaji binafsi. EPZ tayari imelianisha shamba hilo kwa ajili ya kuingizwa kwenye mradi wa uwekezaji. Tatizo ni kwamba ardhi hiyo inalazimika iweze kulipiwa fidia ili wananchi hawa waondoke katika maeneo ya ujenzi wa bandari wakabidhiwe eneo lingine na wao wako tayari kuhama hata leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa kilio chao kikubwa ni kwamba wana ndugu zao, jamaa na marafiki ambao wanaondoka duniani, hawapendi kuwazika pale Pande na Mlingotini kwa vile ardhi hii sasa hivi itachukuliwa kwa ajili ya bandari lakini hawana namna ya kwenda Kidagoni kabla Serikali haijalipa fidia ya Kidagoni ili wakabidhiwe eneo hilo. Naiomba Serikali yangu Tukufu ijitahidi haraka na kuweka msisitizo wa kuhakikisha kwamba katika mwaka wa fedha unaokuja mapema iwezekanavyo shamba lile liwe limelipiwa fidia na wananchi wa Pande na Mlingotini waweze kuhamia katika eneo hilo na ujenzi wa bandari usiweze kuchelewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine la uwezeshaji kwa uchumi wa viwanda ni nishati. Nimefurahi kwamba katika Mpango huu wa Maendeleo, nishati imeainishwa vizuri na msisitizo mkubwa umewekwa katika usambazaji wa nishati katika nchi yetu kuwezesha viwanda na wananchi kuweza kubadili hali ya maisha yao kupitia nishati na hasa nishati ya kutumia gesi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kimoja ambacho napenda kuikumbusha Serikali katika ukurasa ule wa 25 umeonyesha kwamba kutakuwa na mkakati wa kujenga miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia katika Mikoa ya Lindi, Mtwara na Dar es Salaam, nilichokishangaa Mkoa wa Pwani haukutajwa na Mkoa wa Pwani kuna ugunduzi wa gesi mpya Mkuranga na Bagamoyo. Gesi hii imegunduliwa na uchumi wa gesi ni uchumi mkubwa utatuwezesha kuongeza rasilimali, kuongeza fedha katika Serikali yetu na kutuwezesha sisi kuweza kupiga hatua kubwa za maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali inajumuisha katika Mpango huu mradi wa uendelezaji wa gesi Bagamoyo, Mkuranga na maeneo mengine ya Pwani lakini pia uelimishaji wa wananchi katika Mkoa wetu wa Pwani ili waweze kushiriki vizuri katika uchumi wa gesi katika nchi yetu. Tuepukane na fujo ambazo tulizipata huko awali ambazo zilitokana pia na wananchi kutokuwa na elimu. Tuhakikishe kwamba Mpango huu unajumuisha maendeleo ya gesi katika maeneo yetu Bagamoyo, Mkuranga na maeneo mengine ya Mkoa wa Pwani ili tuweze kupiga hatua kubwa zaidi za maendeleo. (Makofi)
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu umeisha, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)